Habari za Punde

Vifaa na Tiba visivyo salama vyakamatwa Uwanja wa Ndege Zanzibar



 Kaimu Mkurugenzi Idara  ya Dawa na Vipodozi  ZFDA  Haji Juma Khamis  akitoa Taarifa kwa umma juu ya kukamtwa kwa kilo 40 za  Dawa,Vifaa tiba na vipodozi vilivyoingizwa Nchini kinyume na Taratibu kupitia  Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid  Amani Karume mnamo septemba 13 , mwaka huu,hafla iliyofanyika Ofisi ya ZFDA Mombasa Zanzibar.


Na Fauzia Mussa ,       Maelezo

Wakala wa ,Chakula na Dawa ZFDA Imekamata shehena ya  Dawa,vifaa tiba na Vipodozi katika uwanja ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume ulioingizwa Zanzibar kinyume na utaratibu.

 Akitoa taarifa kwa Umma, Kaimu Mkurugenzi Idara  ya Dawa na Vipodozi  ZFDA  Haji Juma Khamis  amesema mnamo Septemba 13 mwaka huu wakaguzi wa ZFDA walikamata mzigo huo wenye uzito wa kilo 40 uliongizwa Nchini kutoka Belgium kupitia ndege ya  Shirika la Ethopian Airline kwa nambari ya BL (Bill of Loading )071-4959035 bila ya kuwa na  kibali .

Alifahamisha kuwa kufuatia uchunguzi uliofanywa na ZFDA Umebaini kuwa vifaa hivyo vilikusudiwa kutolewa msaada katika Vituo vya Afya na Skuli za Wilaya ya Kusini  kinyume na utaratibu unaokubalika.

Aidha amesema uchunguzi umebaini uwepo wa dawa zilizomaliza  muda wa matumizi takribani  miaka kumi,na  baadhi ya vifaa tiba vilivyotumika na kufungashwa katika vifungashio visivyo rasmi ndani ya mzigo huo.

Alisema miongoni mwa  Dawa zilizopitwa na muda wa matumizi katika mzigo huo  ni pamoja na  dawa za meno kwaajili ya  watoto aina ya ELEMEX, hivyo aliitaka jamii kutokupokea misaada ya Dawa,Vifaa Tiba na Vipodozi ambavyo havikutolewa na Serikali kupitia Wizara ya Afya .

Aidha alifahamisha kuwa  bidhaa zote zilizokuwemo katika Shehena hiyo  hazikusajiliwa na  Wakala wa Chakula na Dawa jambo ambalo ni kinyume na kanuni na Sheria za ZFDA, Hivyo ZFDA imechukua hatua ya kuuzuia  mzigo huo usisambae na kufika kwa waliokusudiwa huku taratibu za uteketezaji zikiendelea.

Vilevile aliwataka Wananchi kuendelea kutoa taarifa za uwepo wa  bidhaa wanazozitilia mashaka juu ya ubora ,usalama na ufanisi wake ili kumlinda Mtumiaji.

 Hata hivyo alitumia fursa hiyo kuwaomba wadau na wahisani kufuata muongozo na taratibu za Wizara ya Afya Zanzibar za kuingiza vifaa kinga na tiba kwa ajili ya  misaada ili kuondosha usumbufu unaowezakuijtokeza.

“hata kama Zanzibar ni Maskini lakini huu sio msaada tuanaohitaji ,vitu vimeshatumika vimepitwa na muda ndio mnatuletea,kama muhusika wa shehena hii angelifuata taratibu asingeruhusiwa kuingiza ”Alisema kaimu huyo

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.