Habari za Punde

Tembo Warriors Yaitoa Japan Kombe la Dunia, Yatinga Robo Fainali Kwa 3-1. Mchengerwa, Dr. Abbasi waongoza hamasa.

 

Wachezaji wa Timu ya Taifa ya Tembo Warriors wakishangilia ushindi wao dhidi ya Timu ya Taifa ya Japan kwa ushindi wa bao 3-1. Michuano ya Kombe la Dunia inayofanyika Nchini Uturuki

Na John Mapepele
Waziri mwenye dhamana ya michezo nchini, Mhe Mohamed Mchengerwa na Katibu Mkuu wake Dkt. Hassan Abbasi  wameongoza kutoa hamasa na mikakati ya ushindi huo wakiungana na watanzania waishio Uturuki.

Katika kipindi  chote Tembo Warriors wamekuwa wakicheza kama ndiyo wanaanza mpambano hadi kipenga  cha mwisho.

Hadi kipindi cha Kwanza kilipokwisha mabao yalikuwa 1-1 huku Tembo wakiwa wa Kwanza  kuliona goli la Japan katika dakika ya 19 ya mchezo.

Japan walilazimisha penati ambayo ndiyo iliyowapatia goli la kufutia machozi.

Akizungumza mara baada ya ushindi huo, Waziri Mchengerwa amesema timu hiyo imeonesha uzalendo mkubwa kwa Taifa lao kilichobaki ni kumalizia kutwaa kombe Kwa kuwa  wanauwezo mkubwa wa kurudi na kombe hilo nyumbani.

Aidha, amefafanua kuwa, Serikali ya Tanzania ipo pamoja na timu hiyo katika kila hatua na ndio maana Rais ameridhia kuigharamia timu hiyo kwa kila kitu ili iendelee kufanya  vizuri.

“Rais na Serikali yenu ipo pamoja na nyinyi, endeleeni kulipigania Taifa lenu, onesheni uzalendo na kuhakikisha mnarudi na kombe nchini na hiyo itakuwa ni zawadi kwa Rais wenu mpendwa na watanzania wote kwa ujumla ”’ amefafanua Mhe. Mchengerwa.

Pia, ameendelea kusisitiza kuwa ahadi zawadi nono kwa timu hiyo ikiwemo shilingi milioni 40 endapo watafuzu robo fainali, shilingi milioni 80 wakifuzu kucheza nusu fainali na shilingi milioni 100 wakifanikiwa kufuzu fainali za michuano hiyo ipo palepale.

Amewataka wachezaji kuendelea kuzingatia nidhamu, umoja na kumtanguliza Mungu na kusema kuwa Serikali ipo kuhakikisha kila kitu kinakwenda vizuri.













No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.