Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Akijumuika na Viongozi wa Serikali katika Dua Maalum ya Kumuombea Rais wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume Iliofanyika Katika Kaburi la Marehemu Viwanja Vya Afisi Kuu ya CCM Zanzibar.


Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh. Saleh Omar Kabi akisoma Dua Maalum ya kumuombea Rais wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, ilifanyika katika viwanja vya kaburi la marehemu Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dk. Ali Mohamed  Shein leo amejumuika na viongozi  wa Serikali pamoja na viongozi wa madhehebu mbali mbali ya Dini katika dua ya kumbukumbu ya muasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar, marehemu mzee Abeid Amani Karume.

Hafla hiyo ilifanyika kwenye Kaburi la kiongozi huyo liliopo Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui, ambapo viongozi wa madhehebu mbali mbali ya dini walipata fursa ya kumuombea dua marehemu.

Akifungua dua ya kiislamu, Mufti wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kaabi alimtakia malazi mema kiongozi huyo na kusema wakati wa uhai wake akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Marehemu alizingatia umuhimu wa kuweka hali sawa za wananchi wake pamoja na kuhakikisha wanaishi katika makaazi bora.

Alimuomba Mwenyezi Mungu kuinusuru Zanzibar na dunia kwa ujumla ili kuondokana na maradhi ya Corona yaliosambaa Ulimwenguni.

Nae, Kiongozi wa Kanisa la Anglicana Zanzibar, Askofu Michael Henry Hafidh alimtakia msamaha, rehema na amani kiongozi huyo katika malazi yake, sambamba na kumuomba Mwenyezi Mungu kubainisha njia ya kuondokana na ugonjwa wa Corona ulioikumba Dunia.

Aidha, Kiongozi wa jamii ya Kihindu Yoges Pirocit alitumia fursa hiyo kumuombea dua na kumtakia rehma kiongozi huyo.

Dua ya kumbukumbu ya Marehemu Abeid Amani Karume, ambayo kwa kawaida hufanyika kila kifikapo April 7 ya kila mwaka, ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Serikali, akiwemo Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Majaliwa Kassimu Majaliwa, Viongozi wakuu wa Kitaifa wastaafu akiwemo Dk. Amani Abeid Karume pamoja na baadhi ya Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Wengine waliohudhuria dua hiyo ni Kiongozi wa Mabalozi wadogo waliopo Zanzibar George Augostino, Mwakilishi wa Familia ya Marehemu Balozi Ali Karume, Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee, Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Sadalla ‘Mabodi’.

Aidha, wengine  ni pamoja na Kamanda Brigedia JWTZ Zanzibar Fadhil Omar Nondo, Kamishna wa Polisi Zanzibar Mohamed Hassan, Mwenyekiti Idara Maalum SMZ, Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi Hassan Khatibu pamoja na Wawakilishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na Viongozi mbali mbali wa vyombo vya Ulinzi na Usalama vya SMZ na SMT.

Dua ya kumbukumbu ya Marehemu mzee Abeid Amani Karume mwaka huu imehusisha washiriki wachache, ikiwa tofauti na ilivyozoeleka  ambapo wananchi na waumini walipata fursa ya kushiriki na kusoma khitma, hatua hii ikiwa ni juhudi za kukabiliana na maambukizo ya virusi ya Corona vinavyoendelea kusambaa duniani kote.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.