Habari za Punde

Ufungaji wa Kampeni za Uwakilishi CCM Jimbo la Jang'ombe Zanzibar Viwanja Vya Muembematarumbeta Zanzibar ng'


MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amesema kuwa kinachotakiwa siku ya Oktoba 27, 2018 katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Jang’ombe ni kuhakikisha heshima ya CCM inaendelea kuwepo katika Jimbo hilo kwani lina historia kubwa.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika uwanja wa Muembe Matarumbeta, Jimbo la Jang’ombe, Wilaya ya Magharibi Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja katika mkutano wa kufunga Kampeni za Jimbo hilo ambazo zilianza Oktoba 14, 2018 na uchaguzi wake unatarajiwa kufanyika Jumaamosi Oktoba 27 mwaka huu.

Alisema kuwa ushindi wa CCM itaendeleza heshima na historia ya Jimbo hilo kwani  Marehemu Mzee Abeid Amani Karume alisisimama kuwa mgombea wa wa Chama cha ASP mnamo mwaka Januari 1961 ambapo alipata kura 3028 na kuwashinda viongozi wawili walioungana kwa pamoja kutoka kambi ya upinzani wapinzani waliopata kura 216 TU.

Akitoa historia hiyo Rais Dk. Shein alisema kuwa katika uchaguzi uliofuata Mzee Karume pia, aliendelea kushinda na kupata kura zipatazo 5701 katika uchaguzi wa  mwezi Juni na kuwataka wananchi kuyafanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa na viongozi wao katika mikutano ya kampeni za Jimbo hilo.

Katika maelezo yake Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar, alieleza kuwa Jimbo la Jang’ombe ni lazima lirudi mikononi mwa CCM kwani lina historia kubwa ndani ya chama hicho.  

Alisema kuwa Ramadhani Hamza Chande hakupendelewa na ameteuliwa kwa sifa, uwezo na heshima pamoja na uwanachama wake wa CCM na uzalendo wake mkubwa alionao pamoja na imani ya nchi yake na Jimbo lake.

Dk. Shein alisema kuwa  huo ni uchaguzi mdogo, lakini hakuna uchaguzi mdogo uliokuwa haufanyiwi kampeni wala wanachama wake hawahangaiki hivyo, ni lazima wanaCCM wa Jimbo hilo wahakikishe wanakipigania chama chao na wanakipa ushindi.

Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alimpongeza Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Dk. John Pombe Magufuli kwa kuendesha kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho kilichofanya uwamuzi wa kumteua Ramadhan Chande kwani ni uwamuzi sahihi wa kuwaletea ushindi wanaCCM wa Jimbo la Jang’ombe.

Dk. Shein alimpongeza Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara Philip Mangula kwa kuja kuzindua Kampeni hizo hapa Zanzibar mnamo tarehe 14 mwezi huu ambapo leo zimefungwa rasmi na kuwataka wananchi na wanaCCM kumchangua mgombea huyo na kuwapongeza viongozi wote waliokuwa wageni rasmi katika mikutano kadhaa iliyopangwa.

Licha ya mvua zilizokuwa zikinyesha katika eneo la mkutano huo, wanaCCM na wananchi walijitokeza kwa wingi na kumsikiliza Rais Dk. Shein ambaye na yeye kwa upande wake aliwapongeza wanaCCM wa Jimbo la Jang’ombe kwa kuhudhuria kwa wingi katika mikutano yote ya chama hicho tokea kuanza mikutani ya Kampeni na kuwataka kutofanya kosa na badala yake wamchangue Ramadhan Hamza Chande .

Rais Dk. Shein alisema kuwa katika uchaguzi huo mdogo hakuna Ilani mpya ya CCM ila kuna mgombea mpya wa Jimbo la Jang’ombe ambaye atatekeleza Ilani hiyo na kusisitiza kuwa Serikali imetekeleza Ilani hiyo ndani ya miaka mitatu kwa mafanikio makubwa sana ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta za jamii,kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta ya afya, maji, elimu, uzalishaji na nyenginezo.

“Na wapo wanaosema hatujafanya kitu, nawambia yaguju” Dk. Shein alisema kuwa mafanikio makubwa yamepatikana katika kuipatia Zanzibar maendeleo ikiwa ni pamoja na Utiaji Saini Mkataba wa Mgawanyo wa Uzalishaji wa Mafuta na Gesi Asilia, hafla iliyofanyika hivi karibuni katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar.

Kutokana na hatua hiyo iliyofikiwa na Zanzibar, Rais Dk. Shein aliwataka wananchi wote wa Zanzibar kutulia kwani mambo mazuri zaidi yanakuja na wale wote waliosema hayawi wasiwajibu wawatazame watayaona na watayaacha wenyewe.

Alisema kuwa pamoja na mafaikio yaliopatikana katika Majimbo ya Unguja na Pemba ndani ya Majimbo yote hayo 54 pamoja na Jimbo la Jang’ombe bado zipo changamoto ambazo Serikali inaendelea kuzitafutia ufumbuzi wa haraka.

Alisema kuwa wapo watu wanaoshutumu kuwa skuli ya Kidongochekundu ambayo imejengwa mwaka 1956 imetupwa jambo ambalo sio la kweli na kueleza kuwa skuli hiyo kamwe haiwezi kutupwa na badala yake itatengenezwa na kuwa ya kisasa kwani fedha zipo.

Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayafanya juhudi katika kuhakikisha inawafikisha huduma za maji katika Majimbo ya mji wa Zanzibar likiwemo Jimbo la Jang’ombe kwa gharama ya Dola milioni 21 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) ili kuhakikisha tatizo la maji linaondoka kabisa.

Alieleza kuwa tayari mchakato wa kusambaza mabomba kutoka visima vikubwa 9 vilivyopo Bumbwisudi unaendelea ambapo tayari mabomba yameashaanza kuwekwa na Kampuni kutoka China na si muda mrefu mradi huo utakamilika.

Alisema kuwa hakuna mda mrefu mambo hayo yatakamilika na kueeleza kuwa katika suala zima la ujenzi wa barabara za ndani zikiwemo za Jimbo la Jang’ombe zitajengwa kwani kutojengwa kwake kumetokana na uhaba wa vifaa vya kutengenezea barabara ambavyo hivi karibuni vitawasili.

Dk. Shein aliwaahidi wananchi wa Jangombe kuwa barabara zao za ndani zitajengwa na kwa kiwango cha lami na kueleza kuwa kama ahadi aliyoiahidi ya ujenzi wa mtaro mkubwa kwa ajili ya kutoa maji  machafu aliyoiahidi wakati akigombea urais alivyoitekeleza na hilo halina mjadala.

Akieleza hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha inanunua vikalio, tayari vikalio vipatavyo 44,000 vishanunuliwa kutoka China ambavyo vitawasili hivi karibuni na vitasambazwa katika skuli zote za Unguja na Pemba ikiwemo skuli ya Kidongochekundu na Jangombe.

Makamo huyo wa Mwenyekiti wa CCM Zanzibar alisema kuwa Hospitali ya jumba la vigae imeshakarabatiwa na wagonjwa wa akili ya Kidongochekundu inafanyiwa matengenezo makubwa huku  hatua za Serikali za kujenga hospitali mpya ya kisasa huko Binguni zikiendelea ambayo itasaidia katika kutoa huduma mbalimbali.

Alisema kuwa CCM haina papara wala pupa kwani siasa inaijua na chama hicho kimekuwa kikiimarika kila siku na kusema kuwa hakuna jambo ambalo limeahidiwa na hivi sasa haitekelezwi.

Alisema kuwa Jang’ombe ina heshima kubwa sana ni Jimbo la historia na viongozi wengiwa Zanzibar wametoka katika Jimbo la Jangombe “Jangombe ina wenyewe na wenyewe ni CCM, na tarehe 27 ni lazima mkaiendeleze historia hiyo”,alisisitiza Dk. Shein.

Akimuelezea mgombea huyo, Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alisema kuwa Ramadhan Hamza Chande anapenda watu wake na ana heshima kwa watu wake na wazee wake na wa wenzake na majirani zake ambaye pia, ana sifa zinazofaa za kuwa Mjumbe wa Jimbo la Jangombe “Hakuna aliyekuwa hana udhaifu kwani hakuna aliyekamilika hata mmoja”alisisitiza Dk. Shein.

Dk. Shein aliwahimiza wanaCCM wa Jimbo hilo kutofanya dharau kwani hakuna dharau katika kuongoza dola hivyo, kuna kila sababu ya kuipa ushindi CCM kwani chama hicho kinataka watu wenye uwezo na kutokana na uwezo alionao Ramadhan Hamza Chande anaweza kuwa Mwakilishi mzuri wa Jimbo hilo.

Dk. Shein alimtambulisha Ramadhan Hamza Chande kwa wanaCCM na wananchi wa Jimbo la Jang’ombe na kuwataka kumchagua mgombea huyo kwani anaijua Ilani ya CCM na ataitekeleza kwa mashirikiano ya viongozi wengine wa chama hicho na mashirikiano ya Serikali kwa jumla.

Nae Ramadhan Hamza Chande alitoa shukurani kwa wanaCCM wote pamoja na wananchi walioshiriki katika Kampeni hizo pamoja na kuwapongeza viongozi wote waliomchagua kuanzia ngazi za chini hadi juu.

Mgombea huyo alimuahidi Rais Magufuli kuwa amekubali kutekeleza Ilani ya Chama hicho na kuahidi kuitekeeleza kwa vitendo na kushirikiana na viongozi wote waliomtangulia.

Aliwataka wanaCCM na wananchi wa Jimbo la Jangombe kumpa mashirikiano ili kuweza kushinda uchaguzi huo huku akiwataka wananchi na wanaCCM wa Jimbo hilo kushirikiana katika kulijenga Jimbo lao hilo la Jang’ombe.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi alieleza mafanikio ya CCM na kusema kuwa mgombea wa CCM nafasi ya Uwakilishi katika jimbo hilo ana sifa zote zinazohitajika hivyo wananchi wanapaswa kumchagua.

Alisema kuwa Kampeni za CCM zimeenda vizuri sana kutokana na viongozi wa Jimbo hilo pamoja na Serikali kutekeleza Ilani ya Uchaguzi wa CCM kwa vitendo.

Alisema kuwa CCM ni chama cheye uwezo, upeo pamoja na kuweza kuwaunganisha watu ili waishi kwa pamoja na ndicho chama pekee kilicholeta maendeleo.

Mamia ya wananchi na wanaCCM walihudhuria katika mkutano huo wa kufunga Kampeni za Uchaguzi wa Jimbo la Jang’ombe  ambapo uchaguzi wa Jimbo hilo  unafanyika baada ya aliyekuwa Mwakilishi wake Abdalla Maulid Diwani kufukuzwa uanachama katika chama hicho.

Viongozi mbali mbali wakiwemo kutoka Tanzania Bara na Zanzibar walitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kutekeleza vyema Ilani ya Uhaguzi ya CCM ikiwa ni pamoja na kuulinda na kuuendeleza Muungano.

Walieleza kuwa kuna sababu nyingi za Kumchagua Ramadhani Hamza Chande na kuichagua CCM kwani mgombea huyo ana uwezo huku wakisisitiza kuimarisha amani na utulivu.

Viongozi kadhaa walihudhuria katika mkutano huo akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, ambapo mkutano huo ulienda sambamba na burudani kutoka  vikundi mbali mbali vikiwemo vya muziki pamoja utenzi Maalum.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.