Na
Mbaraka Kambona, Tabora
Mkurugenzi
wa Idara ya Uzalishaji na Masoko, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Felix
Nandonde amewahimiza wafugaji nchini kufanya ufugaji wa kisasa, wenye tija na
kuachana na ufugaji wa kienyeji ambao
tija yake ni ndogo.
Dkt.
Nandonde aliyasema hayo katika uzinduzi wa zoezi la kuhamasisha upandikizaji wa
mbegu bora kwa ng’ombe jike
lililofanyika katika Wilaya ya Uyuhi, Mkoani Tabora Mwishoni mwa wiki
(Julai 30, 2020).
Akiongea
baada ya kuzinduliwa kwa zoezi hilo ambalo linategemewa kufanyika nchi nzima,
Dkt. Nandonde alisema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetenga
kiasi cha shilingi milioni 145 kwa ajili ya kuhamasisha wafugaji kuboresha
mifugo yao kwa kufanya ufugaji wa kisasa ikiwemo kutumia mbegu bora za mifugo.
“Mkakati
wa Wizara kwa mwaka huu wa fedha (2020/ 2021) ni kufanya upandikizaji wa mbegu
bora kwa ng’ombe jike milioni tatu (3)
ili tuweze kupata ndama bora walau milioni moja,”alisema Dkt. Nandonde
“Lengo
la zoezi hili ni kuwahamasisha wafugaji kufanya ufugaji wa kisasa ili wawe na
ng’ombe bora watakaowawezesha kujiongezea kipato na kuboresha maisha ya mtu
mmoja mmoja na kaya,”aliongeza Dkt. Nandonde
Aidha,
Dkt. Nandonde alisema kuwa ili wafugaji waweze kuwa na mifugo bora ni muhimu
sasa kuachana na ufugaji wa kienyeji na kufanya ufugaji wa kisasa kwa
kuzingatia kuwa na malisho bora kwa ajili ya mifugo yao, kuzingatia chanjo za
mifugo ili kuwalinda na magonjwa na eneo bora la kufugia.
“Serikali
ya awamu ya tano imehamasisha ujenzi wa viwanda vya nyama hivyo hii ni fursa
nzuri kwa wafugaji kuitumia katika kuboresha kipato chao kwa kuwa na mifugo
bora itakayowapatia mazao bora kwa ajili ya kupeleka katika viwanda hivyo na
kujipatia kipato cha uhakika,”alifafanua Dkt. Nandonde
Naye,
Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Msalika Makungu alisema kuwa zoezi hilo la
kupandikiza mbegu bora litaleta tija kubwa kwa wafugaji kwa sababu litawafanya
wawe na mifugo bora itakayowaongezea kipato chao binafsi na hata Mkoa.
“Mabadiliko
ya tabia nchi yanayoendelea kutokea hayatoi fursa tena kwa ufugaji wa kienyeji,
njia pekee itakayowafanya wafugaji waendelee kubaki katika sekta hiyo ni
ufugaji wa kisasa, waachane na mtindo wa kuwa na kundi kubwa la mifugo na wawe
na kundi dogo lenye tija kubwa,”alisema Makungu.
No comments:
Post a Comment