Habari za Punde

Wafanyabiashara wa Soko la Kibanda Maiti Watakiwa Kuimarisha Umoja na Ushirikiano Katika Utendaji wa Biashara Zao.

Na.Kassim Abdi. OMPR. Zanzibar.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amewataka wafanyabiashara wa soko la Kibandamaiti kuimarisha umoja na ushirikiano katika utendaji wa kazi ili kutengeneza mazingira mazuri katika biashara zao.

Mhe. Hemed alieleza hayo wakati alipofanya ziara katika soko la kibanda maiti kwa lengo la kuskiliza changamoto zinazowakabili wafanyabiashara pamoja na kujionea hali halisi ya mwenendo wa biashara ndani ya soko hilo.

Makamu wa Pili wa Rais katika ziara yake hiyo alipata fursa ya kukagua maeneo ya wafanyabiashara wa Viungo, Mboga mboga, wafanyabiashara wa Nguo pamoja na maeneo yaliotengwa kwa ajili ya Mama Lishe.

Akiyatembelea mabanda hayo waliopewa wafanyabiashara Makamu wa Pili wa Rais alionesha kusikitishwa kwake na tabia ya baadhi ya watu waliopewa nafasi kwa ajili ya kuendesha biashara kuyatelekeza mane ohayo halio inayopelekea usumbufu kwa watu wengine kwa kukosa sehemu za kuendesha biashara zao.

Akifanya majumuisho baada ya kukamilisha ziara yake Mhe. Hemed ametoa muda wa siku Kumi na Nne (14) kwa viongozi wa Mkoa, Wilaya na Halmashauri kuchukua hatua ya kuwaondosha watu ambao hawayatumii maeneo waliokabdhiwa kwa ajili ya kuendesha biashara.

“Fanyeni uchunguzi ili mugundue watu ambao hawayatumia maeneo waliopewa na muchukuwe hatua ya kuwapatia watu wanaohitaji” Alisisitiza Mhe. Hemed

Akizungumzia suala kuwezeshwa kwa Mama Lishe Makamu wa Pili wa Rais amewalekeza viongozi wa Wilaya kwa kushirikiana na manispaa kufanya marekesho ili kupatikana kwa sehemu za kupikia pamoja na sehemu za kulia chakula katika eneo la soko hilo la kibanda maiti.

Ameleza sehemu walizotengewa Mama lishe ni finyu sana hali inayopelekea usumbufu kwa watoa huduma ya chakula kushindwa kupata sehemu stahiki kwa ajili ya kwaweka wateja kujipatia chakula.

“Suala la huduma ya chakula linahitaji uwangalifu mkubwa katika maandalizi yake, hivyo kuna haja ya kuchukua hatua katika kurekebisha changamoto hii” Alisema Makamu wa Pili

Akigusia uimarishaji wa masoko mbali mbali Mhe. Hemed Amefafanua kuwa serikali ina dhamira njema katika kuhakikisha masoko yake yakuwa katika hadhi na kuvutia huku akiwahakikishia wafanyabiashara wa soko la kibanda kuwa serikali itaendelea kulimarisha soko hili ili liweze kutoa huduma kwa wananchi .

Alibainisha kuwa katika mkakati wa uimarishaji wa masoko hayo serikali imepanga mkakati wa muda mrefu wa kulifanya soko la Jumbi kulijenga ili liwe na vigezo vya Soko la Kimataifa.

Makamu wa Pili wa Rais aliuwagiza uongozi wa Mkoa kwa kushirikiana na uongozi wa wilaya kuenedelea kuimarisha miundombinu muhimu katika soko hilo ili kuonndosha kero zinazowakabili wafanyabiashara sambamba na wananchi wanaofika kupata huduma sokoni hapo.

“Mkurugenzi suala la maji sokoni hapa ni jambo la lazima pamoja na eneo la kuegesha vyombo vya usafiri”  Alisema Mhe. Hemed

Pamoja na mambo mengine, Mhe. Hemed pia aliuwagiza Ungozi kupitia Mkurugenzi wa baraza la Manispaa mjini hadi kufikia siku ya Jumatano awe amesimamisha ungozi maalum utakaosimamia soko hilo kwa lengo la kutatua changamoto za wafanyabiashara.

Nae, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharib Idrissa Kitwana Mustafa amewakumbusha wafanyabiashara ambao wanafanya biashara katika sehemu zisizokuwa  rasmi kufuata agizo la serikali kwa kuyatumia maeneo waliotengewa kwa ajaili ya kuendesha biashara zao huku akiahidi kuwa serikali ya Mkoa itatoa ushirikiano wa karibu kwa wafanyabiashara.

Kwa upande wao, wafanyabiashara wa soko hilo walimuleza Makamu wa Pili wa Rais changamoto zinazowakabili sokoni hapo ikiwa ni pamoja na kukosekana kwa mnada wa nazi na mida mengine jambo linalopelekea soko hilo kukosa wateja wengi  jambo linalosababisha wafanyabiashara kuua mitaji yao.

Wamesema wapo baadhi ya watu wamekabidhiwa maeneo kwa ajili ya kuendesha biashara lakini kwa muda mrefu sasa hawapo katika maeneo waliopangiwa jambo linalosababisha sehemu hizo kuwa tupu bila ya matumizi yaliokusudiwa.

Wafanyabiashara hao, walimuomba makamu wa Pili wa Rais kuangalia uwezekano wa kuzifanyia marekebisho ruti za gari ziweze kupita katika soko hilo ili kuwarahisishia wananchi kwa kutumia gari moja kufika sokoni hapo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.