6/recent/ticker-posts

WAFAMASIA Nchini Wametakiwa Kuandaa Mpango Mkakati wa Usalama wa Dawa Katika Ngazi ya Afya ya Msingi

Na.Mwandishi Wetu

WAFAMASIA nchini wametakiwa kuandaa mpango mkakati wa usalama wa dawa katika ngazi ya Afya ya Msingi ili kuhakikisha dawa zinahifadhiwa na kusimamiwa ipasavyo zinapofikishwa katika vituo vyao vya afya.

Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt Mngereza Mzee Miraji, alipokuwa akifunga kikao cha kutathmini mnyororo wa ugavi wa dawa na bidhaa za afya, kilichofanyika katika Hoteli ya Golden Tulip, Malindi Zanzibar.

Amesema kuwa, kutokana na mabadiliko makubwa yaliyofanyika katika sekta ya afya kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, ni wakati muafaka kwa wafamasia kuja na mpango mkakati unaoendana na kasi ya mabadiliko katika sekta hiyo pamoja na maendeleo ya teknolojia.

Dkt Mngereza amesema tathmini hiyo mpya inalenga kufanya uchambuzi wa kina wa hali halisi ya usimamizi wa mfumo wa ugavi wa dawa kuanzia ngazi ya taifa hadi kufikia vituo vya afya vya msingi, hatua itakayosaidia kubaini changamoto na fursa zilizopo katika mnyororo wa ugavi wa dawa.

Kwa upande wake, Mfamasia Mkuu kutoka Wizara ya Afya Zanzibar, Hidaya Juma Hamad, amesema tathmini hiyo itaisaidia Wizara kupanga na kuamua mifumo bora ya ugavi wa dawa ili kwenda sambamba na kasi ya ukuaji wa sekta ya afya hapa nchini.

Ameongeza kuwa tathmini hiyo pia itafanya ufautiliaji wa suala zima la matumizi holela ya dawa miongoni mwa wananchi na kuweka mikakati madhubuti ya kudhibiti matumizi yasiyo sahihi ya dawa hizo, jambo litakalosaidia kulinda afya za wananchi na kuongeza ufanisi wa huduma za afya.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la JSI (John Snow Incorporation),Dkt.Jema Bisimba, amesema mradi wa Ugavi Bora, Afya Bora unalenga kuboresha upatikanaji wa dawa katika jamii kupitia ushirikiano wa karibu na Wizara ya Afya Zanzibar.

Amesema mradi huo unatekelezwa na shirika la JSI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya Zanzibar, na umefadhiliwa na Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, ukiwa na lengo la kuimarisha mifumo ya ugavi wa dawa na bidhaa za afya kwa manufaa ya wananchi.

Kikao hicho kimewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya afya kwa lengo la kujadili na kutathmini kwa pamoja njia bora za kuimarisha usimamizi wa dawa na bidhaa za afya nchini.

Mwisho

Post a Comment

0 Comments