Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                8.2.2016
---
RAIS wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amesema kuwa licha ya mafanikio yaliopatikana katika sekta ya kiuchumi, kijamii na kisiasa kwa lengo la kuimarisha maendeleo ya ustawi wa wanawake bado jitihada za pamoja zinahitajika katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili wanawake hao.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatambua mchango wa wanawake katika kuijenga Zanzibar kabla na baada ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 na ndio maana katika kuadhimisha miaka 50 ya Mapinduzi hayo miongoni mwa waliotunukiwa nishani walikuwa ni wanawake ambao wamefanya mambo makubwa ya kukumbukwa katika historia ya maendeleo ya Zanzibar.

Aliyasema hayo katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Mhe. Bi Hindi Hamad Khamis katika madhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliofanyika katika ukumbi wa Salama, Hoteli ya Bwawani Zanzibar yalioenda sambamba na Usiku wa Taasisi ya Bibi Siti Binti Saad.

Katika hotuba yake hiyo Dk. Shein alisema kuwa mashirikiano ya pamoja yanahitajika katika mapambano dhidi ya unyanyasaji wa kijinsia, maradhi thakili yanayowasibu wanawake, kuongeza jitihada katika kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi, kupunguza mimba za utotoni pamoja na kuimarisha upatikanaji wa fursa na haki mbali mbali.

Dk. Shein alisema kuwa hatua ya maendeleo iliyofikiwa hivi sasa ni matokeo ya jitihada kubwa zinazofanyika kwa pamoja, bila ya kujali jinsia, kupanga na kutekeleza mambo mbali mbali huku akitumia fursa hiyo kuipongeza Taasisi ya Siti Binti Saad kuona umuhimu na mchango wa wanawake katika jamii na kuamua kuwapa tunzo katika hafla hiyo.

“Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, inatambua kuwa itakuwa bora zaidi katika kupanga na kutekeleza mipango yetu ya maendeleo ikiwa kila mwananchi atapewa fursa na haki sawa ya kushiriki katika kupanga na kutekeleza mipango hiyo ya maendeleo”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa katika kipaindi cha miaka mitano iliyopita, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetekeleza mambo mbali mbali katika sekta za kiuchumi na kijamii kwa lengo la kuimarisha maendeleo na ustawi wa wanawake pamoja na watoto.

Dk. Shein alisema kuwa katika  jitihada za kuwawezesha wanawake kiuchumi, Serikali imeziimarisha fursa za upatikanaji wa mikopo kwa wanawake kupitia mifuko mbalimbali ya uwezeshaji iliyokuwepo kabla na iliyoanzishwa hivi karibuni.

Kadhalika Dk. Shein alisema kuwa usawa wa kijinsia katika uteuzi na uchaguzi wa nafasi katika ngazi mbali mbali unazingatiwa  na kueleza kuwa hadi kufikia tarehe 13 Agosti mwaka jana alipolivunja Baraza la Wawakilishi lilikuwa na wajumbe 81 kati ya hao wajumbe wanawake walikuwa ni 27 sawa na asilimia 33 kiwango ambacho hakijafikiwa na nchi nyingi duniani.

Akieleza mafanikio mengine ya wanawake Dk. Shein alieleza kufurahishwa kwake kuona kwa mara ya kwanza, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepata Makamu wa Rais mwanamke Mhe. Samia Suluhu Hassan ambapo pia, wagombea wawili kati ya watatu waliopitishwa na Mkutano Mkuu wa CCM kugombea nafasi ya Urais kwa tiketi ya CCM walikuwa wanawake.

Kwa upande wa sekta ya elimu, Dk. Shein alisema kuwa Serikali imeimarisha fursa za elimu ya juu kwa wanawake sambamba na kuimarisha utoaji wa mafunzo katika Skuli ya Sekondari ya Wawanwake, BenBella na Utaani, ambazo zimeimarishwa zikiwa na lengo la kuwasaidia wanafunzi wa kike waweze kufaulu kwa wingi na kuweza kujiunga katika vyuo vikuu vya ndani na nje ya nchi.

Dk. Shein akieleza kuhusu sekta ya afya, alisema kuwa kwa upande sekta hiyo, Serikali imeimarisha huduma za wanwake na watoto katika vituo vya afya na katika hospitali zote za Zanzibar huku akitilia mkazo agizo alilolitoa mwezi Mei 2012 kwamba wanwake wote wanaojifungulia hospitalini wapatiwe huduma za uzazi bila ya malipo yoyote.

Katika jitihada za kupambana na udhalilishaji na ukatili dhidi ya wanawake na watoto, Dk. Shein alisema kuwa Serikali ilianzisha Kampeni dhidi ya unyanyasaji wa kijinsia tarehe 6, Disemba, mwaka 2014, kampeni ambayo imesaidia sana katika kutoa mwamko wa kupambana na vitendo vya udhalilishaji wa wanawake na watoto.

Nao uongozi wa Taasisi ya Bibi Siti Binti Saad ukiongozwa na Mwenyekiti wake Bi Nasra Mohammed Hilal ulieleza mafanikio ya Taasisi hiyo sambamba na kueleza kujuhudi zilizochukuliwa na akina mama katika kuiletea maendeleo Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla.

Hafla hiyo ya kuadhimisha siku ya wanwake duniani iliyoenda sambamba na usiku wa Taasisi ya Bibi Siti Binti Saad tumbuzo mbali mbali zilitumbuiza katika usiku huo ikiwa ni pamoja na ngoma za  asili ikiwemo ngoma ya Rubamba na taarab ya kikundi cha  Raahat Zamaan.

Katika kikundi cha taarab cha Raahat Zamaan ambacho kiliupamba usiku huo, kirembwe cha Bibi Siti Binti Saad akiwa na wasanii wenziwe waliburudisha na kuwakumbusha nyimbo za mkongwe huyo ambazo zilitia fora wakati wa uhai wake hadi hii leo bado zinaendelea kungara.

Sambamba na hayo, akina mama mbali mbali walikabidhiwa zawadi kutokana na ushiriki wao katika kuiletea maendeleo Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla, zawadi zilizotolewa na Taasisi hiyo akiwemo Mama Fatma Karume, Bibi Siti Binti Saad, Bibi Johari Yussuf Akida, Bi Mtumwa Fikirini, Mhe. Samia Suluhu Hassan, Mhe. Asha Rose Migiro, Mhe. Anna Makinda, Mhe.Khadija Aboud, Zainab Himid, Bi Fatma Aloo, Bi Rufea Juma Mbarouk, Mhe. Amina Salum Ali, Bi Jogha Mohammed, Tatu Ali na wengineo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.