Habari za Punde

Zanzibar Itaungana na Dunia Kuadhimisha Siku ya Wakunga na Wauguzi

Mwenyekiti wa Baraza la wauguzi na wakunga akitoa taarika kwa waandishi wa habari kuhusiana na siku ya wakunga duniani ambayo huadhimishwa mei 05 na siku ya wauguzi  ambayo huadhimishwa kila ifikapo mei 12 duniani kote,hafla iliyofanyika Wizara ya afya Mnazimmoja Zanzibar.
Afisa uzazi Salama  Haidhuru Ramadhan akichangia katika Mkutano na waandishi wa habari kuhusiana na siku ya wakunga duniani ambayo huadhimishwa mei 05 na siku ya wauguzi  ambayo huadhimishwa kila ifikapo mei 12 duniani kote,hafla iliyofanyika Wizara ya afya Mnazimmoja Zanzibar.

Mratibu afya ya akili  Sleiman Abdul Ali akichangia katika Mkutano na waandishi wa habari kuhusiana na siku ya wakunga duniani ambayo huadhimishwa mei 05 na siku ya wauguzi  ambayo huadhimishwa kila ifikapo mei 12 duniani kote,hafla iliyofanyika Wizara ya afya Mnazimmoja Zanzibar.

PICHA NA FAUZIA MUSSA, MAELEZO ZANZIBAR

Na Takdir Ali. Maelezo. 30.04.2024.

Mratibu wa afya afya ya Akili Zanzibar Suleiman Abdu Ali amesema tatizo la Afya ya Akili Zanzibar lipo na linaongezeka siku hadi siku kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo matumizi ya dawa za kulevya.

Akizungumza katika Mkutano na waandishi wa habari kuhusiana na siku ya wauguzi na wakunga Duniani huko Wizara ya afya Zanzibar amesema inakisiwa zaidi ya watu 5000 wameathirika na magonjwa hayo kwa sasa.

Amesema vituo vya kutoa huduma vinaendelea kupokea wagonjwa wapya kila siku mfano Hospitali ya Kidongochekundu inapokea wastani wa wagonjwa wapya kati ya 100 hadi 150 kwa mwezi ambapo wengi wao ni vijana na Watoto.

Akieleza hali ya ugonjwa huo  kisiwani Pemba amesema  mwaka  2023 wagonjwa 1039 wapya kutoka hospitali za Wete, Mkoani, Chake chake, Vitongoji na Micheweni walibainika.

Pia amesema takwimu hizi hazijaangalia hopitali na vituo vingine kama Hopitali ya Kivunge na Makunduchi jambo ambalo linadhihirisha kuwepo kwa tatizo hilo.

Aidha amesema Wizara ya Afya kupitia Shirika la Kuimarisha Huduma za Afya Zanzibar – HIPZ imefanya juhudi kubwa ya kuongeza uwelewa wa afya ya akili Zanzibar na kupunguza unyanyapaa kwa kuwapatia wafanyakazi 55 utaalamu maalum wa utoaji elimu ya afya ya akili kwa wilaya zote za Unguja na Pemba.

Aidha Wahudumu wa Afya Jamii (CHW) ambao nao wanafanya kazi zao chini ya usimamizi wa Wauguzi, takriban Wahudumu wa Afya Jamii 310 wamepatiwa mafunzo maalum ya Tiba ya Kisaikolojia kwa watu wanaosumbuliwa na wasiwasi na msongo wa Mawazo ambapo tayari wahudumu hao wameshahudumia wananchi zaidi 2370 kwa Unguja na Pemba.

Amefahamisha kuwa Magonjwa ya akili hupelekea umaskini na ulemavu ambapo mtu binafsi na familia hudharauliwa katika jamii isiyo kuwa na elimu, kuwanyanyapaa na kutengwa na jamii.

Mapema akitoa taarifa kwa vyombo vya habari kuhusiana na maadhimisho ya siku hizo Mwenyekiti wa Baraza la Wauguzi na Wakunga Sharifa Awadhi Salmin amewataka Waandishi wa habari kuandika habari zinazohusu siku ya wakunga na wauguzi Duniani ili kutoa uelewa kwa jamii.

Aidha amesema maadhimisho hayo kwa upande wa Zanzibar yataambatana na mambo mbalimbali ikiwemo zoezi la uchangiaji wad amu, singo ya kizazi, kutoa elimu ya lishe,afya ya uzazi na afya ya akili kwa vijana pamoja na uzinduzi wa jumuiya ya wakunga Zanzibar.

 Maadhimisho ya siku ya wakunga Duniani yanatarajiwa kufanyika 05.05.2024 amapo kauli mbiu “wakunga: suluhisho muhimu la tabia Nchi” na siku ya wauguzi Duniani hufanyika tarehe 12.05.2024 ambapo kauli mbiu yake ni “wauguzi wetu, mustakbali wetu, nguvu ya Uchumi ya huduma za Afya”.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.