Habari za Punde

Serikali yaahidi kuiunga mkono TASAF



Na Asya Hassan
SERIKALI imesema itaendelea kuunga mkono utekelezaji wa mradi wa Tasaf awamu ya tatu ili kuzikwamua kaya maskini na hali ngumu ya kiuchumi inayozikabili.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd aliyasema hayo wakati akizindua mradi wa awamu ya tatu wa TASAF kwa kanda ya Zanzibar hafla iliofanyika hoteli ya Zanzibar Beach Resort Mazizini.
Alisema lengo la serikali ya Zanzibar ni kuhakikisha wananchi wake wanaondokana na  hali ngumu ya umaskini na utegemezi.
Alisema katika miaka mitano ijayo mpango huo utawafikia walengwa milioni 1.5 Tanzania Bara na Visiwani wanaoishi katika mazingira hatarishi.

Hata hivyo, alisema ili malengo hayo yafikiwe ushiriki wa wadau wote unahitajika.
Aidha alisema ni matarajio ya serikali kuwa mpango huo utaimaisha uwazi, uwajibikaji na kutoa fursa kwa makundi mbali mbali kushiriki kwa kutumia mfumo madhubuti wa kubaini walengwa katika shehia.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Ladislaus Mwamanga alisema Tasaf awamu ya tatu utabeba changamoto zote ambazo zilitokea awamu ya mwanzo na ya pili na kuzifanyia marekebisho ili zisiweze kutokea katika awamu ya tatu.
Alisema Tasaf imetenga fedha za kutosha katika kuyajengea uwezo mifumo yote ili kuweza kufikia lengo lililokusudiwa.
Nae Katibu Mkuu Ofis ya Makamu wa Pili wa Rais, Dk. Khalid Mohammed alisema TASAF awamu  pili kwa Unguja na Pemba ilitekeleza miradi 820 ambapo Unguja ilikua miradi 433 na Pemba miradi 387.
Alisema kuwa fedha zilizotumika katika miradi hiyo ni shilingi bilioni 12 ambapo bilioni 1.3 zilitolewa na wananchi wenyewe.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.