Habari za Punde

Marais wa Afrika wampongeza JPM kwa Ushindi wa Kishindo

 

Rais wa Jamhuri ya Uganda, Yoweri Kaguta Museveni  akitowa salamu na kuzungumza na Wananchi wa Tanzania  katika hafla ya kuapishwa kwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli . iliofanyika katika uwanja wa Jamuhuri Jijini Dodoma jana 5/11/2020. 

Na. Anitha Jonas – MAELEZO Dodoma. 05/11/2020.

Marais waliyohudhuria  sherehe za kuapishwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dkt.John Pombe Magufuli  wampongeza kwa ushindi wa kishindo katika Uchaguzi Mkuu uliyofanyika hivi karibuni pamoja na kuwapongeza watanzania  kwa kumaliza zoezi hilo kwa amani.

Akizungumza katika sherehe hizo, Rais wa Jamhuri ya Uganda, Yoweri Kaguta Museveni alisisitiza kuwa ushiriki  wa nchi mbalimbali za Afrika katika sherehe hiyo ni matunda ya msimamo thabiti wa Hayati Baba wa Taifa Mwl.Julius Kambarage Nyerere  na baadhi ya viongozi  wa Afrika ambao hawakukubali kuwa vibaraka wa mataifa ya nje.

“Napenda kutoa pongezi kwa watanzania kwa kufanya uchaguzi salama na kumaliza bila vurugu zozote pia na toa pongezi kwa Rais Magufuli kwa ushindi wa kishindo kwani ameshinda kwa kura nyingi pamoja na wabunge mbalimbali wa chama cha CCM nao nimewaona wameshinda kwa kura nyingi, nilikuwa nikifuatilia matangazo ya matokeo ya uchaguzi kupitia televisheni ya TBC 1,” alisema Museveni.

Pamoja na hayo naye Rais wa Comoro,  Azali Assoumani  alitoa pongezi kwa Rais Magufuli huku akisisitiza kumuombea katika majukumu yake  aliyopewa ya kuwatumikia na kuwaongoza Watanzania ili aweze kukamilisha  kazi hiyo kama ilivyo desturi  ya viongozi kutekeleza wajibu wao kwa ufanisi kwa msaada wa Mungu.

Naye  Rais wa Jamhuri ya Zimbabwe, Emmaerson Mnangagwa  alitoa pongezi  kwa watanzania  na kutoa  salamu kutoka wananchi wa  Zimbambwe ambapo alisisitiza kuwa Zimbabwe wanaiangalia Tanzania kama baba na mama wa uhuru wa taifa lao kama alivyowasisi Hayati Mwl. Julius Nyerere.

“Tunamshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu katika kipindi alichokuwa Mwenyekiti wa SADC  alikuwa kinara wa kusimamia kuondolewa  kwa vikwazo  mbalimbali ambavyo Zimbabwe tulikuwa tumewekewa kwa kutangaza tarehe 25 Oktoba,2020 kuwa siku maalum ya kupinga vikwazo hivyo ikiwa ni  maamuzi ya Jumuiya ya SADC,” alisema Rais Mnanangwa.

Halikadhalika nae Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Botswana , Slumber Tsogwane alitoa salamu kwa niaba ya Rais wake Mokgweetsi Masisi kwa kumpongeza  Rais Magufuli  kwa ushindi wa kishindo  huku akieleza sababu mbalimbali zilizomfanya rais wake ashindwe kushiriki sherehe hiyo  kwa kubanwa na majukumu ya kitaifa, pamoja na hali ya   kuhitajika kukaa karantini mara baada ya kurejea nchini kwa siku kumi na nne atakapotoka nje ya nchi kutokana na hali ya ugongwa wa Corona .


Aidha, Katika sherehe hizo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli  aliwashukuru watanzania kwa kujitokeza kumpigia kura kwa wingi na kumpa ushindi wa kishindo na alisisitiza kuwa uchaguzi kwa sasa umekwisha na hivyo ni wakati wa kuchapa kazi na kulijenga taifa.

“Napenda kuwapongeza  viongozi wote wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa kusimamia zoezi la uchaguzi vyema na kuhakikisha  linaendeshwa kwa uwazi na haki, pia nawashukuru watanzania wote  kwa kuwa wazalendo na kulinda amani ya taifa na  mara baada ya uchaguzi,” alisema Rais Magufuli.

Akiendelea kuzungumza mara baada ya uapisho huo, Rais Magufuli aliahidi kuendelea kusimamia miradi mikubwa yote aliyoianzisha na kutekeleza mingine mipya pamoja na kuimarisha usimamizi wa rasilimali za taifa na kukuza uchumi, ikiwemo kutatua changamoto ya ajira kwa vijana pamoja na mapambano dhidi ya rushwa.

Sherehe hizo za uapisho zilihudhuriwa na Marais watatu, Mabalozi takribani themanini,  viongozi wa Jumuiya ya  Afrika Mashariki, Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar na viongozi mbalimbali kutoka nchi za Afrika wakiwemo mawaziri wa nchi mbalimbali na viongozi wa mashirika ya kimataifa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.