Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na mgeni wake Mwenyekiti wa Kampuni ya Al Nakhil ya Nchini Dubai, Sheikh Ali Rashid Lootah, aliopofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na Rais wa Zanzibar Dk. Shein leo,3/12/2018.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameikaribisha Kampuni ya Al Nakhil kutoka
nchini Dubai kuitumia fursa ya kuja kuekeza hapa Zanzibar katika sekta ya utalii.
Dk. Shein alitoa maelezo
hayo wakati aliponya mazungumzo na Sheikh Ali Rashid Lootah Mwenyekiti wa
Kampuni ya Al Nakhil kutoka nchini Dubai Ikulu mjini Zanzibar.
Katika mazungumzo hayo,
Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo wa Kampuni kubwa ya ujenzi ya Al Nakhil ya
nchini Dubai kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kutoa
ushirikiano wake mkubwa na kuweka mazingira mazuri katika kuhakikisha azma ya Kampuni
hiyo inafikiwa.
Dk. Shein alimueleza
Mwenyekiti huyo kuwa Zanzibar ina fursa nyingi za uwekezaji katika sekta ya
Utalii na iko tayari kutoa ushirikiano wake kwa Kampuni hiyo hasa ikizingatiwa
kuwa ina uzoefu na uwezo mkubwa katika harakati hizo.
Aidha, Rais Dk. Shein
alimueleza Mwenyekiti huyo juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar katika kuimarisha sekta ya utalii sambamba na hatua zilizofikiwa
katika kuhakikisha idadi ya watalii imeongezeka.
Hivyo, Rais Dk. Shein
aliendelea kusisitiza haja ya kuanzishwa kwa usafiri wa anga hasa kwa kutumia
Kampuni ya ndege ya Emirates ambapo kati ya Zanzibar na Dubai, ambapo hatua
hiyo itaimarisha na kuongeza idadi ya watalii na kuwasaidia wafanyabiashara na
wasafiri wengine.
Alieleza kuwa tayari
makampuni kadhaa ya ndege kutoka nchi mbali mbali duniani yamekuwa yakifanya
safari zake Zanzibar na kusaidia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa sekta ya
utalii hapa Zanzibar, hivyo kuna haja kwa Shirika hilo kufanya safari zake hapa
Zanzibar.
Sambamba na hayo, Rais Dk.
Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi
kwa Mwenyekiti huyo wa Kampuni ya Al Nakhil kwa kuendelea kuiimarisha misikiti
hapa Zanzibar hatua ambayo imewezesha kuikarabati misikiti pamoja na kuijenga
mengine mipya.
Dk. Shein pia, alitoa
pongezi kwa Mwenyekiti huyo kutokana na mapokezi makubwa aliyoyapata yeye na
ujumbe wake wakati walipofanya ziara katika nchi za (UAE) na kutembelea katika
eneo la mradi wa “Palm Jumairah” ambao unasimamiwa na Kampuni hiyo.
Alieleza jinsi hatua za
kuimarisha sekta ya utalii hapa nchini zinaendelea kuimarishwa ambapo pia,
mikakati katika kuendelezwa na kuimarishwa sekta hiyo ilielezwa katika mkutano
wa Uchumi wa Bahari ’Blue Economy’ uliomalizika hivi karibuni mjini Nairobi
nchini Kenya.
Dk. Shein alitumia fursa
hiyo kumueleza Mwenyekiti huyo mikakati ya mashirikiano katika sekta za
maendeleo iliyofikiwa katika mazungumzo kati yake na viongozi wa nchi za Falme
za Kiarabu wakati alipokutana nao katika ziara yake ya nchi za (UAE) mapema
mwaka huu.
Nae, Sheikh Ali Rashid
Lootah Mwenyekiti wa Makampuni ya Al Nakhil kutoka nchini Dubai alipongeza
hatua kubwa za maendeleo zilizofikiwa hapa Zanzibar sambamba na juhudi za
makusudi zilizochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi
wa Rais Dk. Shein katika kuimaisha sekta ya utalii.
Sheikh Ali Rashid Lootah
alitumia fursa hiyo kueleza jinsi alivyoshuhudia ongezeko la ujio wa watalii
hapa Zanzibar na kuahidi kuwa licha ya Zanzibar kujiuza wenyewe kiutalii duniani
lakini pia, atafanya juhudi za makusudi kuitangaza kutokana na fursa za kitalii
zilizopo.
Aidha, alilipokea wazo
la Rais Dk. Shein pamoja na mazungumzo aliyoyafanya na uongozi wa Kampuni ya
ndege ya Emirates ya kufanya safari za ndege hizo kati ya Zanzibar na Dubai
jambo ambalo litaongeza idadi ya watalii sambamba na kuwapa urahisi wafanya
biashara na wananchi wanaosafiri kati ya pande mbili hizo.
Alieleza kuwa kuwepo kwa
mazingira mazuri ya uwekezaji yaliyopo Zanzibar ikiwemo uwepo wa usalama na
amani, ukarimu wa Wazanzibari pamoja na mikakati na Sera za Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya utalii, vyote hivyo vimeivutia
Kampuni yake kuja kuekeza hapa Zanzibar.
Mwenyekiti huyo alieleza
kuvutiwa kwake na hatua za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuweka mradi wa
mji salama katika maeneo ya mji wa Zanzibat ukiwemo Mji Mkongwe ambao ni
kivutio kimoja wapo cha watalii wanaokuja kuitembelea Zanzibar.
Pia, alipokea shukurani
kutoka kwa Dk. Shein kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuiendeleza, kuikarabati na
kujenga misikiti hapa Zanzibar na kuahidi kuendelea kwa lengo la kuiimarisha
Uislamu.
Kampuni ya Nakhil ni
miongoni mwa Kampuni kubwa nchini Dubai ambayo mbali ya ujenzi wa nyumba za
makaazi pamoja na hoteli pia, inahusika na kurejesha ardhi kwa kufukia bahari
ambapo kutokana na usarifu huo imeweza kujenga miradi kadhaa ukiwemo Palm
Island, Dubai Waterfront, Visiwa vya The World, Visiwa vya Universe, Visiwa vya
Jumeirah, ‘Jumerah lake Tower’, ‘Dragon Mart’, ‘Ibn Batuta Mall’ na miradi mengineyo
ambayo ipo nchini humo.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address:
2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment