MKE wa Rais wa Zanzibar
Mama Mwanamwema Shein amewataka akinama na viongozi wa Umoja wa Wanawake
Tanzania (UWT) kutembea kifua mbele kwa lengo la kuyatangaza mafanikio
yaliopatikana hapa nchini hasa katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM
ya mwaka 2015-2020.
Mama Shein aliyasema
hayo leo huko katika ukumbi wa Ofisi za CCM Mkoa wa Amani Kichama zilizopo mjini Unguja, wakati akizungumza na
akinamama, viongozi na wanachama wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT) wa Mkoa
wa Mjini Kichama kwa lengo la kuwasalimia na kuwashukuru kwa kuendelea kuiunga
mkono CCM, na hatimae kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi uliopita.
Katika hotuba yake,
Mama Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imefanya mambo mengi
ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wake ambapo miongoni mwa hayo ni suala zima
la elimu bila ya malipo, utoaji wa pencheni jamii kwa wazee kuanzia miaka 70 na
kuendelea, kuondosha malipo kwa akinamama wanaojifungua katika hospitali za
Serikali.
Mengine ni pamoja na
kulipia ada ya mitihani wanafunzi wa Sekondari pamoja na uimarishaji wa huduma
ya afya ya Mama na Mtoto ambapo Dk.
Shein hivi karibuni aliyafungua majengo mapya huko katika hospitali ya Mnazi Mmoja
ambayo yamesheheni vifaa vya kisasa na lengo likiwa ni kutoa huduma bora za
afya.
Kwa mnasaba huo, Mama
Shein pamoja na ujumbe wake aliofuatana nao wakiwemo wake wa viongozi na
Wabunge na Wawakilishi walitoa pongezi zao za dhati kwa Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk, Ali Mohamed Shein, Makamu wa Pili wa Rais,
Balozi Seif Ali Idd, Mawaziri, viongozi wa Chama na Serikali pamoja na
watendaji wote kwa kutekeleza mipango na shughuli zilizomo katika Ilani ya CCM.
Aidha, Mama Shein
alieleza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika
kutekeleza miradi ya maendeleo na kueleza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na
Serikali katika kulitafutia ufumbuzi tatizo la upungufu wa maji safi na salama
katika maeneo ya mjini.
Hivyo, Mama Shein
alitoa wito kwa viongozi na wananchi kuendelea kuwa na subira na kushirikiana na serikali yao katika
kufanikisha mipango ya maendeleo.
Mama Shein, ambaye
katika ziara yake hiyo amefuatana na viongozi mbali mbali wakiwemo Wabunge na
Wawakilishi wa Viti maalum pamoja na wake wa Wabunge na Wawakilishi, alitumia
fursa hiyo kusisitiza suala zima la amani
Pia, Mama Shein alitoa
nasaha zake kwa viongozi, akinamama na wanajumuiya ya UWT na kuwataka kushirikiana
na vyombo vinavyohusika kuwaripoti watu
wanaobaimika kufanya vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia.
Wakati huo huo, Mama Shein
aliwakabidhi kadi za Jumuiya ya UWT wanachama wapya 42 waliojiunga na Jumuiya
hiyo.
Mapema Mama Asha
Balozi, Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwataka viongozi wa UWT
kupenda kukosolewa na kuwataka kuzidisha mashirikiano na kusikiliza mawazo ya
watu waliochini yao kwani huo ndio uongozi. Aidha, Mama Asha, alipingana na
wale wote wanaosema kuwa hakuna maendeleo.
Pamoja na hayo, Mama
Asha aliwataka akinamama hao kujipanga vizuri katika suala zima la kuwalea
watoto wao sambamba na kutambua nyendo zao hasa nyakati za usiku huku akiwasisitiza
haja ya kuzidisha mapenzi miongoni mwao.
Nae, Mama Fatma Karume
alitumia fursa hiyo kutoa historia ya kudai uhuru wa Zanzibar na jinsi wanawake
walivyoshiriki katika mapambano hayo.
Aidha, Mama Fatma
Karume aliishauri Serikali kuwawekea
watoto wadogo muda maalum wa kutembea nyakati za usiku kutokana na kuepuka
vitendo viovu ambavyo wanaweza kufanyiwa.
Katika risala yao UWT
Mkoa wa Mjini, walimpongeza Dk. Shein kwa kuwateua akinamama wengi katika
Serikali anayoiongoza na kutoa shukurani kwa wanajumuiya ya UWT Mkoa wa Mjini
kwa kujitokeza kwa wingi katika uchaguzi Mkuu wa marudio.
Akinamama hao,
walimpongeza Dk. Shein kwa kutia saini hadharani Mswada wa Sheria ya utafiti na
uchimbaji wa Mafuta na Gesi Zanzibar, na kumpongeza kwa kitendo chake hicho cha
kishujaa huku wakisisitiza haja ya kuendeleza ushirikiano ndani ya chama chao
ili kizidi kuleta mafanikio zaidi. Aidha, viongozi hao walijinasibu kwa mashirikiano
na maendeleo waliyonayo.
Mama Shein alianza
ziara hizo za shukrani katika Mikoa ya Pemba mnamo Novemba 5 hadi 8 mwaka huu na
kuendelea katika Mikoa ya Unguja kuanzia Novemba 21 na kumalizia hii leo.
No comments:
Post a Comment