Habari za Punde

Sheria ijayo wataka Mufti aongezewe hadhi ya kipekee


NA HAJI NASSOR, PEMBA

MASHEIKH, wanaharakati wa mambo ya kiislamu, waalimu wa madrassa na waislamu wilaya ya Wete kisiwani Pemba, wamependekeza kuwe lazima sheria mpya ijayo ya Mufti, impe hadhi ya kipekee, ili aweze kufanya shughuli zake kwa ufanisi.

Walisema kama zilivyo sheria nyengine zilivyowapa hadhi baadhi ya viongozi, hivyo ni vyema ndani ya sheria hiyo, kiwemo kifungu kinachoonyesha Mufti wa Zanzibar anakuwa na hadhi, kama wanavyoshuhudia wa nchi nyengine.

Wakitoa maoni yao juu ya mswada wa sheria ya Mufti mjini Wete mbele ya wajumbe wa Tume ya Kurekebisha waliofika wilayani humo, kukusanya maoni, walisema wakati umefika kwa Mufti nae kuwa na hadhi ya kipekee.

Sheikh Khamis Rashid Suwedi, Imamu wa msikiti wa Ijumaa wa Hanafi, alisema hadhi ambayo wanaitaka kwa Mufti iwe zaidi ya waziri, katibu mkuu au wakurugenzi.

“Kuanzisha sheria kwa ajili Mufti na ofisi yake, ni jambo jema, maana kwa sasa anaonekana kama mtu wa kawaida anapokuwa kwenye misafara yake, jambo ambalo sio sahihi”,alisema.

Nae mwalimu Abeid Seif, alisema baada ya kuwepo kwa kifungu hicho ndani ya sheria hiyo ijayo, lazima kuwe na utekelezaji wake, maana zipo sheria kadhaa nzuri lakini ubora wake hauonekani.

Nae Naibu Katibu wa Jumuia ya Maimu wilaya ya Wete Rashid Khamis Hamad, alisema wasimamizi wa sheria hiyo baada ya kupita, lazima waache ubabaishaji katika kuitekeleza kwake, maana ni tafsiri ya Kur-an na hadithi.

“Kwa Mufti ni kiongozi wa dini ya kiislamu hivyo, hata mambo atakayoyaongoza ni yale ya kiislamu, na hata sheria yake inatokana na kitabu kitakatifu, hivyo lazima kusiwe na ubabaishaji katika hili”,alieleza.

Wakichangia mswada wa sheria ya ndoa na talaka, viongozi hao wa dini walisema, kama ikipita inawez kuondoa mkanganyiko wa tafsiri wa mambo mbali mbali kama mfano wa talaka zilizotokewa tatu kwa wakati mmoja.

Mjumbe kutoka Jumuia ya Maendeleo ya Kiislamu, sheikh Haji Mkubwa Ahmed , alisema wapo masheikh na makadhi wamekuwa na uamuzi unaotofautiana juu ya tamko la talaka zilizotolewa zaidi ya tatu.

“Naamini ujio wa sheria hii, sasa waislamu wanaolalamikiana juu ya matamko ya maandishi ya talaka zilizotolewa 10, sita au tatu na hata mbili kwa wakati mmoja, sasa sheria itaoongoza”,alisema.

Mapema mwanasheria kutoka Tume hiyo Mohamed Ahmed, alisema sheria inayokuja ya ndoa na talaka, itakuwa ya kipee kwa nchi za Afrika Mashariki.

Alisema nchi zote hizo hadi sasa, hazina sheria ya aina hiyo, hivyo anaamini itakapomalizika wanaweza kufika Zanzibar kuiga mfano kwa ajili ya nchi zao.


Tume ya Kurekebisha Sheria Zanzibar chini ya Mwenyekiti wake Jaji Mshibe Ali Bakari na Katibu wake Asma Jidawi, imeshakamilisha ziara yake ya siku nne kisiwanin Pemba, ambapo ilikusanya maoni, juu ya miswada mitatu ya sheria za Mufti, ndoa na talaka na kuifanyia mapitio sheria ya asasi za kiraia no 6 mwkaa 1995.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.