Habari za Punde

Tani 130 za mchele zateketezwa


 Na Fauzia Mussa ,  Maelezo

 

Wakala wa Chakula Dawa na vipodozi Zanzibar (ZFDA) imeteketeza jumla ya  Tani 130 za mchele mbovu  aina ya family gold ulioingizwa Nchini na Kampuni ya Longwide Traders iliyopo maruhubi Wilaya ya Mjini.

 

Akizungumza wakati wa uteketezaji wa mchele huo huko Jaa kuu Kibele  Mkuu wa ukaguzi Bandarini ZFDA  Mohamed Shadhil Shauri amesema Mei 13 mwaka huu ZFDA ilizuia kushushwa kwa  mchele huo  katika Bandari ya Malindi kutokana na kuharibika na  kutokufaa kwa matumizi ya binaadamu.

 

Alisema mchele huo uliharibika kutokana na kujaa Sana katika makontena , hivyo aliwataka wafanyabiashara kuhifadhi bidhaa zao kwa kiasi kinachorushusu hewa kuingia ili kuifanya  bidhaa hiyo kuwa salama wakati wote.

 

Alifahamisha kuwa jukumu la kumlinda mtumiaji ni la watu wote hivyo aliwaomba wafanyabiashara kutoa taarifa kwa wahusika mara Tu wanapoona dalili za kuharibika Kwa bidhaa zao kabla ya kuziingiza sokoni .

 

Hata hivyo aliwashauri wafanyabiashara kuharakisha taratibu za ushushwaji wa mizigo bandarini ili kuepuka changamoto zinazoweza kujitokeza  endapo bidhaa hizo zitakaa kwa  muda mrefu ikiwemo kuharibika.

 

“inawezekana mchele ulipakiwa ukiwa mzima lakini uliharibika kutokana na joto Tu lililomo katika makontena , niwasihi wafanyabiashara mupakie kwa kiasi na kufuata taratibu ili mizigo yenu iweze kutoka kwa wakati ili kuepuka hasara kama hizi.”aliishauri mkuu huyo

 

Mmiliki wa Bidhaa hiyo Fadhil Muhammad Fadhil alisema mara Tu baada ya kugundua mchele huo umeharibika nakutofaa kwa matumizi ya binaadamu alishirikiana na ZFDA kwa hatua za uteketezaji.

 

Alisema licha ya kuwa alinunua na kupakia bidhaa hiyo  ikiwa salama lakini kuchelewa  kufika  kwa bidhaa hiyo kulichangia kuharibika,hivyo aliwashauri wafanyabiashara wenzake kuwa makini katika harakati za usafirishaji wa bidhaa ili kukwepa hasara zisizotarajiwa.

 

"Mchele niliununua ukiwa mzima ila umechelewa kufika ,lile vuke na joto la melini ndio sababu kuu ya bidhaa yangu kuharibika" alisema mmiliki huyo

 

ZFDA ni TAASISI inayofanyakazi chini ya Sheria Na.2/2006 na marekebisho yake Na.3/2017 yenye  jukumu la kudhibiti ubora na usalama wa Bidhaa za chakula kwa kuhakikisha zinakua  salama Kwa mtumiaji kabla ya kuingizwa sokoni.


PICHA KWA HISANI YA ZFDA

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.