Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imesema haitobadilisha
uamuzi wake wa kulifanyia ukarabati jumba la treni liliopo eneo la biashara
Darajani ambalo lipo hatarini kuporomoka.
Waziri wa Ardhi, Makazi Maji na
Nishati, Mhe. Ramadhan Abdalla Shaaban, aliyasema hayo katika ukumbi wa Mamlaka
ya Mji Mokongwe kabla ya kuvunja kikao, kutona na wafanyabiashara katika jumba
kuingia mitini.
Alisema uamuzi wa serikali wa
kuwahamisha wapangaji na wamiliki wa jumba hilo, hauna dhamira mbaya isipokuwa
ni kuokoa maisha ya watu na mali zao sambamba na kuzuia maafa yasiokuwa ya
lazima.
Aidha alisema iwapo
kutajitokeza tatizo lolote litakaloathiri maisha ya watu na mali zao kupitia jumba
hilo bila ya shaka mzigo mzito wa lawama
itabebeshwa serikali.
Hivyo, alisema uamuzi wa
kuwahamisha watu wote katika jumba hilo hauna mjadala mjadala kama wanavyotaka
watu hao bali ni wajibu wao kufuata maagizo ya serikali ili kuepusha vifo visivyo vya lazima.
Mkurugenzi wa Mkuu wa Mji
Mkongwe, Issa Sarboko,alisema kwa mujibu wa ukaguzi wa kina uliofanywa na
watendaji wa mamlaka hiyo, jumba hilo ni bovu na wakati wowote linaweza
kuporomoka na kusababisha mafaafa.
Alifahamisha kwamba miongoni
mwa mambo yaliogunduliwa katika ukaguzi huo ambayo kama yataendelea kufumbiwa
macho yataathiri maisha ya watu ni pamoja na dari jumba hilo kuwa katika hali
mbaya kwa sababu kwa muda mrefu yaijafanyiwa matengenezo,kuvuja kwa paa na vyoo
na kuta kufanya nyufa.
“Watumiaji walio wengi wa jumba
hili hawajali hali hiyo kwa kuwa wamegeuza ghala za bidhaa zao huku wakisahau
kama eneo lile linatumiwa na watu hivyo kama litajitokeza tatizo litawakumba
watu wengi,”alisema.
Mkurugenzi wa Nyumba na
Maendeleo na Makaazi, Ali Mwinyigogo, alisema kitendo cha kutohudhuria kwa
walengwa si jambo la busara kwani kikao hicho ndicho kitachotoa fursa kwa wao
kusikilizwa.
Alisema barua zilitolewa kwa
wale wote ambao wamekuwa na mikataba halali lakini jambo la kusikitisha hawakufuata
maelekezo ya wito na hatimae wameunda kamati ambazo hazitoweza kutimiza dhamira
ya kikao hicho wakiwa wao peke yao.
Mmiliki wa mlango wa duka
katika jengo hilo, Saleh Said Abdalla, alikiri jumba hilo ni bovu na kwamba
uamuzi wa serikali wa kulivunja ni wa busara.
0 Comments