Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
Dokta Hussein Ali Mwinyi ameendelea na ziara yake katika nchi za Falme za Kiarabu.
Baada ya kuwasili Abu Dhabi jana usiku kwa ziara ya
siku tatu katika nchi za Falme za Kiarabu, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza
la Mapinduzi Dokta Hussein Ali Mwinyi leo hii alishuhudia utiaji saini wa miradi
mikubwa ya uwekezaji baina ya Serikali ya Zanzibar na Kampuni ya Eagle Hills Regional
Properties ya Umoja wa Falme za Kiarabu-UAE
Kwa upande wa Zanzibar, utiaji saini huo ulifanywa na Mkurugenzi
Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji Zanzibar-ZIPA na kwaupande wa Kampuni ya Eagle
alikuwa Mheshimiwa Mohammed Ali Rashid Alabar
Mwekezaji huyo alimueleza Dokta Mwinyi kuridhishwa
kwake na mazingira ya uwekezaji Zanzibar tofauti na alivyotembelea mataifa
mengine duniani ambako nako amewekeza miradi mikubwa.
Alimshukuru pia Rais Dokta Hussein Mwinyi kwa kumuunga
mkono na kuahidi atafanya kila linalowezekana kuhakikisha uwekezaji anaotarajia
kuufanya unafanikiwa.
Miradi inayotarajiwa kujengwa na mwekezaji huyo ni Hoteli
ya nyota tano eneo la Kizingo ambapo pia mwekezaji huyo anatarajiwa kujenga
nyumba Zanzibar kwa ajili ya maeneo ya makaazi.
Vilevile chini ya mradi huo eneo jingine
litakalonufaika na uwekezaji huo ni Matemwe Mkoa wa Kaskazini Unguja ambako kutajengwa
hoteli yenye hadi ya nyota tano na vilevile nyumba za kuishi zenye hadhi ya juu
kwa ajili ya soko la watalii na watu wenye uwezo.
Ziara hii ya Rais ilianza kuonesha dalili nzuri mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Abu Dhabi ambapo baada tu ya kutoka ndani ya ndege mvua ya wastani lianza kunyesha.
Mapema nyakati za asubuhi Rais Dokta Hussein Mwinyi
alihudhuria sherehe za kuwatunuku vyeti washindi wa mpango endelevu wa Abu Dhabi unaojikita
kuendeleza masuala ya afya; chakula; nishati; maji na maendeleo ya elimu duniani sherehe iliyofanyika
Dubai.
Rais Dokta Mwinyi katika shughuli nyingine aliyoifanya
leo ni kutembelea banda la Tanzania katika maonyesho ya kimataifa ya Dubai
yanayojulikana expo 2020.
Rais anaendelea na ziara yake katika nchi za Falme za Kiarabu
ziara inayotarajiwa kumalizika Jumatano tarehe 19 Januari.
No comments:
Post a Comment