Habari za Punde

Baraza lasitishwa · Akidi yakosekana Ni baada ya wajumbe kutohudhuria

Mwashamba Juma na Mwanrafia Kombo MCC
BARAZA la Wawakilishi jana lililazimika kuahirisha kikao cha asubuhi kutokana na akidi ya wajumbe wa baraza hilo kutotimia.
Mara baada ya Spika wa Baraza hilo, Pandu Ameir Kificho, kuingia ukumbini na kukalia kiti chake akijiandaa kusoma dua ya ufunguzi, alisimama na kusema asingeweza kuendelea na kikao kutokana na akidi kutotimia na kusema anasitisha ili wajumbe wapate nafasi ya kutafutwa.

Wakati huo wajumbe waliokuwemo ukumbini ni 17 tu kati ya wajumbe wote 82 wanaounda baraza hilo.
Kwa mujibu wa kanuni za kudumu za baraza toleo la mwaka 2012, Spika anaweza kusitisha shughuli za baraza kwa dakika tano iwapo akidi haitatimia baada ya mjumbe yeyote kusimama na kumwambia Spika kwamba akidi haitatimia.

Na baada ya wajumbe kurudi ukumbini na kama bado akidi haitatimia, Spika au Mwenyekiti ana mamlaka ya kusitisha shughuli za baraza kwa dakika 30.

Hata hivyo, katika mkutano wa jana, Spika aliahirisha kwa dakika 30, lakini hata muda huo ulipofika wajumbe waliokuwepo ukumbini walikuwa  25 tu akiwemo Spika mwenyewe.

Kwa mujibu wa kifungu cha 82 kifungu kidogo cha 2 cha katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, ili akidi itimie lazima kuwe na wajumbe zaidi ya nusu ya wajumbe wote wa baraza ambapo ni wajumbe 42 kwa kuwa baraza hilo lina wajumbe 82.

Aidha kifungu cha 72 kifungu kidogo cha 2 cha kanuni za kudumu za Baraza toleo la mwaka 2012, akidi itatimia iwapo kutakuwa na wajumbe zaidi ya nusu ya wajumbe wote wa baraza.


Kikao cha jana kilisitishwa kwa sababu kazi iliyotakikana kufanyika ilihusiana na maamuzi, yanayohitaji kutimia akidi ya wajumbe.

Kikao  cha jana asubuhi kilikuwa kipitishe vifungu vya bajeti ya Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na Nishati ambayo ililazimika kupitishwa jioni na jioni walikuwa wapitishe bajeti ya Wizara ya Fedha.

Aidha kwa mujibu wa kanuni za baraza kifungu cha 74 (2), mjumbe anaweza kupewa adhabu ya kukatwa posho la siku iwapo hakuhudhuria kikao cha siku cha baraza bila ya ruhusa ya Spika au Mwenyekiti na atakuwa amejifukuza barazani kama hatahudhuria mikutano mitatu bila sababu zinazotambuliwa na Spika au Mwenyekiti.


Na iwapo alilipwa posho kabla, atakatwa posho hilo kwenye stahiki zake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.