Habari za Punde

Rais wa Zanzibaer na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein Akisoma Risala ya Kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhini na Kuwataka Wafanyabiashara Kutoongeza Bei Katika Bidhaa Mbalimbali.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein, akitowa Risala ya Kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Mfungo wa Ramadhani unaotaraji kuaza wiki ijayo. Waumini wa Dini ya Kiislamu Duniani hujumuika katika Mfugo huo ikiwa ni moja ya Ibada ya Kiislam 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein amewanasihi wafanyabiashara kuwa waadilifu katika kuwafanyia wanunuzi tahafifu za bei za bidhaa na huduma nyenginezo hasa katika mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Alhaj Dk. Shein aliyasema hayo katika risala maalum aliyoitoa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari katika kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani katika mwaka huu wa 1440 Hijria sawa na mwaka 2019 Miladia.

Katika risala yake hiyo, Alhaj Dk. Shein aliwataka wafanyabiashara kukumbuka kwamba kwa kufanya hivyo hawatokula hasara bali watazidi kupata fadhila mbali mbali za Mola wao Mlezi zinazoambatana na Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Aliwataka wafanyabiashara kuzingatia ubora wa bidhaa wanazowauzia wananchi kwani wanapaswa wahakikishe kwamba wanawauzia bidhaa ambazo hazijapita muda wake wa matumizi.

Kwa msingi huo Alhaj Dk. Shein alieleza kuwa wanunuzi nao wanatakiwa wawe makini wanaponunua bidhaa kwani si jambo la busara kununua bidhaa iliyokwisha muda wake wa matumizi kwa kufuata urahisi wa bei kwa sababu urahisi huo ni gharama kubwa kwa afya zao.

Aidha, aliwataka wakulima waendelee na ustaarabu pamoja na utamaduni wao ule ule wa ustahamilivu na uadilifu kwa kujiepusha na tabia ya uvunaji na uuzaji wa mazao machanga.

Alhaj Dk. Shein aliwataka wauzaji wa bidhaa mbali mbali kama vile matunda, samaki, mboga na nyenginezo waache ile tabia ya kuuza bidhaa zao maeneo ya barabarani au kuziweka chini bila hata ya kutandika kitu kilicho safi.


Alisisitiza kwamba wafanyabiashara ni lazima wafahamu kwamba kufanya biashara bila ya kuzingatia taratibu zilizowekwa kunaweza kuhatarisha usalama wa wapitao njiani, kuathiri ubora wa bidhaa hizo pamoja na afya za watumiaji wa bidhaa hizo.

Rais Dk. Shein aliongeza kuwa lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar si kumkomoa mtu kwa sababu Serikali huwa haiwakomoi wananchi wake bali dhamira yake ni kuwalinda na kuona kwamba hawafikwi na matatizo ambayo yanaweza kuepukika na kujikinga nayo.

Aidha, Rais Dk. Shein alizitaka Taasisi zinazohusika zisimamie vyema shughuli za biashara masokoni na madukani, ili vitendo vya ghilba kwa wananchi ambao ndio wanunuzi na watumiaji wakubwa wa bidhaa visiendelee.

Alisisitiza kuwa mwezi wa Ramadhani ni mwezi wa kuoneana huruma na kufanyiana hisani kwa hivyo wananchi wazidishe imani na huruma ili waweze kuitekeleza ibada ya saumu bila ya bughudha na usumbufu.

Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein alitoa nasaha zake kwa wale ambao si Waislamu na wale ambao watakuwa na dharura zinazowazuwia wasifunge kuwa wasifanye vitendo vitakavyoathiri wanaofunga.

Alieleza kuwa huduma zote muhimu pamoja na zile zinazotolewa kwa wageni hasa watalii ziendeshwe kwa kuzingatia misingi ya kuwaheshimu ndugu zao wanaofunga na kuuheshimu Mwezi Mtukufuwa Ramadhani,

Alhaj Dk. Shein alisisitiza haja ya kuhimizana zaidi kuisoma Qur-an kwa wingi ndani ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani pamoja na kujitahidi kufahamu mantiki ya maelekezo yake.

Aliwataka waumini kuhimizana kuhudhuria darsa katika misikiti ndani ya mwezi wa Ramadhani na kuepuka kutumia muda kwa kufanya mambo yasiyo na manufaa katika mwezi huo ambayo yanapingana na mafunzo ya Uislamu na silka zao.

“Huu ni mwezi ambao umepewa daraja kubwa ya utukufu na Mwenyezi Mungu (S.W) kwa sababu ndani yake kuna mambo matukufu……ni mwezi ambao ibada za waja hulipwa fadhila nyingi kuliko katika kiezi mingine”,alisisitiza Alhaj Dk. Shein.

Kadhalika Alhaj Dk. Shein aliiagiza Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati na uongozi wa Mamlaka ya Maji (ZAWA) kuhakikisha kuwa ule utaratibu wa kila mwaka wa kusambaza maji unatekelezwa katika maeneo yenye shida ya maji na ambayo bado huduma hiyo haijafika Unguja na Pemba.

Pia, Alhaj Dk. Shein aliziagiza Taasisi zote zinazohusika zikiwemo Mabaraza ya Manispaa, Mabaraza ya Miji na Halmashauri zote za Wilaya Ungua na Pemba ziyasimamie ipasavyo majukumu yao ya kudumisha usafi katika miji na vijiji pamoja na shughuli zote za kiuchumi na kijamiizinazofanywa katika Mwezi huo mtukufu.

Alisisitiza kuwa utaratibu wa kufutari kwa pamoja ni vyema ukafanywa kwa kuzingatia sana masuala ya usafi pamoja na kufuata maelekezo kutoka kwa wataalamu wa afya na usafi wa mazingira.

Alhaj Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza jinsi uchumi wa Zanzibar ulivyoimarika ambapo kwa mwaka wa fedha 2017-2018 uchumi ulikuwa kwa kasi ya asilimia 7.1 sambamba na kushuka kwa mfumko wa bei kutoka kasi ya 5.6 mwaka 2017-2018 hadi kufikia asilimia 3.9 mwaka 2018-2019.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwatakia kila la heri Wajumbe wote wa Baraza la Wawakilishi wakiongozwa na Spika Zubeir Ali Maulid katika Mkutano wao wa 14 wa Baraza la Tisa la Wawakilishi utakaojadili Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha wa 2019-2020.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.