Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
Dkt. Harrison Mwakyembe akiwasilisha bajeti ya Wizara hiyo Bungeni jijini
Dodoma ambapo ameomba kutengewa kiasi
cha sh. bilioni 40.1 kwa mwaka wa fedha 2020/2021.
Mbunge wa Chemba Juma Nkamia akichagangia hoja
wakati wa kujadili bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa
mwaka wa fedha 2020/2021.
Wabunge wakiendelea na mjadala wa bajeti ya
bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2020/2021.
Watendaji wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo wakifuatilia mjadala wa hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa
fedha 2020/2021 bungeni Jijini Dodoma.
(Picha na Eleuteri Mangi-WHUSM, Dodoma)
Na Eleuteri Mangi-WHUSM, Dodoma
Bajeti ya Wizara ya Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 imeongezeka hadi
kufikia kiasi cha sh. bilioni 40.1 kutoka sh. Bilioni 30.9 kwa mwaka wa fedha
uliopita ili kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
Akiwasilisha hotuba ya Bajeti
hiyo Bungeni Jijini Dodoma, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt.
Harrison Mwakyembe amesema kuwa ongezeko la sh. bilioni 9.2 ambalo ni sawa na zaidi ya
asilimia 29.2 itaenda kutekeleza miradi ya maendeleo.
“Katika mwaka wa fedha ujao fedha
zitaenda kutekeleza miradi ya maendeleo ikiwemo Programu ya Urithi wa Ukombozi
wa Bara la Afrika yenye kiasi cha sh. milioni
515, Chuo cha Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) kilichotengewa sh. milioni
250 kwa ajili ya ukarabati wa chuo hicho pamoja na Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya kiasi cha
sh. milioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa, mabweni pamoja na
viwanja vya michezo”, alisema Mhe.Mwakyembe.
Dkt. Mwakyembe ameongeza kuwa miradi
mingine itakayotekelezwa ni ujenzi wa eneo Changamani la michezo Dar es Salaam
na Dodoma ambao umetengewa kiasi cha sh. milioni 650, mradi wa upanuzi wa
usikivu redio za TBC Taifa na TBC FM ambao umetengewa kiasi cha sh. bilioni 5
pamoja na mradi wa Habari kwa Umma ambao umetengewa kiasi cha sh. bilioni 1 inayofanya
miradi yote kutekelezwa kwa jumla ya sh.
bilioni 7.7.
Akizungumzia sekta ya michezo, Mhe.Waziri
amesema kuwa ni sekta ambayo inaimarisha
afya na kulitangaza Taifa ndio maana leo nchi inasikika katika matangazo ya
Premier League na UEFA kupitia vijana wanaocheza michezo ya kulipwa nje ya nchi
akiwemo Mbwana Samatta pia mafanikio ya
timu ya wanawake ya mpira wa miguu.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa
Wizara hiyo, Dkt.Hassan Abbasi amesema kuwa Serikali imefanya mambo makubwa kwa
sekta za Wizara hiyo muhimu kwa nchi, na fedha zilizopitishwa zitaenda
kuboresha mkakati wa kuitangaza lugha ya Kiswahili ambayo ni bidhaa adhimu Duniani
kwa kuwekeza kununua vifaa vya ukalimani, kufundisha wakalimani, kutengeneza
vitabu ambavyo vitakuwa ni miongozo ya ufundishaji wa lugha ya Kiswahili kwa
wageni.
“Kwa mara ya kwanza tumepata
bajeti kwa ajili ya taasisi yetu ambayo ni Kampuni yetu ya Magazeti ya Serikali
(TSN) ambayo kwa miaka mingi ilikuwa inajitegemea na kujiendesha kibiashara
lakini kwa sasa Serikali imefanya uamuzi TSN watalipwa mishahara na Serikali
ili waweze kuwekeza katika maeneo mengine”, alisema Dkt. Abbasi.
Aidha, Dkt. Abbasi alifafanua
kuwa mafanikio yaliyopo katika Wizara hiyo yametokana na ushirikiano ambao
inaupata kutoka kwa wadau mbalimbali wakiwemo vyombo vya habari na wanahabari,
wasanii, wanautamaduni na wanamichezo wote nchini.
Akichangia mjadala wa bajeti
hiyo, Mhe. Amina amesema kuwa usimamizi mzuri
na utekelezaji wa majukumu ya Wizara hiyo umefanya sekta zake zifanye
vizuri ikiwemo sekta ya habari ambayo tofauti na nchi nyingi Duniani, Tanzania
ina jumla ya televisheni zilizosajiliwa 44
pamoja na vituo vya redio 186.
Kwa mwaka wa fedha 2020/2021,
Wizara inatarajia kukusanya jumla ya shilingi
960,000,000 kupitia Idara ya
Habari - MAELEZO na Maendeleo ya Michezo, kwa upande wa Taasisi
saba zilizo chini ya Wizara, kiasi
kinachokadiriwa kukusanywa ni jumla ya shilingi 40,171,264,000.
No comments:
Post a Comment