Na. Mawazo Kibamba –MAELEZO Machi 7, 2022.
Waziri wa kilimo Mhe. Hussein
Bashe amesema kuwa Serikali katika kipindi cha mwaka mmoja wa Rais Samia Suluhu
Hassan madarakani imefanikiwa kuongeza bajeti
ya utafiti katika sekta ya kilimo ili kukuza sekta hiyo.
Ameyasema hayo Jijini Dar Es
Salaam katika mkutano maalum na waandishi wa habari akielezea mafanikio ya
Wizara ya Kilimo katika kipindi cha mwaka mmoja wa serikali ya Awamu ya sita
chini ya Rais Samia Suluhu Hassan.
Bashe amebainisha kuwa serikali imeongeza bajeti ya utafiti kutoka Sh. Bilioni 7.35 hadi Sh. Bilioni 11.63
ambapo jumla ya shilingi Bilioni 3.63 zimetolewa kuwezesha taasisi
zinazosimamia sekta ya kilimo zikiwepo za TARI, TORITA, TRIT, TPHPA, na TACRI kufanya utafiti wa mazao ya kilimo ikiwemo mchikichi,
zabibu, mkonge, ngano, alizeti, kahawa chai na tumbaku.
Ameongeza kuwa Wizara
imefanikiwa kufungua masoko mapya ya mazao nje ya nchi ikiwemo soko la
parachichi nchini India na Afrika Kusini na soko la Ndizi nchini Kenya, baada
ya kukidhi viwango vya ubora ambapo Bodi ya nafaka na mazao mchanganyiko
Tanzania (CPB) imefungua vituo vya mauzo katika miji ya Juba (Sudani Kusini) na
Lubumbashi (DR Congo) na kukodi maghala yenye uwezo wa kuhifadhi tani 5,000.
“Serikali katika kipindi hiki
tuliangalia mazao gani ambayo yananunuliwa sana na masoko yanayotuzunguka kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki ama SADC,
serikali iliamua kwenda kujenga maghala katika nchi ambazo ndizo tunazouza mazao yetu ambapo mpaka sasa tumefungua
maghala katika nchi za Sudani Kusini, Congo (Lubumbashi), na haya maghala yote
yanafunguliwa na serikali ya Tanzania ili
wafanya biashara wa Tanzania waweze kupeleka na kuuza mazao” Amesema
Bashe
Aidha Mhe. Bashe Ameeleza kuwa
Wizara imesaini hati ya makubaliano ya miaka mitano na Kampuni ya Smart Import
and Export ya Misri, kwa ajili ya ununuzi wa mahindi ya njano, na rasimu ya
makubaliano ya kuiuzia India mazao ya jamii ya mikunde hususan mbaazi, ambapo
taratibu nyingine zinaendelea.
Akielezea malengo mahususi ya wizara ya kilimo amesema serikali imejipanga kuongeza ukuaji wa Sekta ya kilimo kutoka asilimia 5 za sasa na kufikia asilimia 10, kuongeza mchango wa Sekta ya kilimo kwenye GDP kutoka asilimia 25 hadi kufikia 35 ifikapo mwaka 2030 na kupunguza umasikini kwa zaidi ya asilimia 50 kutoka asilimia 26.4 za sasa na kufikia asilimia 13 ifikapo mwaka 2030, lakini pia kuongeza thamani ya mauzo ya mazao ya kilimo nje ya nchi, kutoka Dola za Marekani Bilioni 1.2 za sasa kufikia Dola za Marekani Bilioni 5 ifikapo mwaka 2025.
No comments:
Post a Comment