Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Atembelea Maeneo Yaliopata Maafa na Kuwafariji Wananchi Kisiwani Pemba.


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                        15.05.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewatembelea na kuwapa pole wananchi wa maeneo mbali mbali kisiwani Pemba kufuatia maafa yaliotokana na mvua za masika zinazoendelea kunyesha ambazo zimeathiri baadhi ya makaazi ya wananchi, mazao  pamoja na miundomninu ya barabara na madaraja kisiwani humo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika ziara yake aliyoifanya katika maeneo mbali mbali Kisiwani Pemba ambayo yameathirika na mvua hizo za masika zinazoendelea  kunyesha na kutumia fursa hiyo kuwafariji wananchi hao pamoja na kuwapongeza kwa moyo mkubwa waliouonesha wa kusaidiana na kustiriana katika kipindi hicho kigumu.

Miongoni  mwa maeneo aliyoyatembelea Dk. Shein katika ziara yake hiyo ni Mchanga wa Kwale, Chamanangwe, Bugujiko, kuungoni, Gando na Pujini kwa upande wa Mkoa wa Kaskazini Pemba na Mgagadu Kiwani, Chonga, Kipapo, Changaweni Mkoani, Ghala la karafuu la ZSTC Mkoani pamoja na Makombeni kwa upande wa Mkoa wa Kusini Pemba.

Katika ziara yake Dk. Shein alieleza kusikitishwa na kuhuzunishwa na athari hizo zilizotokea lakini hata hivyo alitoa pongezi zake kwa wananchi kwa mashirikiano waliyoyaonesha katika kipindi hicho, uongozi wa Mkoa na Wilaya zote za Pemba, uongozi na wafanyakazi wa Wizara ya Ujenzi , Mawasiliano na Usafirishaji   pamoja na vikosi vya SMZ vilivyosaidia katika juhudi za kupambana na athari hizo.

Dk. Shein katika ziara yake hiyo aliwaeleza wananchi kuwa Serikali yao ya Mapinduzi ya Zanzibar iko pakoja na wao na itaendelea kuwapa kila msaada unaohitajika na kuwataka kuendelea kwua na uvumilivu na subira na kutomlaumu mtu ama kuhamaki kwa tukio hilo ambalo ni shani ya Mwenyezi Mungu.

Dk. Shein alipata fursa ya kuiona familia ambayo nyumba yao iliangukiwa na mbuyu ambayo ndani mlikuwa na familia ya watu wanane wakati wa usiku lakini wote walikuwa salama huko katika maeneo ya   Gando Kilimajuu  na kuifariji na kuahidi kuwa Serikali itatoa msaada wake mkubwa ikiwa ni pamoja na kuijenga nyumba hiyo ambapo familia iyo ilimpongeza Dk. Shein kwa hatua yake ya kwenda kuwaona.

Akiwa katika eneo la Bugujiko akizungumza na wananchi waliathirika baada ya nyumba zao kuingia maji katika eneo hilo Dk. Shein alisema kuwa tatizo hilo linamnasaba na mvua hivyo aliwaahidi wananchi kuwa Serikali itajenga msingi wa maji katika eneo hilo ili kuondosha kabisa athari kama hizo wakati wa mvua kwani uwezo huo upo.

Aidha, Dk. Shein akiwa Kipapo kwenye barabara ya Kipapo Mgelema ambapo miundombinu ya barabara na daraja imeathirika, Dk. Shein aliwaeleza wananchi wa eneo hilo kuwa azma ya Serikali ya kuijenga barabara hiyo pamoja na barabara nyengine alizoahidi ambazo hutoa mazao kwa wingi likiwemo zao la karafuu, azma hiyo ipo na barabara hizo zitaendelea kujengwa kwa kiwango cha lami pamoja na madaraja yake yote ili kuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Aliwapa pole wananchi wa eneo hilo na kuwathibitishia kuwa Serikali ipo pamoja nao huku akiwakubalia ombi lao la kujengewa skuli ya chekechea na kuuagiza uongozi wa Mkoa wa Kusini Pemba kushirikiana na Wizara ya Elimu na Mfunzo ya Amali ili kwenda kuliona eneo walilolitayarisha wananchi hao kwa ajili ya ujenzi huo na kama litaruhusu basi Serikali itajenga hadi skuli ya msingi.

“Hakuna dhiki wa dhiki bali baada ya dhiki ni faraja…basi wananchi endeleeni na subira”,alisema Dk. Shein.

Akiwa katika ghala la karafuu la ZSTC Mkoani, Dk. Shein alipata maelezo ya athari zilizotokea kutoka kwa Afisa Mdhamini wa Shirika hilo Abdalla Ali Ussi ambaye alisema kuwa kabla ya athari hizo ghala hilo lilikwua na karafuu kavu gunia 527 sawa na tani 23.7 kwa thamani ya TZS milioni 332.0 ambapo kwa bahati nzuri karafuu kavu gunia 518 sawa na tani 23.3 kwa TZS milioni 326.4 zilipatikana bila ya athari yoyote.

Afisa Mdhamini huyo aliongeza kuwa magunia 9 ya karafuu kavu yenye uzito wa kilo 405 sawa na TZS milioni 5.6  zimeathirika na kueleza kuwa ujenzi waa eneo hilo liloloharibika kutokana na maji mengi yaliotokea barabarani na kusababisha maporomoko na dongo na kusabiisha kugoka kwa mti mkubwa ulioelemea ukuta wa ghala na kuuangusha na maji na matope pamoja na kti kuingia ghalani humo.

Dk. Shein alipongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa katika kurejesha hali yake ghala hilo pamoja na juhudi za ziada zilizofanywa katika kuziokoa karafuu zilizokuwemo ghalani humo.

Katika maelezo yake, Dk. Shein huko Makombeni, aliwapa pole wananchi wa eneo hilo kutokana na athari za nyumba zao zilizoathirika katika Wilaya hiyo zipatazo 540, ambapo Shehia 30 kati ya 34 zimeathirika na mvua hizo na kuwaeleza kuwa Serikali iko pamoja na wao katika tukio hilo na kuwapongeza kwa uvumilivu na umoja wao waliouonesha wakati wa maafa hayo.

Nao uongozi wa Wizara ya Ujenzi pamoja na wataalamu wake walimueleza Dk. Shein hatua zilizochukuliwa katika kuhakikisha barabara zote kisiwani Pemba zinapitika kama ilivyo hivi sasa kwa hatua za awali huku juhudi zaidi zikiendelea kuchukuliwa.

Nao wananchi wa maeneo mbali mbali ambayo Dk. Shein alipita kwa kuwapa pole na kuwafariji sambamba na kuwapongeza kwa umoja na mshikamano wao waliouonesha wakati wa maafa hayo, walimpongeza kwa kwenda kuwaona.

Wananchi hao walimpongeza Dk. Shein kwa kufanya ziara yake hiyo kwa makusudi kwenda kuwaona na kueleza jinsi walivyofurahi na kufarajika kwa kuona kumbe Rais wao yupo pamoja na wananchi wake kwa wakati wote.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar


Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.