STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 6.1.2015
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa mwaliko wa Zanzibar kushiriki
katika Tamasha la Kimataifa la Muziki wa Afrika nchini Ujerumani mwezi Juni
mwaka huu ni njia moja wapo ya kuitangaza Zanzibar kiutalii nchini humo pamoja
na nchi nyengine za Ulaya.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo katika mazungumzo kati yake na Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania
Mhe. Egon Kochanke aliyefuatana na Dk. Stefan Oscman ambaye ni Mkurugenzi wa
Shirika la Kimataifa la Tamasha la Afrika, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu mjini
Zanzibar.
Katika mazungumzo
hayo Dk. Shein alisema kuwa mwaliko huo ni nafasi ya pekee kwa Zanzibar kuweza
kujitangaza kiutalii pamoja na kiutamaduni kutokana na Zanzibar kujaaliwa
katika sekta hizo ambazo zimeweza kuijingea sifa kubwa ndani na nje ya nchi.
Dk. Shein alisema
kuwa Ujerumani na Zanzibar ni nchi zenye uhusiano wa kihistoria ambao uhusiano
huo umeweza kuleta mashirikiano makubwa katika sekta mbali mbali na kusisitiza
kuwa hatua hiyo ni ya pekee kwa Zanzibar ambayo itaweza kusaidia katika
mikakati yake ya kukuza uchumi na kuimarisha utamaduni.
Aidha, Dk. Shein
alitoa pongezi kwa Serikali ya Ujerumani kwa kuithamini Zanzibar na kuipa
mwaliko katika tamasha hilo sambamba na kushiriki kikamilifu kwa wasanii wa
Zanzibar ambao wataonesha tamaduni za kizanzibari ikiwa ni pamoja na muziki wa
taarab na sanaa nyenginezo.
Dk. Shein alisema
kuwa hivi sasa Zanzibar imekuwa ikipokea watalii wengi kutoka Ujerumani ambapo anamatumaini
makubwa kuwa Tamasha hilo litaongeza idadi kubwa ya watalii kutoka nchi za
Ulaya.
Sambamba na hayo,
Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar imekuwa na vipaji kadhaa vya wasanii, hivyo
anaimani kuwa wasanii hao watafanya vizuri katika Tamasha hilo la Kimataifa
nchini humo.
Dk. Shein alisema
kuwa mbali ya kuwa Ujerumani itashirikiana na Zanzibar katika tamasha hilo
lakini hata hivyo, Zanzibar imekuwa na uhusiano na ushirikiano mwema kati yake
na nchi hiyo hasa katika masuala ya mila na utamaduni, elimu na muziki.
Nae Dk. Stefan
Oschman alimueleza Dk. Shein kuwa Tamasha hilo la 27 lina lengo la kuwaalika
wanamuzi kutoka pembe zote za bara la Afrika ikiwemo Zanzibar ambayo tayari
imeshashirikiana nayo katika masuala mbali mbali ya kisanii na filamu.
Alisema kuwa
katika sherehe hiyo kutakuwa na nafasi maalum kwa Kamisheni ya Utalii Zanzibar
kuelezea juu ya utalii wa Zanzibar pamoja na vivutio mbali mbali vilivyopo
nchini jambo ambalo litapelekea kuwavutia watalii wengi kutoka Ulaya kuja
Zanzibar.
Pamoja na hayo,
Dk. Oschman alitoa mwaliko rasmi kwa Dk. Shein ili kushiriki katika Tamasha
hilo na kueleza kuwa Zanzibar itapata
nafasi ya kuonesha utamaduni wake, maisha ya Mzanzibar, kazi zake za sanaa na
vivutio mbali mbali vilivyomo ndani ya Zanzibar.
Aidha, Dk.
Oschman alisema kuwa Tamasha hilo linatarajiwa kuhudhuriwa na watu wapatao laki
moja kutoka nchi mbali mbali za Duniani wakiwemo viongozi wa ngazi za juu
kutoka nchi za Ulaya ikiwemo mwenyeji Ujerumani pamoja na Mabalozi
wanaoziwakilisha nchi zao nchini humo.
Katika mazungumzo
yake hayo Dk. Oschman alisema kuwa tayari ujumbe huo umeshakutana na kufanya
mazungumzo na viongozi wa juu wa Wizara husika pamoja na wasanii mbali mbali
ambao wanatarajia kushiriki katika tamasha hilo.
Wakati huo huo, Dk. Shein alifanya mazungumzo na Balozi wa Misri
nchini Tanzania Mhe. Hossam Moharam Ikulu mjini Zanzibar ambapo katika
mazungumzo hayo viongozi hao walisisitiza haja ya kuendeleza uhusiano na
ushirikiano uliopo.
Katika maelezo
yake Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Zanzibar inathamini uhusiano na
ushirikiano kati yake na misri hasa katika uimarishaji wa sekta ya elimu,
utamaduni pamoja na sekta nyengine za uimarishaji wa uchumi.
Nae Balozi
Moharam alimuhakikishia Dk. Shein kuwa Misri itaendelea kutoa ushirikiano wake
na kukuza uhusiano sambamba na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika juhudi
zake za kukuza uchumi na kuimarisha sekta zake za maendeleo kutokana na
mafanikio yaliopatikana chini ya uongozi wa Dk. Shein.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
0 Comments