Habari za Punde

SMZ Itaendelea Kutoa Ushirikiano na Taasisi Mbalimbali Zinazowahudumia Mahujaji

 
SERIKALI  ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema itaendelea kutoa ushirikiano kwa taasisi mbalimbali zinazowahudumia mahujaji wanaokwenda Makka, Saudi Arabia kutekeleza ibada ya hijja, baada ya kukamika kwa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi, aliyasema hayo alipohutubia Baraza la Eid -El- Fitri kwenye ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdul Wakil, Kikwajuni Mkoa wa Mjini Magharibi.

Alisema Serikali kupitia kamisheni ya Wakhfu  na Mali ya Amana itaendelea kufanyakazi kwa ushirikino na taasisi hizo ili kuzifanyiakazi changamoto zinazowasababishia usumbufu waumini wanaohitaji kwenda Hijjah.

Akizungumzaia suala la maadili wakati huu wa sikukuu ya Eid el Fitri, Al hajj Dk. Mwinyi ameihimiza jamii kuendeleza maadili ili kujiepusha na vitendo viovu vikiwemo uvunjifu wa amani, udhalilishaji, rushwa, ubadhirifu na dhulma.

Pia aliwaasa wananchi kuendelea kuheshimiana, kutii sheria za nchi, kuwa waadilifu, washirikiane pamoja na kuiendeleza amani iliyopo kwa umoja na mshikamano baina yao.

Al hajj Rais Dk. Mwinyi, alisema kwa nyakati tofauti jamii zimekua zikikumbushwa kuhusu umuhimu wa kuendeleza maadili ili kupata mustakbali wa jamii njema.

Aliongeza suala la kuporomaoka kwa maadili bado linaitesa jamii na kuchangia kuzorotesha juhudi za maendeleo kwenye ustawi wa jamii.

Vile vile, Al hajj Mwinyi aliinasihi jamii kuendelea kupiga vita mambo yasiyoendana na maadili, mila, silka na tamaduni za Wazanzibari ili kupata kizazi kilichoongoka.

“Tuendelee kushirikiana katika kuyapiga vita mambo haya, hayaendani na maadili mema, silka na utamaduni walioachiwa na wazee wetu,” alisisitiza Al hajj Mwinyi.

Akizungumzia suala la malezi, Al hajj Dk. Mwinyi aliwaasa wazazi, walezi na wazee kuhakikisha wanasimamia malezi ya watoto wao ili wawe waumini bora na raia wema wa kwa nchi yao pamoja na kuwasimamia kupata haki yao ya elimu ikiwemo elimu ya dini pamoja na kulinda usalama wao dhidi ya mambo yanayoweza kuwadhuru.

Sambamba na hayo aliwahimiza wazazi/walezi kuzingatia usalama wa watoto wao hasa wakati huu wa sikukuu kwani ni wajibu wao kuwasimamia na kuhakikisha wapo salama dhidi ya mambo yote yanayoweza kuharibu furaha na amani yao pamoja na wazazi wao.

“Wajibu huu tuubebe sote kwa kuhakikisha watoto wetu wanatoka majumbani na wanarejea wakiwa salama.

Mapema asubuhi, Alhaj Dk. Hussein Ali Mwinyi, alijumuika na waumini wa dini ya Kislam kwenye sala ya Iddi Fitri iliyosaliwa msikiti wa Masjid Zinjibar Kiembesamaki.

Pia alipata fursa ya kuzungumza na mashehe kutoka maeneo mbalimbali ya Zanzibar waliofika Ikulu, Zanzibar kwaajili ya kumtakia salam ya heri ya Eid el Fitri.

Katika halfa hiyo, Al hajj Dk. Mwinyi pia aliwaasa Mashehe hao kuendelea kuwaelekeza wananchi kuhusu masuala ya maadili, kuendeleza mashndano ya Qur’an alisema mambo yote yaliyokua yakifanywa kwnye mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan yaendelezwe kwenye miezi mingine inayoendelea pamojana kuendelea kuhimiza amani ya nchi kwa waumini wote.

Kwenye hafla ya Baraza la Eid, viongozi mbalimbali wa Serikali na siasa walihudhuria wakiwemo Marais wastaafu wa Zanzibar awamu ya sita Dk. Amani Abeid Karume, Dk. Ali Mohamed Shein, Rais wa awamu na saba, Makamu wa Kwanza wa Rais, Othman Masoud Othman, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdullah, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Mufti Mkuu wa ZanIbar, Shekh Saleh Omar Kabi, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Khamis Ramadhan Shaaban, Mwenza wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Hafidh Ameir  na Mawaziri na Manaibu mawaziri na viongozi wengine wastaafu wa Serikali.

 IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.