Na Fatma Kassim
BARAZA la Tiba Asili na Tiba
Mbadala Zanzibar, limemfungia mganga wa kienyeji kutoka Rufiji, Omar Ali,
kufanya shughuli zake za kiuganga Zanzibar kutokana na kukosa sifa za kufanya kazi
hiyo.
Mrajis wa Baraza hilo, Haji
Juma Kundi, alisema uamuzi huo umekuja
kutokana na kuwepo wimbi kubwa la waganga wasio na uwezo wa kufanya tiba hiyo
na badala yake wanawadanganya wananchi.
Alisema mganga huyo kwa
kushirikiana na wenziwe wanazunguka katika vijiji tofauti na wanatumia njia mbali
mbali za kuwadanganya watu kuwa wamefanyiwa ubaya ili kujipatia fedha kwa
urahisi.
Alisema kufanya hivyo ni
kinyume na utaratibu wa baraza hilo ambapo wanafanya shughuli hizo bila ya kuwa
na vibali vinavyotolewa na baraza hilo.
Aliwataka wananchi wote wenye
nia ya kufanya shughuli hizo wafike katika baraza hilo kufuata maelekezo
ambayo yatawezesha waganga hao kufanya
kazi zao kwa utaalamu.
Kwa upande wa mganga huyo,
alikiri kuwa yupo katika shehia mbali mbali kwa nia ya kuwapatia tiba wananchi
wenye matatizo kwa kutumia vielelezo alivyotoka navyo Tanzania Bara ambavyo havitambuliwi
Zanzibar.
Aliomba kuongezewa muda wa
kufanya shuguli zake kutokana na kuwa ameshawaanzia dawa watu wengi.
Wakati huo huo baraza hilo
limefanya zoezi la kuwakamata wauza dawa za asili katika sehemu za misikiti na
sehemu zilizowazi kutokana na kuwa dawa wanazouza kukosa ubora na kusababisha
maradhi mbali mbali kwa watumiaji.
Mrajis wa Baraza hilo alisema
wameamua kufanya zoezi hilo kutokana na kuwa hivi sasa kumekuwa na wimbi kubwa
la wauza dawa katika sehemu za misikiti na sehemu za wazi ambazo zinakuwa si
salama.
0 Comments