Habari za Punde

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Azungumza na Kamati ya Marathon Zanzibar

 
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, amesema kwamba kuna umuhimu mkubwa kwa taasisi  na wadau mbali mbali kufanya jitihada za kuvitangaza kwa ubunifu zaidi  vivutio vya historia vilivyopo  Mjimkongwe  jambo litakalosaidia kukuza maendeleo ya sekta ya biashara ya utalii katika mji huo na Zanzibar kwa jumla. 

Mhe. Othman ameyasema hayo Ofisini kwake Migombani mjini Zanzibar alipokutana na Kamati ya Mandalizi ya Mashindano ya Marathon ya Kimataifa yanayotarajiwa kufanyika Jumaapili ijayo ya Novemba 3 mwaka huu.

Mhe. Othman amesema kwamba mji huo una mambo mengi ya kihistoria ambayo hadi sasa hayatangazwa ipasavyo kwa kufahamika na wageni pamoja na wenyeji kutokana na kukosekana ubunifu wa kuyatangaza kwa wadau mbali mbali mambo hayo ya kihistoria wakiwemo wageni.

Hivyo, ameitaka Kamati hiyo na wadau wengine kuhakikisha kwamba wanakuwa wabunifu kuyatafuta masuala muhimu katika mji huo yanayoweza kuwa kivutio cha utalii kuyaingiza katika ubunifu wao ikiwemo mashindano kama hayo ya kimataifa ya marathoni ambayo yatajenga uelewa kwa wenyeji na wageni na kuchangia ukuaji wa biashara ya utalii katika eneo hilo.

Amesema kwamba hatua hiyo ni muhimu pia katika kuithmani ipasavyo historia ya Zanzibar ambayo, mbali na majengo yaliyopo ndani ya mji Mkongwe huo, lakini yapo mambo  mengi yanayohitaji kutangazwa zaidi na kuweza kuleta manufua katika sekta ya utalii na Zanzibar kwa jumla.

Amesema miongoni mwa mambo yanayohitaji kutangazwa ni pamoja na kuzifahamu na kuzitangaza historia za majengo mbali mbali ya mji huo ambayo kimsingi haifahamiki ipasavyo licha ya kuwa ni vivutio muhimu kutokana na kutotangazwa ipasavyo .

Hivyo amesema kwamba kupitia matamasha tofauti kunahaja na umuhimu mkubwa kuhakikisha kwamba kunakuwa na juhudi za ubunifu wa kuutangaza mji huo pamoja na historia yake ili iweze kuwa na manufaa zaidi katika kuendeleza biashara ya utalii hapa Zanzibar.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mahindano ya Marathon Hassan Mussa, amesema kwamba katika mashindano ya mwaka huu, kamati imejiongeza kwa kuutumia mji Mkongwe kama kivutio cha utalii ambapo washiriki wa mbio hizo pia watapita katika maeneo mbali mbali ya mji Mkongwe.

Aliyataja maeneo hayo kuwa ni  mtaa wa Darajani  kuelekea Kiponda, Hamamni  ,Mkunazini,  barabara ya Soko Muhogo  na kumalizia maeneo ya Forodhani ambapo maeneo hayo kwa jumla yatakuwa ni urefu wa kilomita moja ya ndani ya Mji Mkongwe kwa washiriki wote.

Hii ni awamu ya nne ya kuwepo mashindano hayo ya marathoni ya kimataifa, ambapo kila mwaka kunaongezwa ubunifu ikiwa ni pamoja na kupata ushiriki wa watu na wanamichezo washuhuri kutoka nchi tofauti Afrika Mashiriki na duniani kwa jumla.

Mwisho

Imetolewa na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa rais wa Zanzibar kupitia Kitengo chake cha Habari, leo Jumatatu tarehe 28 Oktoba 2024. 





     

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.