6/recent/ticker-posts

SMZ Kupitia Wizara ya Afya Imesema Itaendelea Kushirikiana na Washirika wa Maendeleo wa Sekta ya Afya Wakiwemo CDC na Amref

 Na.Omar Abdalla -Wizara ya Afya Zanzibar.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya imesema itaendelea kushirikiana na washirika wa maendeleo wa sekta ya afya wakiwemo CDC na Amref katika kuimarisha huduma mbali mbali Afya pamoja na Methadone (MAT) kwa waathirika wa dawa za kulevya.

Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Mngereza Mzee Miraji, aliishukuru Amref Health Africa Tanzania na (CDC) Tanzania kwa mchango wao mkubwa wa kuimarisha huduma za afya, hususan kwa makundi yaliyo katika hatari zaidi.

Aidha Dkt Mngereza alieleza kuwa licha ya Zanzibar kuwa na kiwango cha maambukizi ya VVU kilicho chini ya asilimia moja kwa idadi ya watu kwa ujumla, bado kuna changamoto kubwa kwa watu wanaotumia dawa za kulevya kwa njia ya sindano, ambapo maambukizi yanafikia asilimia 9.3. Alisisitiza kuwa huduma za MAT zimekuwa nyenzo muhimu ya kupunguza madhara, kuzuia maambukizi mapya ya VVU, na kuimarisha afya na maisha ya wananchi.

Amesema kwa kipindi cha miaka kumi CDC na Amref Afrika wameshirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya katika kuhakikisha kuwa maisha zaidi ya familia 1800 wamepatiwa huduma na kati hayo mia tatu wanaendelea na maisha yao ya kawaida.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa wa Amref Tanzania, Dkt. Florence Temu, amesema kuwa kupitia ushirikiano kati ya Amref Tanzania na CDC Tanzania, jumla ya watu 1,831 (wanaume 1,745 na wanawake 86) wamefikiwa na huduma za OAT/MAT hadi kufikia Desemba 2025.

Amefahamisha kuwa huduma hizo zimejumuisha upimaji na matibabu ya VVU, uchunguzi na tiba ya kifua kikuu, huduma za homa ya ini (hepatitis), pamoja na ushauri nasaha na elimu ya afya.

Aliongeza kwa kusema jumla ya wahudumu 21 wa afya na waelimishaji rika wamepatiwa mafunzo ya kitaalamu, huku watumishi watatu waliokuwa chini ya mradi wanatarajiwa kuajiriwa na Serikali kupitia mpango wa afya wa Zanzibar kwa lengo la kuhakikisha huduma zinaendelea kutolewa bila ya usumbufu wowote.

 Kwa upande wake Jonathan Grund Naibu Mkrurugenzi wa mirad Kituo cha Marekani cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano katika kuhakikisha kuwa huduma zinatolewa kwa ufanisi mkubwa na kuipongeza Wizara ya Afya kwa kuchukua jukumu la kuendeleza huduma hizo hapa nchini

Aidha amefahamisha kuwa CDC itaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali kupitia Wizara ya Afya za kuimarisha mifumo ya utoaji huduma ili wananchi wa Zanzibar wapate huduma zenye ubora na endelevu.

mwisho

Post a Comment

0 Comments