Habari za Punde

Dkt.Shajak Amewataka Wakaguzi wa Ndani Kutoa Maamuzi Sahihi ya Ukaguzi wa Hesabu za Ndani.

Na Raya Hamad – OMKR   06/10/2021.                                                                                       Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Dkt Omar D. Shajak amehimiza mashirikiano katika kutekeleza majukumu ya kazi jambo ambalo litasaidia kutoa maamuzi sahihi ya kiutendaji hasa kwenye masuala yanayohusu ukaguzi wa hesabu za ndani

Dkt Omar D. Shajak ameyasema hayo wakati akizindua kamati ya Ukaguzi wa ndani ya Ofisi hio iliyofuatiwa na mafunzo kwa wajumbe hao, kwenye ukumbi wa mkutano wa Migombani na kuwataka wajumbe wa kamati hiyo kuhakikisha wanatoa ushauri unaofaa kwenye masuala ya matumizi ya fedha

Amewakumbusha wajumbe hao kuwa lengo la kuundwa kwa kamati hiyo ni kuzipitia kwa kina na kuzifanyia kazi hoja zitakazojitokeza kwenye taarifa ya mkaguzi na kufanya maamuzi sahihi ya taarifa hio kwa vile moja kati ya jukumu lao ni kumshauri msimamizi mkuu wa fedha ndani ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais

Dkt Shajak amesema Kamati ya ukaguzi imeundwa kisheria ili kuhakikisha matumizi yote yanafanyika kama ilivyokusudia “nyinyi mtasaidia kunyoosha utaratibu na kama kuna dosari muweze kuzianisha ili kuepusha kukiuka taratibu zilizowekwa” alisisitiza Dkt Shajak

Aidha amewasisitiza fedha ya serikali inatakiwa kutumika kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa ili kuepusha matumizi yaliyo nje na utaratibu pamoja na kuhakikisha hoja zitakazoibuliwa na mkaguzi wa ndani zinapatiwa ufumbuzi wa haraka

Akitoa sifa za mjumbe wa Kamati ya Ukaguzi mkufunzi wa mafunzo Bi Safia Zubeir kutoka Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Uchukuzi amesema wajumbe wa Kamati ya ukaguzi ili waweze kufanya kazi vyema na kutoa maamuzi sahihi anatakiwa kuwa muadilifu, muwajibikaji, mwenye uwezo wa kupima na kushauri.

Pia amesema uadilifu unakufanya kuwa mwaminifu na kuaminika katika majukumu ya kazi, kujali muda mambo ambayo yanasaidia kuifanya kamati kuwa imara na kuwa tayari muda wote kufanyakazi kwa ajili ya kumsaidia Katibu Mkuu ili kuwezesha kufanikiwa majukumu na malengo waliyojipangia kwa wakati

Wajumbe wa Kamati hio wamejifunza maadili ya kazi na majukumu ya kamati, sifa zake, faida ya kuwepo kamati ya ukaguzi na changamoto ambapo mkufunzi huyo amesisitiza haja ya wajumbe wa kamati hio kujengewa uwezo ili kuelewa vyema majukumu yao na kuyatekeleza kitaalamu zaidi

Kwa upande wake Mkaguzi wa ndani wa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Bi Maryam Rajab Baraka na kwa niaba ya kamati hio ametoa shukurani kwa Katibu mkuu kufuatia kuunda kamati ambayo ipo kwa mujibu wa utaratibu wa sheria.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.