Habari za Punde

Tume ya Uchaguzi NEC Imemteua Ndg.Catherine Nyakao Ruge Ateuliwa Kuwa Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA.



Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imemteua Ndugu Catherine Nyakao Ruge kuwa Mbunge wa Viti Maalum katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Mhe. Dkt. Elly Marko Macha aliyefariki dunia Machi 31 mwaka huu.

Akitoa taarifa ya uteuzi wa mbunge huyo Mkurugenzi wa Uchaguzi Bw. Kailima Ramadhani amesema kuwa uteuzi wake umefanyika katika kikao cha Tume kilichofanyika leo (Me 4, 2017) jijini Dar es salaam  kwa mujibu wa Ibara ya 78 (4) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ikisomwa pamoja na kifungu cha 86 A (8) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi Sura ya 343, Tume ya Taifa ya Uchaguzi.


Amesema Tume imemteua Ndugu Catherine Nyakao Ruge baada ya kupokea taarifa kutoka kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye kwa mujibu wa kifungu cha 37(3) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura 343 aliitarifu Tume juu kuwepo kwa nafasi wazi ya Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Dkt. Elly Marko Macha.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.