Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Amtumia Salamo za Pongezi Rais Wa Djibout Ismail Omar Guelleh.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein amemtumia salamu za pongezi Rais wa Djibout, Ismail Omar Guelleh kwa kutimiza miaka 42 tokea Taifa hilo kupata uhuru wake.

Salamu hizo zilieleza kuwa wananchi wa Zanzibar wanaungana na ndugu zao wa Djibout katika kusherehekea siku hii adhimu  kwa Taifa hilo.

“Kwa niaba yangu binafsi, watu wa Zanzibar na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar natumia fursa hii kukupongeza wewe pamoja na wananchi wote wa Djibouti kwa kutimiza miaka 42 ya uhuru”, ilieleza sehemu ya salamu hizo alizotuma Dk. Shein.

Aidha, katika salamu hizo, Dk. Shein alimuhakikishia Rais Guelleh kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano mkubwa uliopo kati yake na Djibout sambamba na kuimarisha maeneo mapya ya mashirikiano kama walivyokubaliana na Rais huyo wa Djibout wakati wa ziara yake aliyoifanya mnamo mwaka 2017.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein katika salamu hizo alieleza kuwa miaka 42 ya uhuru wa Taifa hilo inaimarisha zaidi mashirikiano kati ya nchi mbili hizo pamoja na watu wake.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia nafasi hiyo kumtakia uongozi mwema Rais Ismail Omar Guelleh pamoja na kusherehekea vyema siku hii adhimu kwa Taifa hilo sambamba na kuendelea kuliongoza kwa amani na utulivu mkubwa kwa maendeleo endelevu ya wananchi wa Djibout.

Djibout ilipata uhuru wake mnamo tarehe 27 Juni mwaka 1977 kutoka koloni la Ufaransa chini ya Jemedari wake Hassan Gouled Aptidon ambaye alikuwa Rais wa kwanza wa Djibout.

Wakati huo huo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein amemtumia salamu za pongezi Rais wa Msumbuji, Felipe Nyusi kwa kutimiza miaka 44 tokea kupata Uhuru kwa Taifa hilo.

Salamu hizo zilieleza kuwa kwa niaba yake Dk. Shein, wananchi pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wanaungana pamoja na ndugu zao wa Msumbuji katika kusherehekea siku hiyo adhimu ya uhuru wa Taifa hilo.

Aidha, katika salamu hizo, Dk. Shein alimuhakikishia Rais Nyusi kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano mkubwa uliopo kati yake na nchi hiyo sambamba na kuimarisha udugu uliopo kati ya wananchi wa pande mbili hizo.

Pia, salamu hizo zilieleza namna ya Zanzibar itakavyoimarisha ushirikiano uliopo kati yake na Msumbuji kwa kukuza uhusiano mwema wa kikanda na kimataifa.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumtakia Rais Nyusi afya njema yeye na familia yake na kumtakia maisha marefu yenye furaha pamoja na sherehe njema ya siku hiyo adhimu ya uhuru wa Taifa hilo kwa amani, utulivu na upendo kwa maendeleo endelevu ya wananchi wa Msumbiji.

Msumbiji ilipata uhuru wake Juni 25 mwaka 1975 kutoka kwa koloni la Ureno chini ya Jemedari wake Samora Machel.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.