STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba 11.10.2015
WANACCM na wananchi kisiwani Pemba wametakiwa kutowachagua viongozi wa vyama
vya upinzani kikiwemo chama cha CUF kwani wamekuwa wakiwafanya vitega uchumi na
badala yake wawachague viongozi wa CCM ambao watawatekelezea mahitaji yao na
kuwaletea maendeleo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika
mkutano wa Kampeni ya uchaguzi wa CCM uliofanyika uwanja wa Pujini, Jimbo la
Chonga, Wilaya ya ChakeChake, Mkoa wa Kusini Pemba, viongozi wa CCM
waliohudhuria mkutano huo walisema kuna kila sababu ya kuwachagua viongozi wa
CCM ambao watakuwa nao wakati wote wa shida na raha.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM ambaye pia,
ni Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Iddi aliwataka wananchi wa Pemba
kufanya mabadiliko na kuwaeleza kuwa viongozi wa CUF wataendelea kuwafanya
vitenga uchumi kama hawakuwatambua ujanja wao kuwa wakishakuwachagua tu
huwakimbia.
Alisema kuwa viongozi wa chama cha CUF
hawana nia ya kuwapa maendeleo, na kueleza kuwa katika Bunge la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kuna Mifuko ya Majimbo
ambapo viongozi hao hupewa fedha kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wao Majimboni.
Balozi Seif alitolea mifano ya Majimbo
ambayo hayafaidiki na mifuko hiyo kama likiwemo Jimbo la Mji Mkongwe ambalo
Mwakilishi ameukacha Mfuko huo na kuwanyima wananchi waliomchagua kuwanyima
fursa ya kuatekeleza miradi ya maendeleo ambayo wangeliitekeleza kupitia mfuko
huo.
Alisema kuwa iwapo watawachagua viongozi
wa CCM watakuwa karibu nao na watafaidika na Mfuko huo pamoja na kuwasaidia
katika kutekeleza miradi ya mbali mbali ya maendeleo Majimboni mwao.
Balozi Seif aliwasisitiza kutokubali
kuuza vitambulisho vyao vya kupigia kura pamoja na kuwatahadharisha wanaCCM kwa
wale vijana wa CUF wanaochukua sare za CCM kuwa waangalifu nao ili wasije
kuzitumia kwa lengo la kuwahujumu wanaCCM.
"Watu hawa hawana nia njema kwani
wamekuwa wakisema kuwa mara hii CCM watatukoma...najua maana ya neno hili ni
kufanya vurugu lakini wajue kuwa vyombo vya ulinzi vipo",alisema Balozi
Seif.
Aidha, Balozi Seif Alisema kuwa viongozi
wa CUF wamekuwa wakiwadanganya wananchi na wafuasi wao kuwa mwaka huu
watashinda uchaguzi jambo ambalo haliwezekani na kusisitiza kuwa mwaka huu ndio
mwisho wa chama cha CUF.
Aliwataka wanaCCM kuendelea kupamba
bendera zao na picha za viongozi wao pamoja na kupamba Maskani, nyumba na
Matawi yao kwa lengo la kusherehekea ushindi wa CCM kwani ndio chama
kinacholeta maendeleo Zanzibar.
Alisisitiza kuwa chama cha CUF hakina lengo la kuwaletea maendeleo
wananchi wao na kazi yao baada ya kupata uongozi ni kuwakimbia wananchi
waliowachagua na kwenda katika miji ya Dodoma, Unguja na Dar-es- Salam.
Waziri wa Maji, Ardhi na Nishati ambaye pia, ni Mjumbe wa Halmashauri
Kuu ya Taifa, Ramadhan Abdalla Shaaban aliwataka wananchi wa kisiwa cha Pemba
wasikubali kudanganyika kwa suala la mafuta kama linavyozungumzwa na vyama vya
upinzani.
Alisema kuwa suala la mafuta na gesi
litachukua muda mrefu sana kutekelezwa na kueleza jinsi juhudi zilivyochukuliwa
na Dk. Shein katika kulisimamia suala hilo na kuliendeleza vyema kwa
mashirikiano na Rais Jakaya Mrisho Kikwete.
Alisema kuwa CCM inatenda na itaendelea
kutenda yale yote inayoyaahidi na kuwataka wananchi wa Pemba kuwachagua
viongozi wa CCM ili kwenda vizuri na kupata maendeleo.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Maua Abeid
Daftari kwa upande wake alisema kuwa Dk. Shein ametekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi ya CCM hivyo kuna haja ya
kumchagua ili aendelee kuwa Rais wa Zanzibar.
Alisema kuwa Dk. Magufuli na Dk. Shein ni
wachapa kazi na amefanya nao kazi na anawafahamu vizuri huku akisisitiza kuwa
wanaweza kuongoza kutokana na uzoefu mkubwa na uadilifu wao.
Aliwataka wananchi wa Wilaya ya Chake
likiwemo Jimbo la Chonga hasa Pujini kuwachagua viongozi wa CCM ili wawasaidie
katika kuwaletea maendeleo kwani hao waliowachagua katika uchaguzi uliopita
hawawasaidii wananchi wao na wamekuwa wakichukua fedha kwenye vyombo vya
kutunga sheria na kufanyia shughuli zao binafsi.
Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Asha
Abdalla Juma alieleza sababu mbali mbali za kuwachagua viongozi wa CCM kwani
wana sifa za kutosha, waadilivu, makini, wakweli na wachapakazi na kuwataka
wawachague.
Akizieleza sifa za Mama Samia Suluhu Hassan,
Asha alisema kuwa wanawake wanaweza na wataendelea kuweza ndani ya CCM na
kukipongeza chama hicho kwa kuwajali wanawake na hatimae kuwapa uongozi mkubwa.
Alisema kuwa Mama Shein na Mama Balozi
wametoa milioni 389 kwa vikundi mbali mbali vya akina mama Unguja na Pemba ambapo
miongoni mwa fedha hizo milioni 54 vilipewa vikundi vya Pemba na kusema kuwa
hiyo yote ni azma yao ya kuwasaidia wanawake kupata maendeleo.
Asha alieleza kuwa uchumi wa Zanzibar
umeimarika chini ya uongozi wa Dk. Shein, na kumsifu hatua alizochukua katika
kusimia maendeleo ya nchi sambamba na kuongezeka kwa uajibikaji kwa
wafanyakazi.
Aliwataka wananchi kumchagua Dk. Magufuli
kwa lengo la kuendeleza na kuimarisha Muungano, Samia Suluhu pamoja na Wabunge,
Wawakilishi, Madiwani.
Kaimu Katibu Mkuu wa Vijana Tanzania
Shaka Hamdu ambaye pia, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM alisema kuwa ASP ya
mzee Karume ndio CCM ya leo kutokana na kutekeleza vyema ahadi zake na kuwaomba
vijana wenzake kuendelea kuiunga mkono CCM.
Aliwahakikishia wananchi wa Pemba kuwa
ushindi wa CCM hauepukiki na Dk. Shein ndio atakae kuwa Rais kwani ni muungwana
na bingwa kwa kuahidi na kutekeleza ambaye pia, ni mvumilivu na MwanaCCM
kindakindaki.
Aliongeza kuwa Dk. Shein ni jasiri wa
kusimamia maendeleo na kuwaambia kwua kupiga kura ndio haki ya msingi lakini
kumwaga damu haikubaliki Tanzania hivyo wasidanganyike na wale wasio hubiri
amani na utulivu .
Shaka alisisitiza amani na utulivu na
kuwaasa vijana kuimarisha umoja wao na kueleza kuwa kwa wale wote wanaotumia
majukwa kutangaza kuvuruga amani hawana maslahi na wananchi.
Aliwataka wanaCCM na Wananchi mara baada
ya kumaliza kupiga kura warudi majumbani na kusema kuwa CCM ni chama kikubwa na
kueleza kuwa kusimamishwa kwa Dk. Shein kuwa mgombea urais wa Zanzibar haikubahatishwa.
Alisema kuwa CCM ilitambua kuwa mgombea
nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia UKAWA hana soko na
atakapokatwa kwenye CCM anakwenda upinzani na huko anakwenda kuvimaliza vyama
vya upinzani.
Alitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa kuandaa
mazingira mazuri ya ajira kwa vijana.
Nae Modelin Kastiko alieleza mafanikio
yaliopatikana katika sekta ya elimu na maji pia, alieleza kuwa hapo siku za
nyuma kulikuwa na matatizo makubwa ya maji ambapo kwa hivi sasa tatizo hilo
limebaki kuwa historia.
Nao viongozi wa Mkoa wa Kaskazini kwa
nyakati tofauti walisisitiza haja ya kuendelea kusimamia amani na utulivu na
kuwataka vijana wanaotumiwa kuja kufanya fujo siku ya uchaguzi kuachana na azma
yao hiyo.
Viongozi hao walieleza kuwa WanaCCM wa
Wilaya ya ChakeChake waliahidi kuwa kura zote watapewa wagombea wa CCM, huku
wakimuhakikishia ushindi Dk. Shein kuendelea kuwa Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
1 Comments
Inamaana hawa CCM hadi leo wanafikiri vijana wapo na mawazo yale yale ya 1964? miaka zaidi ya 50 hatukuwahi kuona wabunge wa CCM wakituletea hizo pesa wanazopewa bungeni seuze leo!!! safari hii vijana tumeamua ni mabadiliko kwenda mbele ccm inafaa kukaa chonjo kusubiri 1920 kuja na sera nyingine.
ReplyDelete