Habari za Punde

Bank of Africa -Tanzania Yazindua Huduma za Wakala

 

Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa BANK OF AFRICA-TANZANIA , Bw. Adam Mihayo (Kulia) akifanya mhamala kwa wakala wakati wa uzinduzi wa huduma ya ‘Bank of Africa WAKALA’ jana,kushoto ni Maofisa Waandamizi wa Benki hiyo,Nandi Nandi Mwiyombella Mkuu wa Masoko na Mawasiliano na Mkuu wa Huduma za Kidigitali  Bw. Jesse Jackson na wa pili kulia ni Meneja huduma wa Selcom,Galus Lutanya

Bank of Africa -Tanzania Limited imezindua huduma za wakala za kibenki zinazoitwa ‘Bank of Africa WAKALA’ kwa lengo la kuboresha ukaribu na wateja wake  na kuongeza mtandao wa wateja kote nchini.

Mfumo huu mpya unaiwezesha BANK OF AFRICA, kuingia mkataba na mawakala wa  kampuni ya Selcom nchini pote kuweza kutoa huduma za kifedha   Kwa niaba yake.

Akiongea wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa BANK OF AFRICA-TANZANIA LIMITED, Bw. Adam Mihayo alisema, “Haya ni mafanikio makubwa kwa benki hii, tunapoendelea na safari ya kuelekea kuweka bidhaa na huduma zetu katika mfumo wa kidijitali, na hivyo kuwarahisishia wateja wetu kupata huduma mahali popote na wakati wowote mbali na kutumia mtandao wa matawi yetu wa siku zote”.

“Tunapozindua huduma mpya  leo  huduma zetu za kifedha zitapatikana kwa mawakala 100 nchini pote kwa awamu hii ya kwanza , na mawakala wengine 200 wataongezeka katika awamu ya pili. Haya ni mafanikio makubwa katika kupeleka huduma za kibenki kwa wananchi wa Tanzania, benki bado ina dhamira ya dhati ya kuendeleza ajenda ya uchumi wa nchi kupitia uwekezaji mbalimbali unaofanywa na tunaendelea kuwekeza”.

Mkuu wa Huduma za Dijitali wa Benki hiyo, Bw. Jesse Jackson,    alieleza kuwa huduma hii imeanzishwa kwa ajili ya kukidhi na mahitaji ya soko na kuhakikisha huduma za kifedha zinapatikana katika maeneo mengi zaidi. "Lengo letu linatokana na mkakati wetu wa kuongeza  ujumuishaji wa kifedha na hitaji la kuendesha mifumo ya kidijitali inayowawezesha wateja wetu kupata huduma za kifedha moja kwa moja katika maeneo yao, Bank of Africa WAKALA  inaleta urahisi kwa wateja wetu kwa  kutuma na kuweka fedha  kwa kuanzia".

"Uzoefu wa kipekee kwa wateja ni muhimu kwetu kama BANK OF AFRICA, tunataka wateja wetu wajisikie wamekaribishwa sio tu kwenye kumbi za benki bali kwenye maeneo mengine wanayoishi. Tunataka kuanzisha uhusiano na kila mtu anayestahili kupata huduma za kibenki bila kujali kiwango cha kipato chake au hali yake na huduma za kidigitali ni moja ya nguzo muhimu zilizopo katika  malengo ya kimkakati ya benki katika mpango mkakati wetu, ubunifu zaidi bado unakuja tunapoelekea kufanikisha lengo hili,” alisema Jesse.

Kwa kuzindua mfumo huu wa  Mawakala, benki pia inaongeza idadi ya wadau katika mnyororo wa thamani wa mfumo wa kifedha hivyo basi kutengeneza nafasi za ajira na kiuchumi kwani inatoa viwango vya kamisheni vizuri kwa WAKALA wake.

Bw. Jesse Jackson alisisitiza kuwa  mwelekeo wa kimkakati wa Benki, BANK OF AFRICA-TANZANIA imedhamiria kutoa huduma mbalimbali  za kidigitali kwa wateja wake  sio tu zinazoendana na matakwa yao,mtindo wao wa maisha na mahitaji yao ya huduma za kifedha , na zinaleta  uzoefu wa kipekee wa wateja.

Nia ni kukidhi mahitaji yote ya makundi yote ya wateja wetu, kusaidia ujumuishaji wa kifedha na kutoa jukwaa kwa  watu wote kupata huduma za benki.

Akigusia ushiriki wa Selcom, Mkurugenzi Mtendaji wa Selcom, Sameer Hirji anabainisha kuwa Selcom itaendelea kuwajibika katika uongozi wa sekta ya teknolojia ya fedha. Ushirikiano huu na benki ya BOA ni hatua moja mbele tunapoelekea kwenye malengo yetu. "Kwa takribani miaka 20 sasa, Selcom imekuwa kinara katika teknolojia ya kifedha na huduma za malipo ikiwa ni pamoja na benki za wakala na huduma za malipo bila fedha taslimu. Tunatarajia ushirikiano zaidi katika sekta ya fedha miaka ijayo".

Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa BANK OF AFRICA-TANZANIA , Bw. Adam Mihayo (wa tatu kutoka kushoto) akiwa na wafanyakazi wa benki hiyo wakati wa hafla ya uzinduzi  huo
Baadhi yan  wafanyakazi wa Bank of Africa wakifurahia  baada ya uzinduzi huo.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.