Na Mwandishi Wetu Pemba.
MGOMBEA Urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk. Ali Mohammed
Shein amesema kuwa juhudi za kuimarisha lugha ya Kiswahili na kuzifanya lahaja
za Kiswahili za Zanzibar kuwa chimbuko la Kiswahili fasaha zitaendelezwa katika
miaka mitano ijayo chini ya uongozi wa chama hicho.
Akizungumza na wananchi pamoja na WanaCCM
waliohudhuria katika mkutano wa Kampeni za uchaguzi kwa upande wa CCM
uliofanyika uwanja wa Pujini, Jimbo la Chonga, Wilaya ya ChakeChake, Mkoa wa Kusini
Pemba, Dk. Shein alisema kuwa tayari Kamusi za lahaja za Kipemba, Kimakunduchi
na Kitumbatu zimechapishwa na kusambazwa kwa wananchi.
Alisema kuwa hatua ya ukaguzi wa kazi za
sanaa kwa lengo la kulinda na kuhifadhi mila, desturi na silka za Mzanzibari
imetekelezwa na kusisitiza kuwa kituo kikuu cha lugha ya Kiswahili kwa nchi za
Afrika Mashariki kitakuwa Zanzibar kwani ndio chimbuko ya lugha ya Kiswahili.
Akieleza kuhusu uimarishaji wa viwanja
vya michezo, Dk. Shein alisema kuwa tayari uwanja wa Amani umewekewa nyasi za
bandia, njia za kukimbilia na kwa upande wa uwanja wa mpira wa Gombani Pemba
nao umeiwarishwa kwa kuwekewa nyasi za bandia, taa, kujengwa paa jipya na hivi
sasa mchakato wa ujenzi wa njia za
kukimbilia unaendelea katika kiwanja hicho.
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa ujenzi wa
kiwanja kipya cha michezo cha Mao Tse Tung unatarajiwa kuanza mapema mwezi
Februari mwaka ujao hatua ambayo baada ya kukamilika kwa ujenzi huo wa kiwanja kipya
na cha kisasa kitasaidia kwa shughuli za michezo na sherehe za kimataifa.
Tayari Sera na Sheria zinazoongoza
Utamaduni zimefanyiwa mapitio ili kukidhi matarajio na mahitaji ya wakati na
sheria mpya ya Baraza la Sanaa na Sensa ya Filamu na Utamaduni imetungwa.
Ambapo chini ya Sheria hiyo Bodi ya Sensa
ya Filamu na Baraza la Sanaa la Zanzibar vimeunganishwa.
Pamoja na hayo, utafiti wa Urithi wa
Utamaduni usioshikika umefanyika na matokeo ya utafiti huo yameweza kuhifadhiwa
Kimataifa na kuingizwa katika orodha ya UNESCO ya tamaduni zinazohifadhiwa.
Sambamba na hatua hiyo matokeo ya utafiti
huo pia, yamerejeshwa kwa wananchi wa maeneo husika ili kuzitumia kama sehemu
ya ajira na kupambana na umasikini.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kusisitiza azma
ya Serikali ya Mapinduzi ya Znzibar chini ya uongozi wa CCM kuimarisha sekta ya
michezo nchini huku akisisitiza kupewa kipaumbele kwa michezo yote pamoja na
wanamichezo wake.
0 Comments