Na Maulid Yussuf WEMA ZANZIBAR
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe Simai Mohammed Said amewaagiza Wakurugenzi wa Idara zake kuhakikisha wanafanya vikao vya mara kwa mara na watendaji wa Idara zao ili kujua matatizo yanayowakabili watendaji wao.
Ameyasema hayo wakati alipofanya mkutano na Wafanyakazi wote wa Wizara hiyo huko Mazizini Unguja amesema hali hiyo itasaidia kuweza kuyatatua matatizo yao na kuwafanya kufanya kazi kwa weledi zaidi.
Amesema muda umefika sasa kwa kila mtendaji kufanya kazi kwa kufuata sheria zote za kazi za utumishi Serikalini na kuhakikisha kila mmoja atambua wajibu wake.
Amesema Wizara imeanza kwa kasi ndani ya mwaka mpya wa bajeti 2021/2022 hivyo ni lazima watendaji wite wa Wizara hiyo kuenda sambamba na Kasi hiyo kwa lengo la kuleta maendeleo ndani ya Sekta ya Elimu.
Pia Mhe Simai, amemuagiza katibu Mkuu wa Wizara hiyo kuhakikisha zoezi la usafi wa Mazingira linafanyika kila mwisho wa mwezi kama ililivyopangwa hapo awali, huku akimtaka kufanya uhakiki wa Wafanyakazi wote wa Wizara hiyo kwa ujumla ili kujua taarifa zao.
Aidha amewataka watendaji wa Wizara hiyo kuachana na tabia ya kufanya ofisi ni sehemu ya mazungumzo pamoja na kuacha kutumia mitandao kwa mambo yasiyo maana na badala yake kutumia kubuni masuala mbali mbali kwa ajili ya maendeleo ya elimu nchini.
Akizungumza suala la ugatuzi kurudishwa Wizara ya Walimu amesema, ni Lazima Wizara ijipange kuhakikisha wanapunguza changamoto mbalimbali zilizokuwa zikijitokeza ili kuona maendeleo yanapatikana kwa wote.
Nao watendaji wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar wamesema Mkutano huo ni wa mafanikio kwani utasaidia kwa kiasi kikubwa kutekeleza maagizo ya Mhe Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Hussein Mwinyi aliyoyatoa baada ya ziara zake katika sekta ya Elimu kwa Unguja.
Wamesema kuhusu kuhakiki wafanyakazi, watendaji hao wamesema kutasaidia kwa kiasi kikubwa kujua watendaji waliopo, waliostaafu na wanaohitajika ili kuweza kufikia lengo.
Aidha wamempongeza Mhe Waziri wao kwa juhudi anazozichukua katika kuleta maendeleo ndani ya Sekta ya Elimu huku wakimuomba kuendeleaza vikao hivyo kwani vitawapa hamasa na ukumbusho katika kufanya kazi zao vizuri zaidi.
No comments:
Post a Comment