Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, Afungua Masjid Maryam Mtende leo Wilaya ya Kusini Unguja.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein. akiondoa Kipazia kuashiria kuufungua Msikiti wa Masjid Maryam Mtende kushoto Mfanyabiafhara Maaruf Zanzibar Mfadhili wa ujenzi Msikiti huo, Bw. Said Salim Bakhressa hafla hiyo imefanyika katika Kijiji cha Mtende Mkoa wa Kusini Unguja leo.5-4-2019. 

Na .Abdi Shamna Ikulu.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amewataka waumini wa Dini ya kiislamu nchini kujiepusha na migogoro katika kusimamia uendeshaji wa huduma za misikiti na badala yake waifanye kuwa chemchem ya kutoa elimu ya dini kwa kuzingatia misingi ya Masheikh mashuhuri wa Zanzibar waliotangulia.

Dk. Shein amesema hayo huko Mtende, Mkoa wa Kusini Unguja, katika hafla ya ufunguzi wa msikiti “Masjid Maryam”, uliojengwa kwa msaada wa mhisani.

Alisema mizozo, migogoro, fujo na mapambano hayapaswi kupangwa wala kutekelezwa kwenye misikiti, akibainisha kuwa misikiti ni nyumba ya Mwenyezi Mungu na sehemu tukufu kwa waislamu kufanya ibada.

Alisema kwa mnasaba huo na kwa lengo la kumcha Mwenyezi Mungu, ndio sababu wahisani huamuwa kuchangia uimarishaji wa nyumba za Mwenyezi Mungu , hivyo akawataka waislamu wa kijiji cha Mtende kuendelea kuwa wamoja na kupendana.

Aidha, aliutaka uongozi wa msikiti huo kupitia  Ofisi ya Mufti wa Zanzibar kuchukuwa hatua za haraka kusawazisha pamoja na kuitafutia suluhu migogoro  itayojitokeza kwa mujibu wa sheria na taratibu za dini, kupitia Quraan na hadithi za Mtume Muhammad (SAW).

“Msikiti pawe ni sehemu muhimu ya kuhimizana umuhimu wa kuitunza amani iliyopo na kujitahidi kufuata maadili mema”, alisema.

Dk. Shein, aliwataka waumini watakaopewa dhamana ya kuusimamia msikiti huo kufanya uadilifu na kujipambanuwa kwa sifa njema, sambamba na kujiepusha na mambo yote ambayo Mtume ameasa kuepukwa.

“Nimefurahishwa sana na risala yenu na nakupongezeni kwa kueleza bayana na kutuhakikishia kuwa uongozi wa msikiti huu hautakaribisha mizozo kama inavyojitokeza katika baadhi ya misikiti”, alisema.

Rais Dk. Shein aliitaka Kamati inayosimamia msikiti huo kuweka mikakati pamoja na mipango madhubuti  iliyo endelevu ili kuhakikisha msikiti na madrasa iliopo inakuwa chimbuko la kuwapata maulamaa na masheikh wapya.

“Tunataka tuwapate kina marehemu Sheikh Juma Baraka wengine wa Mtende, naamini Mwenyezi Mungu atatupa uwezo wa kuwapata masheikh wapya watakaotokea hapa”, alisema.

Vile vile, aliwahimiza wazazi na walezi  wa kijiji hicho na vyengine jirani kusimamia vyema maendeleo ya elimu ya vijana wao, akinasibisha kauli yake na matokeo yasioridhisha ya Skuli ya Mtende katika mitihani ya Taifa, mwaka uliopita.

“Nakuhimizeni mtumie fursa na namna mnavyoshirikiana pamoja na umoja mlionao kuzitafutia ufumbuzi  changamoto zote zinazosababisha vijana wenu wasipate matokeo mazuri katika mitihani yao ya Taifa”, alisema.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwataka wazee wa kijiji hicho na vyengine jirani kutumia vyema fursa ya kufunguliwa msikiti huo wenye madrasa kujiongezea maarifa katika masuala ya dini ili waweze kufanya ibada kwa usahihi.

Alisema ujenzi wa Msikiti huo na hatua ya maendeleo yake umezingatia suala zima la kuendeleza elimu, ikiwa ndio msingi wa mambo yote sambamba na kumuongoza binadamu kupata mafanikio na maisha mema.

“Elimu ndio nyenzo inayomuwezesha muumini kutekeleza vyema ibada zake na kuishi katika uchamungu”, alisema.

Dk Shein alieleza kuwa  kitendo cha waumini kutowa sadaka ni miongoni mwa ibada muhimu zilizohimizwa katika Qoraan na hadithi za Mtume Muhammad (SAW), ambapo Mwenyezi Mungu amewahakikishia malipo makubwa waumini wanaotekeleza ibada hiyo.

Alisema kupitia Aya za Suratul Hadyd Mwenyezi Mungu amebainisha kumuongeza baraka zaidi mja anaetowa, ambapo faida zake huonekana duniani na kesho mbele ya haki, hivyo akamuombea malipo mema mhisani aliefadhili ujenzi huo.

Katika hatua nyengine, Dk. Shein aliwapongeza wananchi wa kijiji cha Mtende kwa kuwa wamoja na kuendeleza ushirikiano na Serikali, hatua iliyowawezesha kupata maendeleo makubwa katika huduma mbali mbali za kijamii, ikiwemo  miundombinu bora ya barabara.

“Mtende hivi sasa inafikika kirahisi kwa kuwa na barabara nzuri ya lami na watu wanafaidika na huduma za umeme, huduma za Afya na elimu ya maandalizi”, alisema.

Kuhusiana na changamoto za upatikanaji wa huduma za maji safi na salama , Dk. Shein alisema changamoto hiyo imechangiwa kwa kiasi kikubwa na ongezeko la kiwango cha chumvi katika pango la Chau ambalo ni tegemeo la huduma hiyo kwa muda mrefu.
Alisema kupitia mradi wa uchimbaji wa visima wa Ras Al Khaimah , tayari kisima kimoja kipya kimechimbwa katika kijiji hicho.

Aidha, alisema Serikali ya  Mapinduzi ya Zanzibar imejenga tangi jipya la maji lenye uwezo wa kuhifadhi lita 120,000 kwa ajili ya matumizi ya wananchi wa shehiya hiyo na kubainisha kuwa miundombinu ya umeme na mabomba inatarajiwa kuungwa hivi karibuni.    

“Nakuombeni muendelee kuwa na subira, kwani wazee walisema ‘subira huvuta kheir’, nina imani jitihada zetu zitafanikiwa na kheri itapatikana kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu kabla ya kumalizika mwaka huu”, alisema.

Mapema,  Sheikh Khamis Ramadhan, akisoma risala ya wananchi wa Mtende, alisema ujenzi  wa msikiti huo umewapunguzia masafa ya kufuata eneo la ibada waumini wa karibu na kitongoji hicho na hivyo kupata fursa nzuri ya kufanikisha ibada zao.

Alimpongeza mfadhili wa ujenzi wa msikiti huo Sheikh Said Salim Bakhresa kwa imani na mapenzi makubwa aliyonayo kwa wananchi wa kijiji hicho na kufadhili ujenzi huo.

Katika hatua nyengine, wananchi wa Mtende wamepongeza mafanikio makubwa  ya kiuchumi na kijamii yaliofikiwa na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, awamu ya saba chini ya uongozi wa Dk. Shein.

Aidha, walipongeza juhudi zinazochukuliwa na serikali katika kuitafutia ufumbuzi wa kudumu changamoto ya maji safi na salama inayokabili kijiji hicho.

Nae, Mufti Mkuu wa Zanzibar, Sheikh Saleh Omar Kabi, aliwataka waumini wa msikiti huo kuutunza, sambamba na kuwaendeleza watoto kitaaluma, akibainisha hatua hiyo yaweza kuwa sababu ya kupatikana imani na upendo miongoni mwao.

Aidha, alisema ni fahari kubwa kwa watu wa Mtende kupata msikiti huo na kufunguliwa na kiongozi mkuu wa nchi, hivyo akawataka waumini hao kuutumia kwa ajili ya kuwaunganisha.

 Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.