6/recent/ticker-posts

Kituo cha afya Wesha huwachwa wazi bila ya kuwepo madaktari


NA HAJI NASSOR, PEMBA


MALI za wizara ya afya zilizomo kituo cha Afya Wesha wilaya ya Chakechake Pemba, ziko hatari kuibiwa wakati wowote, iwapo mtindo kukifungua kituo hicho na kukiwacha wazi kwa muda, unaofanywa na madaktari hawatouwacha.

Madaktari kwenye kituo hicho, wamekuwa na mtindo wa kikufungua kituo hicho na kisha kurudi nyumbani, hasa kwa yule daktari aliejengewa nyumba karibu kituo hicho.

Imefahamika kuwa, utaratibu wa kukiwacha wazi kituo hicho na kisha kurudi tena nyumbani, ndio wa kawaida kwa madaktari hao, jambo linaloweza kusababisha wizi kwa njia rashisi.

Hayo yamegunduliwa na Kamati ya maofisa wadhamini kisiwani Pemba, ilipofanya ziara ya kushitukia, walioifanya kwenye Kituo hicho majira ya saa 1:38 asubuhi, ili kuangalia mwenendo wa utendaji kazi kwenye sekta ya afya.

Akizungumza na madaktari hao baada maofisa wadhamini hao kukitembelea kituo hicho kikiwa wazi, pasi na kuwepo daktari yoyote, Afisa Mdhamini anaeshughulikia Utumishi wa Umma Pemba, Massoud Ali Mohamed, alisema lazima sheria na kanuni za Utumishi wa umma zifuatwe kwa vitendo.

Aliwaeleza kuwa mtindo wa kukifungua Kituo hicho cha Afya na kukiwacha wazi, unaweza kuwasababishia hasara, iwapo atatokezea muhalifu na kufanya hujuma kwenye jengo hilo la serikali.

“Tumekikuta kituo kiko wazi, sisi tumeingia vyumba vyote viko wazi na hapana hata mlinzi, zaidi ya mama mjamzito tuliemkuta, sasa hapo inaweza kuwa rahisi kufanyika kwa wizi’’,alifafanua.

Mdhamini huyo, alisema alipomuhoji mama huyo mjamzito, alimueleza kuwa, ndio kawaida kwa kituo hicho cha afya cha Wesha, kuanza kutoa huduma saa 3:00 licha ya kufunguliwa saa 1:00.
Nae Afisa Mdhamini anaeshughulia wanawake na watoto Pemba, aliekuwemo kwenye ziara hiyo Khadija Khamis Rajab alisema uhaba wa madatari kwenye kituo hicho isiwe sababu ya kikufungua Kituo hicho, na kikiwacha wazi kwa madai ya machofu.

“Bora mchelewe kikufungua, ingekuwa afadhali, kuliko kikifungua mapema na kisha mkarudi nyumbani, au kwa sababu mtu yuko karibu anakwenda kazini, hili sio sahihi”,alifafanua.

Madaktari waliofika kituoni hapo nusu saa baadae, waliwaeleza maofisi hao wadhamini kuwa, wamekuwa wakifanya kazi nje ya wakati na kuondoka hapo wakiwa wamechoka.

“Tukiondoka hapa siku nyengine tumechoka, maana tuko wachache, kazi inakuwa inapindukia muda, sasa tukifika majumbani tumechoka na asubihi huchelewa kuja’’,alisema daktari mmoja.

Aidha madaktari hao, waliwaahidi maofisa wadhamini hao kuwa mtindo wa kukifungua kituo hicho na kisha kuondoka, utakoma kwani hufanya hivyo kwa dharura.

Hata hivyo wamewaomba kuhakikisha wanalitafutia ufumbuzi tatizo la uhaba wa watendaji kwenye kituo hicho, kwani  ikitokezea mmoja amepata dharura utoaji wa huduma husuasua.

 Wakati huo huo maofisa wadhamini hao, wamemuagiza daktari aliekifungua kituo hicho cha afya Wesha, na kikiacha wazi kwa zaidi ya nusu saaa, kuandika barua haraka ya kujieleza sababu zilizomsukuma kufanya hivyo.

“Huyu daktari ambae amejengewa nyumba na serikali, ili aishi karibu na Kituo cha Afya, akaamua kukifungua na kisha kurudi kwake, mwambieni aandike barua ya kujieleza, kwa kukitelekeza kituo”,alisema Mdhamini wanawake na watoto.

Baadhi ya wananchi wanaokitumia kituo hicho, walisema ni jambo la kawaida, kukikuta kiko wazi, pasi na kuwepo kwa daktari.

“Mimi juzi nilimpeleka mke wangu machana na kufika tukakaa kwa muda mrefu, na vyumba vyote tukavimaliza kumtafuta, hatujamuona daktari wowote’’,alifafanua Mohamed Juma Abdi.

Maryam Mohamed Ali, alisema hawaoni faida kubwa ya kuwepo kwa kituo hicho, kutokana na madaktari waliopo kutokaa sehemu yao ya kazi, kwa wakati husika.

“Sisi wajawazito tunapokwenda na watoto wetu kwanza usubiri daktari pengine yuko kwake, au hao wengine hawajafika au wametoka ndio yaliopo pale’’,alifafanua .

Naibu sheha wa shehia ya Wesha Haji Mohamed Ali, alikiri kuwepo kwa tatizo hilo, na kuiomba wizara ya afya kuajiri watu wenye hamu na nidhamu ya kazi.

“Kituo cha afya kipo na dawa zipo, lakini ukifika mara kwanza daktari mmoja hayupo, mwengine kwenda nyumbani hili lazima lishughulikiwe ili wananchi waone faida ya kuwepo kwa Kituo hicho’’,alishauri sheha huyo.

Safia Ali Kwale (50), alisema mwaka jana alipokwenda kwenye kituo hicho alipata huduma mzuri na hakuona mashaka yoyote kwa madaktari hao.

“Mimi sio mara nyingi kwenda kituo chetu cha afya, lakini nilipokwenda hawajanidharau na nimewakuta juu ya viti vyao tayari kwa kuhudumia wananchi’’,alifafanua.

Uchunguuzi uliofanya na mwandishi wa habari hizi, umebaini kuwa kituo hicho cha afya kinadaktari mmoja mzalishaji, mmoja wa kawaida na kukosekana kwa odali jambo linalotajwa kuwapa kazi ya ziada watendaji waliopo.


Katika siku za hivi karibuni kamati ya maofisa wadhamini Pemba, imekuwa ikiandaa ziara ya kushitukizia kwenye wizara, taasisi na mashirika ya umma, ili kuangalia uwajibikaji ukiwemo wa muda wa uingiaji na utokaji wa kazini.

Post a Comment

0 Comments