Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Ambae pia ni Msarifu wa Taasisi ya Benjamin Mkapa Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi Ameongoza Harambee ya Kuchangia Taasisi hiyo.

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi ambaye pia ni Msarifu wa Taasisi ya Benjamin Wiliam Mkapa, akizungumza katika hafla maalum ya Chakula cha usiku na Harambee ya kuchangia Mfuko wa Taasisi ya Benjamin Mkapa, iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Madinat Al Bahr Mbweni Wilaya ya Magharibi “B” Unguja jana usiku 13-7-2022. na (kulia kwa Rais) Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mariam Mwinyi na (kushoto kwa Rais) Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Mkapa Dr. Adeline Kimambo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa taasisi ya Benjamin Wiliam Mkapa licha ya shughuli zake ambazo zinahitaji nyenzo ili kuyafikia malengo yaliyowekwa bado inahitaji kupata michango kutoka kwa taasisi na watu mbalimbali kwa ajili ya kuyafikia malengo hayo.

Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo katika ukumbi wa hoteli ya Madinat Al Bahri, Mbweni Zanzibar wakati wa chakula pamoja na harambee ya kuchangia Mfuko wa taasisi ya Benjamin Wiliam Mkapa. 

Rais Dk. Mwinyi alieleza imani yake kwamba wapo wengi walio na imani ya kuichangia taasisi hiyo ili ifikie malengo na matarajio yake.

Aliwashukuru washiriki wa shughuli hiyo kwa ushiriki na moyo walio nao katika kuhakikisha zinapatikana fedha kuiwezesha taasisi hiyo ili iweze kutekeleza malengo yake.

Rais Dk. Mwinyi ambaye pia ni Msarifu Mpya wa Taasisi ya Benjamin Wiliam Mkapa, alieleza jinsi taasisi hiyo inavyofanya kazi kubwa na nzuri kusaidia sekta ya afya  katika pande mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wageni wote waliotoka nje ya Zanzibar kuvitembelea vivutio mbalimbali vya utalii viliopo ili wawe mabalozi wa kuitangaza Zanzibar nje ya nchi.

Rais Dk. Mwinyi alitoa shukurani za dhati kwa niaba ya watendaji wa taasisi hiyo kwa kuitikia wito wa kuja kushiriki pamoja katika kufanikisha Kongamano la siku mbili Zanzibar.

Nao viongozi wa Taasisi ya Benjamin Wiliam Mkapa walieleza azma ya harambee hiyo pamoja na chakula ikiwa ni pamoja na kuendeleza na kuimarisha sekta ya afya kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara.

Naye Waziri wa Afya wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ummy Ally Mwalimu alieleza juhudi za makusudi zitakazochukuliwa na Serikali zote mbili kuiunga mkono taasisi hiyo.

Katika harambee hiyo jumla ya TZS Bilioni 1.2 zimepatikana, ambapo Rais Dk. Mwinyi alitoa shukurani kwa wachangiaji wote huku  akiahidi kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar nayo haitokuwa nyuma katika kutoa mchango wake.

Imetayarishwa na Idaya ya Mawasiliano

Ikulu Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.