Habari za Punde

Serekali kwa Sekta na Binafsi Inazijengea Mazingira Mazuri Skuli za Zanzibar

Na. Hassan Hamad (OMKR).

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad amesema serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi itahakikisha kuwa inazijengea mazingira mazuri skuli za Zanzibar ili kuwapa matumaini wanafuzni wanasoma masomo ya sayansi.

Amesema wanafunzi wengi wamekuwa wakikata tamaa kusoma masomo hayo kutokana na visingizio kuwa ni magumu, sambamba na ukosefu wa vifaa vya sayansi, mambo ambayo amesema serikai imejidhatiti kakabiliana nayo, ili kuwawezesha wanafunzi wengi zaidi kusoma masomo hayo.

Maalim Seif ametoa kauli hiyo leo huko skuli ya Mwanakwerekwe “C” katika mahafali ya tatu ya kidato cha sita na michepuo katika skuli hiyo.

Amesisitiza haja kwa wadau wa elimu kuwahamasisha wanafunzi kusoma masomo ya sayansi, hisabati na teknolojia, ili kwenda sambamba na ushindani wa soko la Afrika Mashariki na maendeleo ya kiuchumi duniani.

Amesema Zanzibar bado inakabiliwa na upungufu wa wataalamu wa fani mbali mbali zikiwemo uhandisi, udaktari na jiolojia, na kutaka juhudi za makusudi zichukuliwe ili kuziba pengo hilo.

“Ili tupate wahandisi, madaktari wa binadamu na wanyama, tupate wanajiolojia wa kushughulikia utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia, lazima wanafunzi wetu wapate msingi imara wa masomo ya sayansi, hisabati na teknolojia”, alisistiza.

Sambamba na hilo, Makamu wa Kwanza wa Rais amewahimiza wanafunzi kuwekeza katika kujifunza lugha mbali mbali za kigeni ikiwemo lugha ya kichina, ili kujiweka tayari kukabiliana na soko la ajira la Afrika Mashariki.

Amesema vijana wengi wa Zanzibar wamekuwa wakikosa ajira katika mashirika ya kimataifa kutokana na kutojua lugha, jambo ambalo linapaswa kuwekewa mikakati maalum.

“Ndugu wanafunzi, nakuombeni sana muweke mkazo katika kusoma lugha hizi za kigeni hasa Kiingereza na Kichina, lazima tukubali kuwa Kiingereza ni lugha ya kimataifa duniani lakini na ulimwengu tunaoelekea utaongozwa na wachina”, alisema Maalim Seif na kuongeza kuwa lugha zote ikiwemo kichina zinasomeka na kufahamika, sio ngumu kama mnavyofikia kwani hapa hapa Zanzibar tunao watu wanaozungumza Kichina kama wenyewe kabisa.

Katika hafla hiyo, Maalim Seif ameahidi kuchangia shilingi milioni tatu na nusu, komputa mbili za mezani na vifaa vya michezo kwa ajili ya maendeleo ya skuli hiyo.

Katika hatua nyengine Maalim Seif amewataka wananafunzi, walimu, wazazi na wadau wote wa elimu kuungana ili kuinusuru Zanzibar na kashfa ya kughushi mitihani.

Amesema ni aibu kwa Zanzibar yenye waislamu zaidi ya asilimia 98 kusubiri kughushi mitihani, jambo ambalo limekatazwa katika misingi ya dini ya kiislamu.

Amewataka wanafunzi kujiandaa kwa ajili ya mitihani yao ya kitaifa na kuachana na tabia ya kufanya ghushi, kwani kufanya hivyo ni kuliangamiza taifa ambalo baadaye litakosa wataalamu wenye sifa.

Katika risala yao iliyosomwa na Mwalimu Bi. Mwajuma Abadi, walimu wa skuli hiyo wamesema wamepata mafanikio makubwa katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, na kwamba juhudi zaidi zinafanywa ili kuleta maendeleo zaidi.

Bi Mwajuma amesema katika mahafali ya kwanza ya skuli hiyo mwaka 2010, jumla ya wanafunzi 69 walifanya mitihani ambapo karibu wote walifaulu na kuingia vyuo vikuu, na kuifanya skuli hiyo kuwa ya mwanzo kwa skuli za serikali Zanzibar.

Ameongoza kuwa mwaka 2011, wanafunzi 89 walifanya mitihani na wengi kati yao pia walifaulu kuingia vyuo vikuu ambapo kwa mwaka huo skuli hiyo ilishika nafasi ya nne kwa skuli za serikali Zanzibar

Amefahamisha kuwa tofauti hiyo ya matokeo ya miaka miwili iliyopita, kunadhihirisha changamoto ya kitaifa katika masomo ya sayansi, ikizingatiwa kuwa katika mahafali ya kwanza nay a pili, wanafunzi wote walifanya masomo ya sanaa (Art).

Viongozi mbali mbali walihududhuria katika mahafali hayo wakiwemo Waziri wa Elimu na Mafunszo ya Amali Mhe. Ali Juma Shamhuna, Waziri wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati Mhe. Ramadhan Abdallah Shaaban na Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Mhe. Abdallah Mwinyi Khamis.

Hafla hiyo ilikwenda sambamba na kukabidhi vyeti kwa wahitimu wa kidato cha sita, pamoja na kukabidhi zawadi kwa wanafunzi wa michepuo na walimu wastaafu wa skuli hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.