RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi amesifu fursa kubwa ya biashara
iliyopo baina ya Tanzania ikiwemo Zanzibar na Visiwa vya Comoro.
Rais Dk. Mwinyi ameyaeleza hayo Ikulu Zanzibar,
alipozungumza na Balozi mpya wa Tanzania nchini Comoro Mhe. Said Othman Yakoub
aliefika kumuaga baada ya kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe Dk. Samia Suluhu Hassan tarehe 13 April, mwaka huu.
Katika mazungumzo yao wamegusia
kuendeleza makubaliano yaliyopo baina ya Zanzibar na Comoro hasa kwenye
nyanja za Elimu kupitia Chuo Kikuu cha Zanzibar (SUZA) na vyuo vya Comoro,
sekta ya Usafirishaji, Afya, Biashara na vyombo vya habari kupitia Shirika la
Utangazaji la Zanzibar (ZBC) na Shirika la Utangazaji la Comoro.
Alisema, ishara ya uhusiano mzuri baina ya pande hizo
mbili ni utekelezaji wa Makubaliano ambayo awali yaliazimiwa na pande mbili
hizo sambamba na uhusiano wa damu uliopo baina ya Zanzibar na Comoro.
Rais Dk. Mwinyi alisema, sekta ya biashara ni fursa
adhimu kwa Zanzibar kunufaika na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia
Shirika la Meli tayari imeagiza meli mbili zitakazofanya safari zake ikiwemo
visiwa vya Comoro sambamba na meli ya MV Mapinduzi ambayo imefanyiwa matengezo
makubwa na inatarajiwa kujeresha safari zake visiwani Comoro.
Akizungumzia suala la usafirishaji na ufanisi hasa
kwa bandari za Zanzibar, Rais Dk. Mwinyi alisema, Serikali inazifanyia
maboresho makubwa ili kurejesha ufanisi wa handari hizo. Pia Rais Dk. Mwinyi
alieleza kuhusu usafiri wa anga kwamba utakuwa na tija kubwa kwa fursa za
biashara baina ya Zanzibar na Comoro.
Dk. Mwinyi pia aligusia sekta ya Afya, akimweleza
Balozi Said kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ina nia ya kukuza Utalii
wa matibabu nchini kupitia hospitali ya Mkoa ya Lumumba iliyopo Mkoa wa Mjini
Magharibi inayotarajiwa kupokea watalii wengi wa matibabu kutoka mataifa
mbalimbali ya dunia ikiwemo visiwa vya Comoro.
Hata, hivyo Rais Dk. Mwinyi alieleza uhusiano baina
ya Zanzibar na Comoro ni maalum ni wa damu na undugu na amemuahidi Balozi Said
kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Comoro
wataangalia uwezekano wa kuanzisha ubalozi mdogo wa Comoro Zanzibar na kuahidi
Serikali itatoa ushirikiano wa hali ya juu kwenye eneo hilo ilkiwemo kuwasaidia
jengo la ubalozi huo.
Pia Rais Dk. Mwinyi ametumia
fursa hiyo kumpongeza Balozi Saidi kwa kuteuliwa kuiwakilisha Tanzania kwenye
visiwa vya Comoro na kumuahidi kumpa
ushirikiano wa hali ya juu kwenye majukumu yake ya kuitangaza na kuitekeleza
kwa vitendo Diplomasia ya Uchumi ya Tanzania.
Kwa upande wake, Balozi Said amemshukuru Rais Dk. Mwinyi kwa nasaha na maelekezo yake na kumuahidi
kuitangaza vyema nchi na kuzitumia fursa zinazopatikana Comoro kwa maslahi ya
Tanzania ikiwemo Zanzibar.
Alisema
Kariakoo, Dar es Salaam na Zanzibar ni vitovu vya biashara baina ya Tanzania na
Comoro ambako awali wafanyabiashara wengi waliingia nchini na kufanya vizuri
zaidi kwenye Sekta ya biashara.
Alisema hadi
mwaka jana Soko la Kariako, Dar es Salaam lilikusanya zaidi dola milioni 54 sawa
na bilioni 145 kwa mwaka.
Kuhusu Sekta ya
Afya, Balozi Said alisema Comoro ni fursa adhimu ya Tanzania kuendelea
kunufaika nayo kwani inaleta watalii wengi wa matibabu nchini.
Alisema kwa
mwaka jana zaidi ya wagonjwa 14, 300 raia wa Comoro waliingia nchini kwaajili
ya matibabu, sawa na wastani wa wagonjwa 12,000 kwa mwezi, wagonjwa 300 kwa
wiki na 42 kwa siku ambao hutibiwa Tanzania.
Balozi Saidi
alisema, kuanzishwa kwa hospitali ya Mkoa ya Lumumba, Zanzibar ni fursa adhimu kwa
Sekta ya Afya Zanzibar kupitia uhusiano wa kindugu uliopo baina ya Comoro na
Zanzibar.
Aidha, Balozi
Saidi alipongeza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kudhamiria
kuongeza meli mbili zitakazoleta tija na kuimarisha uhusiano uliopo baina ya
Comoro na Zanzibar hasa kwenye sekta ya usafirishaji na biashara na kuwataka
Watanzania hususani Wazanzibari kuitumia fursa hiyo adhimu ya kukuza uchumi wa
nchi.
Balozi Saidi
pia amesifu ushirikiano uliopo baina ya Comoro na Tanzania hasa kwenye usafiri
wa anga kwa kuwepo safari mbili kwa siku baina ya Tanzania na Comoro kupitia
ndege za “Precian Air” na Air Tanzania ambazo pia alizieleza kuwa ni fursa
lukuki kwa wa Tanzania kuwanufaisha kiuchumi na kijamii.
Uhusiano wa Diplomasia baina ya Tanzania na Comoro ni wa kihistoria, ambapo Comoro ilifungua ubalozi wake Dar es Salaam mwaka 2013 na mwaka mmoja baadae Tanzania ilifungua ubalozi wake jijini Moroni, Comoro mwaka 2014. Mwaka jana 2023, pande mbili hizo za Diplomasia zilianzisha Tume ya kudumu ya pamoja (JPC) ambapo mwezi Julai mwaka huu inatarajiwa kufanya mkutano wa pamoja utakaotoa wawakilishi baina yao.
No comments:
Post a Comment