6/recent/ticker-posts

Serikali imeongeza tija ya uzalishaji wa kilimo cha mpunga kwa kutoa ruzuku

Waziri wa Kilimo Umwagiliaji Maliasili na Mifugo Suleiman Masoudi Makame akisisitiza jambo wakati akizungumza na Vyombo vya Habari kuhusiana na Mafanikio na Maendeleo ya Wizara kutimia Siku Mia Moja za Uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Hussein Ali Mwinyi kwa kipindi chake cha Pili hafla iliofanyika katika Ukumbi wa Habari Maelezo Rahaleo Zanzibar.

Na Maelezo Zanzibar  10.03.2026

Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifungo Mhe. Suleiman Masoud Makame amesema Serikali imeongeza tija ya uzalishaji wa kilimo cha mpunga kwa kutoa ruzuku inayowezesha upatikanaji wa zana za kilimo zinazotumika katika kutoa mafunzo kwa vijana wanaohudumia mabonde ya mpunga.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo kuhusu siku 100 za mafanikio ya uongozi wa awamu ya pili ya Dkt. Mwinyi amesema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa mageuzi ya sekta ya kilimo unaolenga kuwaunganisha vijana katika kuimarisha thamani ya kilimo.

Amesema kuwa lengo ni kuwaunganisha vijana hao na Taasisi za kifedha, ikiwemo Benki ya Kilimo Tanzania (TADB), ili kuwawezesha kupata mikopo nafuu kwa ajili ya ununuzi wa zana na teknolojia za kisasa.

Amefahamisha kuwa uanzishwaji wa kiwanda cha vifaranga vya kuku kilichopo katika eneo la Kwambani chenye uwezo wa kuzalisha vifaranga 30,000 kwa wiki ambapo mwekezaji mwingine katika eneo la Pangeni yupo katika hatua za mwisho za kukamilisha ujenzi wa kiwanda cha vifaranga pamoja na kiwanda cha uzalishaji wa chakula cha kuku, miradi hiyo inatarajia kuimarisha sekta ya ufugaji kuku na kupunguza utegemezi wa uagizaji kutoka nje.

Haya yote yasingewezekana bila ya uwepo wa mashirikiano mazuri baina ya wakulima, wafugaji na wataalamu wa wizara wenye jitihada za dhati na malengo ya pamoja ya kuleta mageuzi ya kilimo kutoka kilimo cha kujikimu na kuwa kilimo-biashara” ameeleza Mhe. Waziri.

Amewasisitiza vijana kujikita katika kilimo na ufugaji ili kujiimarisha kimaisha kwani sekta hiyo imekuwa ni mkombozi mkubwa katika kuleta maendeleo na kukuza uchumi wa nchi pamoja na kuinua kipato cha mtu moja moja.




Post a Comment

0 Comments