Habari za Punde

Wafanyabiashara Zanzibar Watakiwa Kutopandisha Bidhaa Wakati Huu wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.

Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja Mhe. Ayoub Mohammed Mahmoud akizungumza na kutowa shukrani kwa niaba ya Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, wakati wa hafla ya futari ilioandaliwa na Benki ya Watu wa Zanzibar kwa Wateja wao na Wananchi wa Zanzibar katika ukumbi wa Hoteli ya Verde Mtoni Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein ameendelea kuwasisitiza wafanyabiashara kutowauzia wananchi bidhaa kwa bei ya juu katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhani na miezi ijayo.

Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya Rais Dk. Shein, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharii Ayoub Mahamoud aliyasema hayo katika futari maalum iliyoandaliwa na Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Verde Mtoni, Mjini Zanzibar.

Katika maelezo ya shukurani hizo Rais Dk. Shein aliwataka wananchi kutokwenda kinyume na maagizo yake aliyoyatoa katika hotuba yake aliyoitoa kwa wananchi katika kuukaribisha mwezi wa Ramadhani mwaka huu kwa kuwanasihi kutouza bidhaa zao kwa bei ya juu hasa mwezi huu wa Ramadhani.

Aliongeza kuwa kuuza bidhaa kwa bei ya juu kutawapelekea wananchi kupata usumbufu mkubwa katika kutekeleza ibada yao ya funga hivyo, aliwataka wafanyabiashara kutofanya vitendo hivyo kwa mwezi huu wa Ramadhani na miezi ijayo hasa ikizingatia pia, mwezi ujao kuna Sikukuu ya Idd Fitr ndani yake.

Aidha, Rais Dk. Shein aliendelea kuwasisitiza wafanyabiashara kutowauzia wananchi bidhaa zilizopitwa na muda pamoja na bidhaa ambazo hazijafika muda wa kuliwa hasa mazao ya chakula ili kuendelea kuupa heshima mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwataka wananchi wa Zanzibar kuendelea kuitumia hiyo Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) kwani ni benki ya Serikali pamoja na kuendelea kufungua hesabu zao kwa huduma za Kiislamu na zisizo za Kiislamu.

Rais Dk. Sheim pia, alitumia fursa hiyo kutoa pole kwa wale wote waliopata athari za mafuriko ya mvua za masika zinazoendelea hapa nchini.

Pia, aliwataka wananchi wa Zanzibar kuendeleza umoja na mshikamano ambao utadumisha amani na utulivu uliopo nchini ili maendeleo zaidi yazidi kupatikana.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa Benki hiyo kwa juhudi zake kubwa inazoendelea kuzichukua katika kutoa huduma bora kwa wananchi na kusisitiza haja ya kuziendeleza zaidi  ili zizidi kuleta tija na maendeleo kwa nchi na wananchi wake.

Mapema, Mjumbe wa Kamati ya Sheria ya Benki hiyo ambaye pia, ni Katibu wa Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana Sheikh Abdallah Talib alitoa shukurani kwa Benki hiyo kwa kuendeleza utamaduni wa kuwafutarisha wananchi wakiwemo wateja wao na kueleza kuwa kitendo hicho cha heri kinaleta mapenzi makubwa ndani yake.

Sheikh Abdallah Talib alieleza kuwa kitendo hicho cha kufutarisha kilichofanywa na Benki hiyo ya Watu wa Zanzibar kinaonesha alama ya watu walio wema sambamba na kuonesha jinsi Benki hiyo ilivyokuwa karibu na inavyowajali wateja wake.

Katika hafla hiyo ya futari viongozi mbali mbali walihudhuria akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid na viongozi wengine wa dini na Serikali pamoja na wananchi mbali mbali wakiwemo wateja wa Benki hiyo.

Leo Alhaj Dk. Shein anatarajia kuungana pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja katika futari maalum aliyowaandalia.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.