Habari za Punde

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Afungua Hospitali ya Wilaya ya Kati Mwera Pongwe.Ikiwa ni Shamrashamra za Miaka 60 ya Mapinduzi ya Zanzibar

Serikali ya Awamu ya Nane (8) itaendelea kuboresha miundombimnu ya upatikanaji wa huduma mbali mbali ikiwemo huduma za Afya nchini ikiwa ni azma ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964 ya kutoa huduma bora za Afya  kwa  kila mwananchi bila ya malipo na  ubaguzi wa aina yoyote.

Akifungua Hospitali ya Wilaya ya Kati iliyopo  Mwera Pongwe , Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe Hemed Suleiman Abdulla amesema kupitia ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020-2025, Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya mwaka 2050, Sera na Mikakati mbali mbali Serikali imeweza kujenga hospitali kumi (10) za Wilaya kwa Unguja na Pemba ambazo zina vifaa tiba pamoja na  magari ya kubebea wagonjwa pindi dharura itakapotokea.

Mhe. Hemed amesema miradi hii ya maendeleao inayofanywa na Serikali inaakisi malengo ya Mapinduzi ambayo ndio fikra na mawazo ya waasisi wa Mapinduzi matukufu ya mwaka 1964 hivyo Serikali itaendelea kuimarisha huduma bora kwa jamii kwa kuhakikisha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, TEHAMA,wafamasia, wauguzi pamoja na madaktari wakutosha katika hospitali na vituo vya Afya nchini.

Aidha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameuagiza Uongozi wa Wizara ya Afya kuhakikisha wanaisimamia vyema hosptiali hio na hospitali nyengine  ili kuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali kwa kuwapatia wananchi huduma bora bila ya ubaguzi wa aina yoyote.

Amesema Wiza ya Afya ina wajibu wa kuhakikisha hospitali hizi zinatunzwa na kufanyiwa ukarabati wa majengo na vitendea kazi mara kwa mara ili kuviwezesha kuwa endelevu katika utoaji wa huduma na kuwataka wafanyakazi waliopangiwa katika hospital ya Mwera Pongwe.              

Mhe. Hemed amezitaka kampuni ya Lancet na Saifee amabazo zimepewa mkataba wa kutoa huduma hospitalini hapo kuhakikisha huduma zote zinapatikana kwa wakati na kwa ubora wa hali ya juu kama makubaliano yanavyoelekeza.

Sambamba na hayo amewataka wahudumu na madaktari kuendelea kutumia lugha nzuri na kufuata maadili yao ya kazi wakati wanapowahudumia  wagonjwa wanaofika kupatiwa huduma hospitalini hapo pamoja na kuwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa madaktari na wahudumu sambamba na kuilinda miundombinu iliyomo hospitalini ili iweze kudumu na kutumika kwa muda mrefu.

Nae Waziri wa Afya Mhe Nassor Ahmed Mazurui amesema hudu za Afya zimeimarika zaidi Zanzibar ndani ya miaka mitatu (3) ya Uongozi wa Rais Dk Mwinyi kwa kujengwa mahospitali ya Wilaya, Mkoa na zile za Rufaa pamoja na kufanyiwa maboresho makubwa baadhi ya vituo vya Afya.

Amesema kuwa hospitali na vituo vya Afya vilivyojengwa vimekidhi viwango na ubora, pamoja na kuwepo vifaa tiba vya kutosha kulingana na uhitaji sambamba na utolewaji  wa huduma za matibabu kwa wananchi wote bila ya ubaguzi  na kufikia zile fikra na mawazo ya waasisi wa mapinduzi akiwemo rais wa kwanza wa Zanzibar Marehemu Sheikh ABEID AMANI KARUME.

Akitoa Taarifa ya Kitaalamu kuhusu ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kati ya Mwera Ponge Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. Amour Suleiman amesema Jumla ya shilingi Bilioni 9.7 zimetumika katika Ujenzi wa Mradi wa Hospital hiyo ambapo kwa wakati mmoja ina uwezo wa kulaza zaidi ya wagonjwa mia moja(100) na kupatiwa matibabu hospitalini hapo.

Amesema kuwa hospitali hiyo ya Wilaya inatoa huduma mbali mbali ikiwemo Huduma ya mama na mtoto, huduma ya maabara, huduma ya magojwa ya dharura hivyo amewataka wananchi kuendelea kuitumia vizuri hospitali hiyo kwa kutoa ushirikiano kwa madaktari na watoa huduma hospitalini hapo ili kuweza kufikia malengo ya mapinduzi matukufu ya mwaka 1964 ya kutoa huduma bora kwa kila mwnanchi.

Imetolewa na kitengo cha Habari (OMPR)

tarehe  02.01.2024

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.