6/recent/ticker-posts

Dk Shein azindua Tawi jipya la CCM Mombasa kwa Mchina na kuwataka wanaCCM kujitokeza kwa wingi Okt 25


  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                         17.10.2015
---
MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein ameendelea kuwasisitiza wananchi na wanaCCM kuitumia vyema haki yao ya msingi ya kupiga kura siku ya Oktoba 25 mwaka huu na kuwataka mara tu baada ya kumaliza upigaji kura warudi majumbani.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwasisitiza wananchi na wanaCCM kuwa kwa mujibu wa Sheria za Tume ya Uchaguzi chombo chenye mamlaka ya kulinda kura siku hiyo ni Tume hiyo ya Uchaguzi na kwa kushirikiana na Vyombo vya dola vyote kwa pamoja vitahakikisha hilo linatendeka na kuwataka wananchi hasa vijana kutokubali kutumiliwa na watu wachache katika kuvuruga amani.

Hayo aliyasema leo katika uzinduzi wa Tawi jipya la CCM la Mombasa Kwamchina, liliopo Wilaya ya Dimani, Mkoa wa Magharibi Kichama, Jimbo la Kiembesamaki Zanzibar.

Aidha, DK. Shein ambaye pia, ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliwataka wananchi baada ya kumaliza kupiga kura warudi majumbani na kusubiri kutangaziwa mshindi na kuwaeleza kuwa ulinzi wa kisheria wa kura ni wa vyombo vya kisheria vilivyowekwa maalum.


Dk. Shein aliwahakikishia wanaCCM kuwa atarudi Ikulu baada ya kura nyingi watakazompa wananchi kutokana na kumkubali na kuzikubali Sera za chama chake.

Aidha, alitoa pongezi kwa Balozi Seif Idd kwa  kufanikisha kupatikana kwa kiwanja hicho pamoja na wanaCCM wote waliowezesha ujenzi huo na kueleza kuwa jitihada zake na zile za wanaCCM za kukilinda na kukitetea chama na juhudi za Serikali ndio sababu za kuhemkwa kwa wapinzani.

Alisifu hatua za kujitolea ndani ya chama cha CCM ambazo juhudi hizo zilianzwa na muwasisi wa ASP Mzee Abeid Karume na kusema kuwa CCM ina kila sababu ya kufanya juhudi kutokana na historia yake kwani ndio chama chenye historia ya ukombozi wa Zanzibar na kueleza kuwa kamwe vyama vyengine haviwezi kulingana na CCM.

Alisema kuwa viongozi wa CCM ni viongozi mahiri na wana uwezo wa kuongoza Dola na ndio Zanzibar imeweza kupata mafanikio kutokana na uongozi wa CCM na kuwasisitiza wanaCCM kuendeleza wajibu wao, wakitumikie chama na Serikali yao.

Alisema kuwa ujenzi wa jengo hilo unaenda sambamba na mradi wa CCM wa kumarisha chama, na kutolea mfano wa kuzinduliwa kwa jengo jipya la CCM huko Dodoma mwezi Julai mwaka huu, ujenzi wa jengo la UVCCM  lenye ghorofa 32 lililojengwa huko Dar-es-Salaam yote hayo ni uamuzi thabiti wa kuiimarisha CCM.

Dk. Shein, alipongeza azma ya Tawi hilo ya kujenga maduka, mafunzo ya kompyuta, ushoni na ukodishwaji wa ukumbi wa mkutano,kuwaenzi wajasiriamali, shughuli za kijamii na kuwataka kuongeza kasi katika mipango hiyo kwa lengo la kuimarisha maslahi ya wanaCCM wa Tawi hilo.

Aidha, Dk. Shein alifurahishwa na azma ya Tawi hilo kutoa elimu ya itikadi na kutoa nasaha kwa vijana kutokuba kupotoshwa na watu wasioitakia mema nchi yao ambao wako tayari kufanya lolote kwa ajili ya kulinda maslahi yao binafsi, bila ya kujali hali na maisha ya wengine.

Dk. Shein aliwahimiza vijana kujitokeza kwa wingi huku wakiwa na ari na hamasa ya kupokea mafunzo hayo ya itikadi na historia ili wawe na moyo wa kizalendo na utayari wa kuitumikia na kuilinda nchi yao.

Ni jukumu lao la kuwaeleza historia ya chama chaio kilipotoka, kilipo na kinapokusudia kwenda na kama hakikufanyika hicho ndipo vijana wanapoanza vurugu barabarani.

Kuna kila sababu ya kuwafundisha vijana historia na kuwaambia ukweli wa mambo yalivyokuwa na kuwaeleza kuwa Zanzibar ni nchi ya watu wote na ilikuwa Zanzibar na itaendelea kuwa Zanzibar na itaongozwa na Wazanzibar ambao wana historia ya Zanzibar.

Alisema kuwa wanaCCM wana ulezi mkubwa katika kuwaeleza vijana kuijua historia ya nchi yao sambamba na kuzingatia silka na maadili ya Kizanzibari.

Alieleza matumaini yake kuwa tawi hilo litatoa elimu kwa CCM, na kuwataka vijana kujitokeza kuwenda kupokea elimu ya itikadi na kueleza kuwa mafunzo ya itikadi yanatoa elimu kubwa.

“Mafunzo ya itikadi ndiyo wanayoyafanya vijana katika nchi za wenzetu kuwa na moyo wa kizalendo na uchungu wa nchi yao”,alisema Dk. Shein.

Alieleza kuwa siri kubwa  ya maendeleo ya nchi zinazoendelea ni mafanikio waliyoyapata katika kuwakuza vijana wao wakiwa na mapenzi na moyo wa kizalendo kwa nchi zao popote walipo.

Dk. Shein alisema kuwa CCM ni chama makini chenye uwezo wa kuongoza watu na kusisitiza kuwa kila mmoja ana ruhusa ya kusema kwa vile kila mmoja ana mdomo wa kusema lakini cha ulazimu ni kuangalia anachosema nini na anasema wapi jambo ambalo CCM hilo inalijali.

Sambamba na hayo, Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alitumia fursa hiyo kuwaeleza wanaCCM kuwa wanajukumu la kuwashawishi wale wachache ambao hadi sasa hawajafikia maamuzi ya busara ya kukichagua Chama  Cha Mapinduzi ili kiendelee kuwatumikia wananchi na kuwaletea maendeleo ya haraka nchi yao.
 
Mapema Mwenyekiti wa ujenzi wa Tawi hilo Ahmada Yahya Abdulwakil alisema kuwa  Tawi hilo ni miongoni mwa matawi ya CCM yaliyomo katika Mkoa wa Magharibi Wilaya ya Dimani kichama, Jimbo la Kiembesamaki.

Alisema kuwa chimbuko laTawi hilo ni utekelezaji wa maelekezo ya katiba ya CCM Ibara ya 31 (2) kinachosema kuwa Tawi litafunguliwa tu iwapo mahala hapo panapohusika kuwa na wanachama wanasiopungua 50 na wasiozidi 600.

Mwenyekiti huyo alisema kuwa Wazo la ujenzi wa Tawi hilo lilibuniwa na wanachama wa CCM wa tawi hilo baada ya kuona ipo haja ya kutanua wigo ili kukiwezesha chama hicho kutekeleza vyema majukumu yake katika eneo hili kwa urahisi zaidi. Aidha, wazo hilo ni utekelezaji wa mradi wa kuimarisha CCM Awamu ya Tatu.

Alisema kuwa kabla ya kuanzishwa kwa tawi hilo wanachama wa tawi la CCM kwa mchina walikuwa wakitumia tawi la CCM, Tomondo na wakati wakiwa katika heka heka za dhamira za ujenzi wa tawi hilo walikuwa wakifanyia shughuli zao mbali mbali za kichama kwa mwanachama mwenzao muanzilishi bi Khadija Kassim Shamte.

Walitoa shukurani kwa Balozi Seif Idd kwa kupatikana eneo hilo ambapo shughuli za ujenzi zilianza rasmi Septemba 28 mwaka 2013 ujenzi mara tu baada ya kubapatikana hati miliki ambapo jiwe la msingi liliwekwa Disemba 27 mwaka 2014.

Katika ujenzi huo wanachama mbali mbali wa CCM walichagia akiwemo Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein ambaye alitoa T.shs 17,000,000 ambazo zilisaidia kumalizia ujenzi wa Tawi hilo,na Balozi Seif Idd ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM alitoa T. shs. 5,800,000 pamoja na Tsh. milini 4 kwa ajili ya kununulia mbao za kuezekea.

Ahmada alisema kuwa hadi kumalizika kwa jengo hilo jumla ya T.shs. milioni 79.340,000 zimetumika.

Nae Mwenyekiti wa Tawi la Mombasa Kwamchina, Bi Subira  Kahalan Urua alitoa pongezi wka Kamati ya Ujenzi na wananchi na wanachama wote waliohuidhuria  pamoja na waliochangia ujenzi huo.

Nae Balozi Seif Ali Idd, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alitumia fursa hiyokutoa shukurani kwa wanaCCM wa Tawi la Mombasa Kwamchina na kuwapongeza kwa michago yao na kuwasisitiza wanaCCM kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura

Mwenyekiti wa Mkoa wa Magharibi Yussuf Mohammed alisema kuwa ufunguzi huo ni sehemu ya ushindi wa chama hicho.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

Post a Comment

0 Comments