Na Khamis Haji, OMKR
WAGONJWA
waliolazwa na wale wanaopata huduma katika hospitali ya Wete, Kaskazini Pemba
wamepata faraja kubwa kufuatia ziara ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar,
Maalim Seif Sharif Hamad aliyoifanya Novemba 23 mwaka jana hospitalini hapo.
Katika ziara hiyo
alipotembelea taasisi zilizopo chini ya wizara ya Afya, Makamu wa Kwanza wa Rais alitoa maagizo ya kutafutiwa ufumbuzi wa
haraka baadhi ya huduma zinazokosekana katika hospitali hiyo.
Huduma ambazo Maalim
Seif aliagiza zipatiwe ufumbuzi ni kuharibika
kitanda katika chumba cha upasuaji, kutafutwa friji la kuhifadhia dawa
na vifaa vya matibabu, kuongezwa vitanda katika wodi za hospitali pamoja na
kuzingatiwa mazingira ya usafi.
Maalim Seif, juzi
alifika hospitalini hapo kwa ajili ya kufuatilia utekelezaji wa maagizo
aliyoyatoa mwezi Novemba, ambapo alikuta takriban yote yamepatiwa ufumbuzi na
wananchi wanaendelea kupatiwa huduma zilizokuwa zikikosekana kwa ufanisi
mkubwa.
Daktari Dhamana wa
hospitali ya Wete, Othman Maalim Haji alimueleza Maalim Seif kuwa friji tayari
limepatikana, kitanda kilichokuwepo kimefanyiwa matengenezo pamoja na kuletwa
chengine kutoka Mkia wa Ng’ombe, ambapo pia vitanda vyengine vipya kwa ajili ya
chumba hicho vinatarajiwa kuwasili hivi karibuni.
Aidha, daktari huyo
dhamana alisema tayari wamepokea vitanda 20 pamoja na magodoro yake ambavyo
vimeshafungwa katika wodi kwa ajili ya kusaidia kutatua tatizo la uhaba wa
vitanda pamoja na uchakavu wa vitanda, magodoro na matandiko yaliyopo hivi
sasa.
“Kwa kweli ziara
yako Mheshimiwa Makamu imekuwa chachu ya utatuzi wa changamoto nyingi
zilizokuwa zikiikabili hospitali, hivi sasa takriban zote zimepata ufumbuzi,”
alisema daktari dhamana alipokuwa akizungumza na Maalim Seif.
Daktari huyo
alisema maagizo mengine ambayo yameweza kutekelezwa ni kuwekwa utaratibu mzuri
na kumbukumbu sahihi za utoaji na uingizwaji wa dawa, zikiwemo zinazotolewa kwa
wagonjwa pamoja na zinazoingia katika bohari ya hospitali hiyo, kutoka Bohari
Kuu ya Wizara ya Afya.
Pamoja na maagizo
katika hospitali hiyo, Maalim Seif pia mwezi Novemba aliutaka uongozi wa Wizara
ya Afya kushughulikia kwa haraka malalamiko ya wafanyakazi, ikiwemo yanayohusu
mafao yao
pamoja na malalamiko ya kuwepo upendeleo.
Afisa Dhamana wa
Wizara hiyo Pemba, Dk.Ukasha alisema baadhi ya maagizo hayo yameshatekelezwa,
ikiwemo tatizo la wafanyakazi wapya waliopelekwa Pemba kucheleweshewa mishahara
na posho zao, pamoja na mfanyakazi Sanura Salehe wa hospitali ya Chake Chake
aliyedai kudhulumiwa kwenye mkopo wake wa baiskeli.
Wakizungumza na
mwandishi wa habari hizi wananchi na wagonjwa waliokuwepo hospitalini hapo
walisema ni kweli kumekuwa na mabadiliko makubwa hospitalini hapo tokea
kufanyika ziara ya Maalim Seif mwishoni mwa mwaka jana.
Walisema hata
suala la usafi katika hospitali hiyo limeimarika vizuri, ikilinganishwa na hali
ilivyokuwa huko nyuma.
Wakati huo huo,
Maalim Seif amezindua maabara ya kisasa katika hospitali ya Micheweni mkoa wa
Kaskazini Pemba, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 49 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Akizungumza katika
hafla ya uzinduzi wa maabara hiyo, ambayo ujenzi wake ulifadhiliwa na kituo cha
Center for Diseases Control (CDC) cha Marekani na Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar (SMZ), Maalim Seif alisema hatua hiyo ni ukombozi kwa wananchi wote wa
Micheweni kwa sababu hivi sasa wataweza kuchunguzwa maradhi yao hapo hapo.
Alisema awali
wananchi walikuwa wakipata shida kubwa kwa kulazimika kukaa siku nyingi
kusubiri matokeo ya uchunguzi wa maradhi yanayowashumbua, ambao ulikuwa
ukifanywa katika hospitali za Chake Chake, Wete na Mkoani, lakini pia maabara
hiyo itakuwa ya rufaa kwa vituo vyote vya afya vya Wilaya ya Micheweni.
0 Comments