Habari za Punde


SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinaendelea kuchukua hatua za kisera na za kimkakati katika ujenzi wa uchumi wa viwanda  ili Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ifikie hadhi ya nchi ya uchumi wa kati.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ameyasema hayo leo katika ufungaji wa Maadhimisho na Maonesho ya Nne ya wiki ya Viwanda ya Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere, jijini Dar-es-Salaam.
Katika hotuba yake, Rais Dk. Shein alisema kuwa utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo miradi ya umeme, barabara, reli, bandari na viwanja vya ndege unalenga katika kujenga misingi imara ya ukuaji wa sekta ya viwanda na biashara ambazo muhimu katika kutatua changamoto za ajira na kuongeza kasi ya uchumi.
Aliongeza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinaendelea kuimarisha sekta binafsi kwa lengo la kuhakikisha kwamba inaongeza fursa za ajira kwa vijana wanaomaliza masomo yao kwa ngazi zote.
Alieleza kuwa maonesho hayo aliyoyafunga yamesaidia na yatakuwa na mchango mkubwa katika utekelezaji wa mipango na mikakakti iliyopo ya kuleta mageuzi makubwa ya uchumi wa viwanda katika nchi zote 16 wanachama wa SADC.
Alisema kuwa taaluma, ujuzi na maarifa yaliyopatikana katika maadhimisho na maonesho hayo itatumika katika kukuza ubunifu wa kuendeleza viwanda, utafutaji wa masoko pamoja na kukuza uhusiano baina ya wazalishaji, wanunuzi, wasafirishaji na watumiaji bidhaa zinazozalishwa na viwanda vya nchi wanachama wa SADC.
Rais Dk. Shein alisema kuwa kauli mbiu ya Maadhimisho na Maonyesho ya SADC  mwaka huu 2019 ambayo imeweka msisitizo katika mazingira ya viwanda inakwenda sambamba na juhudi zinazochukuliwa za kuimarisha viwanda na Serikali zote mbili.
Alieleza matumaini yake kwamba maazimio yote yaliyofikiwa kwa pamoja katika vikao hivyo yatafanyiwa kazi na Sekretarieti ya SADC kwa kushirikiana na nchi wanachama na yawe msingi na kichocheo cha mafanikio ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa kikanda na nchi wanachama.
Alisema kuwa kazi iliyo mbele hivi sasa ni kuhakikisha kwamba kila mmoja anaunga mkono utekelezaji wa maazimio yaliyopitishwa katika vikao vilivyofanyika pamoja na mikakati ya Serikali zote ya kuendeleza viwanda kwa kununua na kuzipenda bidhaa za viwanda vya ndani ya nchi za SADC.
 “Tujenge utamaduni wa kuwapenda na kuwatumia wataalamu wetu wa ndani na tuondokane na utegemezi wa wataalamu wa nje, sambamba na kujenga misingi imara ya kuendeleza teknolojia yetu wenyewe”,alisema Dk. Shein.
Aidha, alisema kuwa kufanya hivyo ni kutafsiri kivitendo ile dhamira ya nchi wanachama wa SADC kuunda umoja wa SADC kwa ajili ya kuongeza fursa ya masoko na ajira.
Rais Dk. Shein alisema kuwa nchi wanachama wa SADC wataweza kuongeza masoko ya ajira ikiwa zitanunua bidhaa zinazozalishwa na wataalamu wazalendo.
Kwa msingi huo Rais Dk. Shein alisisitiza haja na umuhimu wa kuzingatia falsafa na hekima za Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, Rais wa Kwanza wa Zanzibar kwa kuzingatia maneno aliyoyasema kwamba ”Tukuza kilicho chako hadi usahau cha mwenzako”.
“Wakati umemfika wa kuhakikisha kwamba tunapenda kuzitumia bidhaa zinazozalishwa na viwanda vyetu wenyewe”,alisisitiza Dk. Shein.
Vile vile, Rais Dk. Shein alitoa shukurani za dhati kwa wanahabari wa vyombo vyote ambao kwa muda wa wiki nzima walikuwa wakifanya kazi muhimu sana ya kuwapa habari wanachi kwa kutangaza na kuhamasisha wananchi kuhusu matukio yote muhimu ambayo yalikuwa yakifanyika katika viwanja hivyo.

Dk. Shein pia, alitoa shukrani wka wenye viwanda katika nchi za Jumuiya ya SADC kutokana na juhudi kubwa wanazizifanya katika kuongeza utengenezaji wa bidhaa za viwandani ikiwa ni pamoja na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo,mifugo, uvuvi, uchimbaji madini na utengenezaji wa mashine na mitambo ya ain azote.

Alisisitiza kuwa fursa ya kuimarisha ushirikiano waliyoipata katika maadhimisho na maonesho hayo lazima iendelezwe katika nyanja zote za kiuchumi na kijamii, ili kuifanya Jumuiya ya SADC kuwa imara zaidi na yenye nguvu kubwa katika masula muhimu ya kikanda na Kimataifa.

Dk. Shein alilipongeza wazo la kuifanya lugha ya Kiswahili kuwa ni miongoni mwa lugha rasmi za mawasiliano katika majukwaa ya SADC kwani ni hatua muhimu katika kuimarisha umoja na mshikamano kwa Wanachama wa Jumuiya hiyo.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwaalika washiriki wa mkutano huo wa SADC katika maonyesho makubwa yaualii ya Zanzibar “Zanzibar Tourism show” yatakayofanyika mwishoni mwa mwezi wa Septemba, 2019.

Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa wanachama wan chi za SADC kutochukua muda wa kukutana kwani hatua hiyo inapunguza nguvu za hamasa ya kuwa pamoja kidugu katika shughuli za Jumuiya hiyo kwa maslahi ya nchi hizo na bara zima la Afrika.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.