Rais wa Jamhuri ya Uganda, Yoweri Kaguta Museveni akitowa salamu na kuzungumza na Wananchi wa Tanzania katika hafla ya kuapishwa kwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli . iliofanyika katika uwanja wa Jamuhuri Jijini Dodoma jana 5/11/2020.
Na. Anitha Jonas – MAELEZO Dodoma. 05/11/2020.
Marais waliyohudhuria sherehe za kuapishwa Rais wa Jamhuri wa
Muungano wa Tanzania, Dkt.John Pombe Magufuli
wampongeza kwa ushindi wa kishindo katika Uchaguzi Mkuu uliyofanyika
hivi karibuni pamoja na kuwapongeza watanzania
kwa kumaliza zoezi hilo kwa amani.
Akizungumza katika sherehe
hizo, Rais wa Jamhuri ya Uganda, Yoweri Kaguta Museveni alisisitiza kuwa
ushiriki wa nchi mbalimbali za Afrika katika
sherehe hiyo ni matunda ya msimamo thabiti wa Hayati Baba wa Taifa Mwl.Julius
Kambarage Nyerere na baadhi ya
viongozi wa Afrika ambao hawakukubali
kuwa vibaraka wa mataifa ya nje.
“Napenda kutoa pongezi kwa
watanzania kwa kufanya uchaguzi salama na kumaliza bila vurugu zozote pia na
toa pongezi kwa Rais Magufuli kwa ushindi wa kishindo kwani ameshinda kwa kura
nyingi pamoja na wabunge mbalimbali wa chama cha CCM nao nimewaona wameshinda
kwa kura nyingi, nilikuwa nikifuatilia matangazo ya matokeo ya uchaguzi kupitia
televisheni ya TBC 1,” alisema Museveni.
Pamoja na hayo naye Rais wa
Comoro, Azali Assoumani alitoa pongezi kwa Rais Magufuli huku
akisisitiza kumuombea katika majukumu yake
aliyopewa ya kuwatumikia na kuwaongoza Watanzania ili aweze kukamilisha kazi hiyo kama ilivyo desturi ya viongozi kutekeleza wajibu wao kwa ufanisi
kwa msaada wa Mungu.
Naye Rais wa Jamhuri ya Zimbabwe, Emmaerson
Mnangagwa alitoa pongezi kwa watanzania na kutoa
salamu kutoka wananchi wa Zimbambwe
ambapo alisisitiza kuwa Zimbabwe wanaiangalia Tanzania kama baba na mama wa
uhuru wa taifa lao kama alivyowasisi Hayati Mwl. Julius Nyerere.
“Tunamshukuru sana Rais wa
Jamhuri ya Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu katika kipindi
alichokuwa Mwenyekiti wa SADC alikuwa
kinara wa kusimamia kuondolewa kwa
vikwazo mbalimbali ambavyo Zimbabwe
tulikuwa tumewekewa kwa kutangaza tarehe 25 Oktoba,2020 kuwa siku maalum ya
kupinga vikwazo hivyo ikiwa ni maamuzi ya
Jumuiya ya SADC,” alisema Rais Mnanangwa.
Halikadhalika nae Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Botswana , Slumber Tsogwane alitoa salamu kwa niaba ya Rais wake Mokgweetsi Masisi kwa kumpongeza Rais Magufuli kwa ushindi wa kishindo huku akieleza sababu mbalimbali zilizomfanya rais wake ashindwe kushiriki sherehe hiyo kwa kubanwa na majukumu ya kitaifa, pamoja na hali ya kuhitajika kukaa karantini mara baada ya kurejea nchini kwa siku kumi na nne atakapotoka nje ya nchi kutokana na hali ya ugongwa wa Corona .
Aidha, Katika sherehe hizo
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli aliwashukuru watanzania kwa kujitokeza kumpigia
kura kwa wingi na kumpa ushindi wa kishindo na alisisitiza kuwa uchaguzi kwa
sasa umekwisha na hivyo ni wakati wa kuchapa kazi na kulijenga taifa.
“Napenda kuwapongeza viongozi wote wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)
kwa kusimamia zoezi la uchaguzi vyema na kuhakikisha linaendeshwa kwa uwazi na haki, pia
nawashukuru watanzania wote kwa kuwa
wazalendo na kulinda amani ya taifa na mara
baada ya uchaguzi,” alisema Rais Magufuli.
Akiendelea kuzungumza mara
baada ya uapisho huo, Rais Magufuli aliahidi kuendelea kusimamia miradi mikubwa
yote aliyoianzisha na kutekeleza mingine mipya pamoja na kuimarisha usimamizi
wa rasilimali za taifa na kukuza uchumi, ikiwemo kutatua changamoto ya ajira
kwa vijana pamoja na mapambano dhidi ya rushwa.
Sherehe hizo za uapisho
zilihudhuriwa na Marais watatu, Mabalozi takribani themanini, viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Waziri wa Mambo ya Nje wa
Qatar na viongozi mbalimbali kutoka nchi za Afrika wakiwemo mawaziri wa nchi
mbalimbali na viongozi wa mashirika ya kimataifa.
No comments:
Post a Comment