Na Haji Nassor, Pemba
MAJAJI na Mahakimu nchini, wameshauriwa kuzitolea maamuzi ya haraka kesi
zinazohusiana na uchaguzi,badala ya kuziweka hadi miaka mitatu kwani kufanya
hivyo kunaondoa maana kwa wananachi au vyama kulalamika uchaguzi mahakamani.
Hayo yalielezwa na Mkuu
wa Mkoa wa Kusini Pemba,Mwanajuma Majid Abdalla, alipokuwa akizungumza kwenye
maadhimisho ya siku ya sheria Zanzibar yaliyofanyika uwanja wa tenis mjini
Chake Chake Pemba.
Alisema ili wananchi na
vyama vione umuhimu wa kupeleka kesi zao mahakamani pale wanapoona
hawakutendewa haki kwenye chaguzi, basi ni vyema uamuzi ukatolewa kwa wakati
muafaka.
Alisema kesi kama za
uchaguzi hazifai kuendeshwa pole pole hadi kufikia kuvuka miaka mitatu, na
kufanya hivyo ni kupoteza maana.
“Sio busara hata kidogo
kuona kesi za uchaguzi zinakaa muda mrefu mahakamani, kwani kufanya hivyo
hakuleti maana hata kidogo kwa vyama au wananchi kulalamikia uchaguzi,”alifanaua.
Katika hatua nyengine, Mkuu
huyo wa Mkoa aliwataka Mahakimu na Majaji
kuendelea kutoa haki kwa wanaostahili.
Kwa upande wake wakili
wa kujitegemea,Yussuf Mohamed, wakati akisoma risala kwa niaba ya wanasheria wa
kujitegemea, alisema bado baadhi ya Mahakimu na Majaji wamekuwa wakizizorotesha
kesi zinazohusiana na uchaguzi.
Alitoa mfano kwamba
tokea kumalizika kwa uchguzi mdogo wa jimbo la Bububu Unguja mwaka 2012 hadi
leo kesi hiyo imeshindwa kutolewa uamuzi.
Aidha alisikitishwa na
kitendo cha baadhi ya Majaji, Mahakimu na Waendesha Mashitaka, kuingilia kazi
zao na kuwapa wakati mgumu wanapokua mahakamani.
Hata hivyo, alisema
kutokuwepo kwa Majaji wakaazi kisiwani Pemba kati ya wale sita waliopo kisiwa
cha Unguja, husababisha mrundikano wa kesi kwenye mahakama kuu.
Kwa upande wake, Jaji wa
Mahakama Kuu Zanzibar, Mkusa Issac Sepetu, alisema changamoto ya uchakavu wa
majengo ya mahakama tayari imeanza kutatuliwa, kwa kufanyiwa matengenezo
makubwa Unguja na Pemba.
0 Comments