Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein, Afungua Mkutano Mkuu wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja.

MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekitiwa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kwamba CCM ina uzoefu mkubwa wa kufanya mageuzi ya kifikra, itikadi, Sera na mabadiliko mengine ya kimaendeleo kwa kufuata matakwa ya wananchi bila ya kuathiri misingi imara iliyowachwa na waasisi wa Taifa hili.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika Mkutano Mkuu wa CCM wa Mkoa wa Kusini Unguja ulioenda sambamba na uchaguzi wa viongozi wa Mkoa huo Kichama, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Coconut, Marumbi, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja ambapo Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muunago wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan alihudhuria.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa CCM si chama cha mtu mmoja kama ilivyo vyama vyengine vya siasa vinavyoendelea kupoteza muelekeo na kusambaratika hivi sasa kwa kukosa uzoefu wa historia kama ilivyo kwa CCM.

Dk. Shein ambaye Mkoa huo ndio Mkoa wake Kichama aliongeza kuwa ni vyema kwa wajumbe wa mkutano huo wakatambua hivyo na wakahakikisha kwamba viongozi watakaowachagua wanaielewa itikadi ya chama hicho na sera zake na wapo tayari kuzilinda, kuzisimamia na kuzitekeleza kwa vitendo.

Alisisitiza kuwa viongozi watakaochaguliwa katika mkutano huo ambao wamepelekwa na CCM watalazimika kuwa tayari kuwakemea na kupambana na wazembe, wababaishaji, wabinafsi na wale wote wenye tabia ya kufanya kazi kwa mazoea.

Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar aliwataka viongozi watakaochaguliwa hawanabudi wawe makini, kama ilivyokawaidida kwa viongozi wa CCM ambapo umakini wao katika uchaguzi wa viongozi pamoja na kukemea maovu ndio unaokipa chama hicho nguvu zaidi za kukubalika, kuchaguka na kupendwa na wananchi wote wanaopenda amani na maendeleo nchini.

“Chama chetu kinapendwa kina wavutia wananchi na kina uwezo mkubwa na wa peke yake wa kurejesha na kujenga matumaini mapya kwa wananchama wake na wananchi wete hivyo, hapana shaka tuna nafasi nzuri ya kuendelea kushika dola kwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa dahari na zama nyingi zijazo”,alisisitiza Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa ushindi wa kishindo ambao CCM umeipata katika uchaguzi Mdogo wa Madiwani uliofanyika wiki iliyopita tarehe 26 Novemba, 2017 katika Kata 43 zilizoko katika Mikoa 19 ya Tanzania Bara ni ithibati ya kwamba CCM ilipitisha viongozi wenye sifa, uwezo, nia njema na waliokubalika kwa wananchi katika kugombea nafasi hizo.

Alisema kuwa ushindi mkubwa uliopatikana hata katika maeneo ambayo wapinzani walidhani kwamba ni ngome zao ni uthibitisho wa kuwa wananchi wanaendelea kukiamini na kukipenda chama hicho na kwamba maendeleo ya dhati ya nchi yamo ndani ya CCM.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliupongeza Mkoa huo kwa kuendelea kutekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2015-2020 ambapo tayari wameaza kutekeleza vyema kwa kipindi cha mwaka mmoja kuanzia Januari hadi Disemba 2016 kwa kushirkiana na Serikali ambapo mafanikio yamepatikana katika sekta za kiuchumi na kijamii.

Aliwahakikishia wananchi wa Mkoa huo kuwa Serikali anayoiongoza itafuata maelekezo ya Ilani hiyo ya CCM katika kuwafikishia huduma bora za jamii huku akitumia fursa hiyo kuipongeza  Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira pamoja na taasisi zake za ZECO na ZAWA kwa kutekeleza agizo lake alilolitoa katika ziara yake la kuhakikisha wananachi wa Makunduchi na Kibuteni wanapata maji kutoka katika kisima cha Mwambiji.

Aliongeza kuwa hivi leo tayari maeneo ya Kibuteni na Makunduchi yameshapata huduma za maji zinazotokana na kisima cha Mwambiji ambapo tangi lenye uwezo wa lita laki tatu limeleta ufanisi kwa wananchi kupata maji kwa kutwa nzima bila ya usumbufu badala ya saa sita tu kama ilivyokuwa hapo mwanzo na kueleza kuwa mapema mwezi ujao maji yatapatikana kwa uhakika zaidi katika maeneo hayo.

Pia, Dk. Shein alieleza kuwa katika kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa upande wa Michamvi, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Ras al Khaiman imechima kisima maalum katika eneo la Ghana, Bwejuu kwa ajili ya kupeleka maji safi na salama katika kijiji hicho.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwasihi viongozi wote ambao kura zao hazitotosha, wasivinjike moyo na watambue kuwa mwisho wa uchaguzi mshindi mkubwa ni CCM huku akiwanasihi viongozi watakaochaguliwa kusimamia nyadhifa na majukumu watakayokabidhiwa vizuri, ili Mkoa huo uendeleze historia yake ya kuwa ni tishio kwa wapinzani.

Nae Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan ambaye pia, ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, alitoa salamu za Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama hicho Dk. Johm Pombe Magufuli na kusisitiza haja kwa wajumbe wa Mkutano huo kuwachagua viongozi watakaokiimarisha zaidi chama hicho ili kiendelee kupata ushindi katika chaguzi zake zote zijazo.

Mapema Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Juma Abdalla Mabodi alitoa salamu za chama na kueleza mchakato wa uchaguzi ulivyooanza tokea Shina na kueleza kuwa chama kimekuwa imara na viongozi waliochaguliwa na watakaochaguliwa katika Mkutano huo ni weliedi na watakipeleka chama hicho katika ushindi mkubwa wa  uchaguzi wa mwaka 2020 na kusisitiza kuwa chama hicho hakitokuwa na chuwa  huku akiwapongeza viongozi wa CCM wa Mkoa huo waliopita kwa kukipa ushindi mkubwa chama hicho katika chaguzi zote zilizopita.

Nao viongozi wa CCM Mkoa huo wa Kusini walitumia fursa hiyo kumpongeza Dk. Shein kwa juhudi zake kuwa aanazozichukua katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar na kumpa pongezi maalum kwa kuongeza mishahara kwa wafanyakazi wa sekta ya umma  sambamba na kuwapa wazee waliofikia umri wa miaka 70  pencheni jamii ambayo imeipa sifa kubwa Zanzibar.

Pia, viongozi hao walimpongeza Dk. Shein kwa juhudi maalum alizozichukua kutokana na agizo lake alilolitoa katika ziara yake aliyoifanya katika Mkoa wa Kusini mwezi Agosti mwaka huu la kuitaka Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja wananchi wa Mitakawani wanapata kaji safi na salama jambo ambalo limefanikiwa  na wananchi hao wanapata huduma hiyo.

Wakati huo huo, Dk. Shein pamoja na Mama Samia Suluhu Hassan ambao wote ni wajumbe wa Mkutano huo, uliosimamiwa na Professa Makame Mbarawa ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walitumia fursa hiyo kuwapigia kura viongozi wa Chama wa Mkoa  huo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.