Habari za Punde

100% ZANZIBARI YATOA FORA KANGAGANI, PEMBA

Sherehe za maridhiano na umoja wa kitaifa zilizoandaliwa na taasisi ya Swahili Center zinaendelea kwa kasi ambapo kwa Jumamosi iliyopita, magwiji wa Taarab kutoka vikundi mchanganyiko vya Unguja na Pemba vilirindima katika kijiji cha Kangagani, Pemba.

Katika onesho hilo ambalo lilifanyika katika uwanja wa Skuli ya Kangagani, Wilayani Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba, wapenzi wa Taarab kutoka sehemu mbali kama vile Chake, Kambini na hata kutoka Mkoani waliliminika na kujimwaga katika burudani hizo zilizoanza saa 2 usiku.


Baadhi ya wasanii maarufu walioshiriki katika onesho hilo ni kama vile Bi. Fauziya Abdalla (Nadi Ikhwan Safaa), Taymour Rukun (Kalcha Music Club), Ali Said ‘Wazera’ (Light Star), Malik Hamadi ‘Wastara’ (Kiuyu-Minungwini), Makame Khamis Nyange ‘Prof. Gogo’ (Maendeleo Taarab) na wengine wengine kutoka vikundi vya Unguja na Pemba.

Kwa kuibusha hisia za mashabiki wao, wakali hao wa Taarab asilia walipiga vibao vingi vinavyopendwa vikiwemo ‘Ahadi’ (Fauziya Abdalla), ‘Kibali’ (Amina Abdalla), ‘Watu Wananiuliza’ (Sameer Basalama), ‘Mtoto wa Mjini’ (Fatma Ali Faki), ‘Mgomba’ (Said Dokoa), ‘Mpewa Hapokonyeki’ (Bahati Hamadi), ‘Vijumbajumba’ (Malik Hamadi Wastara) na Lulu (Prof. Gogo).

Katika kuutambulisha mradi huo kwa waliohudhuria onesho hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa Swahili Center Bw. Kheri Abdalla Yussuf, aliwajulisha wapenzi hao wa sanaa kuwa dhamira ya mradi huo ni kuimarisha misingi ya umoja wa kitaifa nchini Zanzibar kupitia sanaa za utamaduni zenye burudani na mafunzo kwa jamii yote.

Mradi wa 100% Zanzibari (tafsiri; Mzanzibari asilimia mia moja) umekuwa ukifanya maonesho katika Mikoa ya Unguja na Pemba kufuatia kambi za kisanii zinazoshirikisha fani za Taarab, Ngoma za Utamaduni na michezo ya Kuigiza. Shangwe hizo zimekuwa zikifanyika kwa awamu katika sehemu mbali mbali ambapo kwa hiki hii zitahamia katiak kijiji cha Nungwi, Mkoa Kaskazini Unguja.

Swahili Performing Arts Center (Kituo cha Sanaa za Maonesho cha Waswahili) ni taasisi ya iliyoanzishwa kwa dhamira ya kuchangia katika maendeleo ya sanaa za maonesho asilia za Zanzibar pamoja na zile za mwambao wa Waswahili kupitia uwezeshaji (wasanii), uzalishaji wa kazi za sanaa, maonesho na ushirikishaji jamii. Dira ya Swahili Center ni kuurejeshea hadhi utambulisho wa utamaduni wa Kiswahili.

Mradi wa 100% Zanzibari umedhaminiwa na Ubalozi wa Norway pamoja na kampuni ya mawasiliano ya Zantel.

Kwa taarufa na maelezo zaidi, tafadhali wasiliana nasi kupitia anuani zifuatazo: -

Kheiri A.Y. Jumbe
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji
Email: kheiri.jumbe@swahili-center.org
Mobile: 077.3620202

The Swahili Performing Arts Center
Ground Floor, Old Dispensary Building
Mizingani Road, Stonetown
Zanzibar, United Rep. of Tanzania

Email: info@swahili-center.org

Homepage: www.swahili-center.org

Facebook: Swahili Performing Arts Center

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.