Na Khadija Khamis –Maelezo .
Waziri wa Afya Ustawi wa Jamii Jinsia Wazee na Watoto Zanzibar Mhe.Nassor Ahmed Mazrui amewataka wazazi na walezi kushirikiana na Serikali katika mapambano ya vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto nchini .
Hayo ameyasema katika Nyumba ya kulelea Wazee, Welezo wakati wa makabidhiano ya vifaa vya matumizi mbali mbali kwa ajili ya nyumba salama ya kuhifadhia wahanga wa udhalilishaji kutoka kwa Muakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji Nchini Tanzania (IOM) Dr Qasim Sufi .
Amesema vitendo vya udhalilishaji ni janga la kitaifa hivyo iko haja jamii kiujumla kushirikiana kwa pamoja na Serikali ili kuhakikisha vitendo hivyo vinaondoka katika jamii .
Aidha ameitaka jamii kutokuwa na muhali wa kuwaficha wahalifu wa vitendo hivyo kufanya hivyo kutasaidia mapambano ya vita dhidi ya udhalilishaji .
“Ni wajibu wetu kushirikiana kwa pamoja kuunga mkono mapambano ya vita dhidi ya udhalilishaji wa wanawake na watoto tuacheni muhali, tuwe mstari wa mbele kwa kutoa ushahidi wa ukweli .“alisema Waziri .
Nae Muakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji Nchini Tanzania (IOM) Dr Qasim Sufi amesema iko haja kusaidia nyumba salama hapa Zanzibar kwa lengo la kukabiliana na vitendo vya udhalilishaji .
Amesema tatizo hilo ni la kidunia ambalo limekuwa likiwaathiri hususan wanawake na watoto ambao wameonyesha kuathirika zaidi duniani kote.
Kwa upande wa Mkurugenzi wa Idara ya Ustawi wa Jamii na Wazee, Abdalla Saleh Omar amesema nyumba salama inapokea watoto waliofikwa na kadhia mbali mbali ikiwemo udhalilishaji wa kingono kama kubakwa, kulawitiwa pamoja na kupigwa kupitiliza .
Pia amesema usafirishaji haramu wa wahanga ambao hutumika kwa kufanyakazi za majumbani wakiwa katika umri mdogo hupatia hifadhi ya muda watoto hao, ambapo kwa kipindi cha mwezi wa Agosti hadi Oktoba mwaka huu wahanga walipokelewa 22 katika nyumba salama kwa hifadhi ya muda.
Hata hivyo alisema wahanga hao wa kike ni 19 na wa kiume ni 3 wengine hupelekwa katika nyumba salama kwa shaka ya kudhurika ikiwa wazazi wakishtukiwa kuwa watumiaji wa madawa ya kulevya pamoja na watoto waliokosa jamaa hapa Zanzibar.
Waziri wa Afya, Ustawi wa Jami,i Wazee, Jinsia na Watoto Nassor Ahmed Mazrui (wa kwanza kulia) na Mwakilishi Mkaazi kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM Dk. Qassim Sufi wakionyesha hati ya makabidhiano ya msaada wa vifaa mbalimbali walivyokabidhiana ikiwa ni msaada kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM mara baada ya kusaini hati hiyo huko Ukumbi wa nyumba za kuhifadhia Wazee Welezo.
Waziri wa Afya, Ustawi wa Jami,i Wazee, Jinsia na Watoto Nassor Ahmed Mazrui akiangalia baadhi ya vifaa kwaajili ya matumizi katika nyumba salama ikiwa ni msaada kutoka kwa shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM .
Baadhi ya vifaa walivyokabidhiwa Idara ya Ustawi wa Jamii kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM.
Waziri wa Afya Ustawi, wa Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto Nassor Ahmed Mzrui (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watendaji wa Idara ya Ustawi wa jamii
PICHA NA FAUZIA MUSSA –MAELEZO ZANZIBAR.
No comments:
Post a Comment