Habari za Punde

SMZ Itaendelea Kuimarisha Ujenzi wa Majengo ya Kisasa Zanzibar.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Shaaban Seif Mohamed akifanya ziara ya ghafla kwenye Ofisi Kuu ya Tume ya Kitaifa ya Kudhibiti na Uratibu wa Dawa ya kulevya Kidongo chekundu.
Na.Othman Khamis OMPR.                                                                                             
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itaendelea kuimarisha miundombinu katika ujenzi wa majengo ya kisasa kwa lengo la kuwawezesha watendaji wake kufanya kazi katika mazingira wezeshi yanayoendana na wakati wa sasa wa sayansi na teknolojia.
Kufanya hivyo ni kuendeleza dhana ya serikali ya kutoa huduma bora kwa wananchi wake sambamba na kuongeza ufanisi kwa watumishi wa umma katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku wanapokua katika sehemu zao za kazi.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Raiswa Zanzibar  Ndugu Shaban Seif Mohamed alieleza hayo wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika Tume ya usimamizi na uratibu wa madawa ya kulevya ikiwa ni muendelezo wa ziara zake za  kukagua taasisi anazozisimamia zilipo chini ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais zilizopo eneo la Kidonge Chekundu.
Nd. Shaaban alisema ziara yake kwenye taasisi hiyo imemuwezesha kujionea hali halisi ya  watendaji hao kufanya kazi katika mazingira magumu.  Hivyo Uongozi wa Wizara  una wajibu wa kuangalia namna gani unaweza kuipatia ufumbuzi changamoto hiyo.
Aliwataka watendaji hao kuendelea kuvuta subra katika kutoa huduma kwa mujibu wa mazingira walionayo huku serikali ikiendelea kutafuta eneo jengine mbadala kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi mbali mbali kwa zile taasisi ambazo bado zinakabiliwa na changamoto hiyo.
“ Ili Mfanyakazi afanye kazi vizuri anahitaji apate sehemu yenye mazingira mazuri ya kufanyia kazi” Alieleza Katibu Mkuu
Nae Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kitaifa ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa ya kulevya Bi heriyangu  M. Khamis alimueleza Katibu Mkuu ingawaje tume hiyo inakabiliwa na changamoto ya mazingira ya kufanyia kazi lakini watendaji wake wanaendelea kufanya kazi kwa uwadilifu bila ya kukata tamaa.
Alisema kutokana na changamoto inayowakabili imelazimika kulisanifu jengo walilonalo ili liweze kukidhi haja kwa wafanyakazi walikuwepo hali iliyopelekea kila mfanyakazi kupata sehemu ya kufanya kazi zake lakini jitihada za kuwapatia eneo jengine bado zinahitajika.
“Urefu wa jengo letu haukidhi haja kwani hauruhusu hewa safi kuingia ndani kama inavyosatahiki”. Alisema Mkurugenzi Heriyangu.
Akizunngumzia suala la utendaji kazi Mkurugenzi Heriyangu alisema Tume inafanya kazi zake kwa umahiri na umakini katika kuisaidia jamii kuachana na vitendo viovu vya utumiaji wa dawa za kulevya sambamba na kuzuia dawa hizo kuingizwa nchini.
Alisema Ofisi hiyo  tayari imeandaa maandiko mbali mbali yenye mapendekezo na karibuni yatawasilishwa wizarani kwa ajili ya kujadiliwa ili kupata ufumbuzi wa kujengwa kwa majengo mapya ya Ofisi hizo.
Mapema Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Shaaban Seif  Mohamed alifika eneo la Mwanakwerekwe kukagua maendeleo ya ujenzi wa Ofisi za idara  ya sherehe na maadhimisho ya  kitaifa unaoendelea.
Wakati akikagua maendeleo ya ujenzi huo Katibu Shaaban ametoa maelekezo ya kufanyiwa marekebisho katika baadhi ya sehemu ili kuimarisha ulinzi na usalama wa Ofisi hiyo akitolea mfano kuwekwa kwa madirisha na milango imara kwa chumba cha kuhifadhia stakabadhi muhimu za Ofisi.
Katika ziara hiyo katibu mkuu alipata fursa ya kukagua milango ya duka ambayo inamilikiwa na idara hiyo pamoja na mambo mengine  itasaidia kuiingizia kipato Idara ya sherehe.
Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kitaifa ya Kudhibiti na Uratibu wa Dawa ya kulevya Bibi Heriyangu Khamis akimueleza Katibu Mkuu Shabaan majukumu ya watendaji wake licha ya ufinyu wa Ofisi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kitaifa ya Kudhibiti na Uratibu wa Dawa ya kulevya Bibi Heriyangu Khamis akimueleza Katibu Mkuu Shabaan majukumu ya watendaji wake licha ya ufinyu wa Ofisi.
Mkurugenzi wa Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa Bi.Riziki Daniel Yussuf akimuelezea Katibu Mkuu Shaaban hatua ya ujenzi wa Ofisi ya Idara hiyo hapo Mwanakwerekwe.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Shaaban Seif Mohamed akiuagiza Uongozi wa Idara ya Sherehe kufanya marekebisho katika baadhi ya sehemu za Ofisi hiyo ili kwenda na mazingira sahihi ya eneo hilo.

Picha na – OMPR – ZNZ.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.